Yeremia 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yeremia anahubiri katika hekalu

1Yawe akamutolea Yeremia ujumbe, akisema: Kwenda kusimama

2kwenye mulango wa hekalu lake na kutangaza ujumbe huu: Musikilize neno la Yawe enyi watu wa Yuda munaoingia humu kwa kumwabudu Yawe.

3Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Mugeuze mwenendo wenu na matendo yenu, nami nitawaacha muendelee kukaa pahali hapa.

4Musitumainie maneno haya ya udanganyifu mukisema: Hili ni hekalu la Yawe, hekalu la Yawe, hakika hili ni hekalu la Yawe.

5Lakini mugeuze mwenendo wenu na matendo yenu. Mufuate sheria yangu kati yenu.

6Musiwatese wageni, wayatima au wajane au kuwaua watu wasiokuwa na kosa katika inchi hii. Musijiangamize wenyewe kwa kuabudu miungu mingine.

7Mukifanya hivyo, mimi nitawaacha mukae siku zote pahali hapa, katika inchi niliyowapa babu wenu tangu zamani.

8Lakini kumbe, munatumainia maneno ya udanganyifu yasiyokuwa na faida kwenu.

9Munaiba, munaua, munafanya uzinzi, munaapa kwa uongo, munamufukizia mungu Bali ubani na kuabudu miungu mingine ambayo hamujapata kuijua.

10Kisha, mutakuja na kusimama mbele yangu katika hekalu hili linalojulikana kwa jina langu na kusema “Tuko salama”, ingawa munaendelea kufanya mambo hayo yanayonichukiza.

11Munazani kwamba hekalu hili linalojulikana kwa jina langu limekuwa kimbilio la wanyanganyi? Mujue kwamba mimi nimeona yote munayofanya!

–Ni ujumbe wa Yawe.–

12Muende kwenye pahali pangu kule Shilo, nafasi nilipochagua kwa kuabudiwa mara ya kwanza, muone maangamizi niliyofanya kule kwa sababu ya uovu wa watu wangu, Israeli.

13Ninyi mumefanya mambo hayo yote.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Na hata niliposema nanyi tena na tena hamukunisikiliza. Nilipowaita hamukuitika.

14Kwa hiyo, kama vile nilivyoutendea muji wa Shilo, ndivyo nitakavyolitendea hekalu hili linalojulikana kwa jina langu, hekalu ambalo ninyi munalitegemea; ndiyo pahali hapa ambapo niliwapa ninyi na babu zenu.

15Nitawafukuza ninyi mbali nami kama nilivyowatupilia mbali wandugu zenu, wote wa uzao wa Efuraimu.

Kutokutii kwa watu

16Nawe Yeremia, usiwaombee watu hawa, usinililie kwa ajili yao, usinililie kwa ajili yao wala kunisihi kwa ajili yao, maana sitakusikiliza.

17Wewe hauoni mambo wanayofanya katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema?

18Watoto wanaokota kuni, wababa wanawakisha moto na wamama wanaponda unga kwa ajili ya kutengeneza mikate ya kumutambikia mungu wa kike, wanayemwita malkia wa mbinguni. Tena wananikasirikisha kwa kuitolea miungu mingine sadaka ya divai.

19Lakini ni nani wanayemukasirikisha? Mimi? Hata kidogo! Wanajikasirikisha wao wenyewe na kujifezehesha!

–Ni ujumbe wa Yawe.

20Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitaimwanga hasira yangu juu ya pahali hapa, juu ya wanadamu na nyama, miti katika mashamba na juu ya mazao ya inchi. Nayo nafasi hii itawaka moto wala hautaweza kuzimishwa.

21Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Muongeze sadaka zenu za kuteketezwa kwa moto juu ya sadaka zenu zingine, nanyi mujikulie nyama zile!

22Maana, siku nilipowaondoa babu zenu katika inchi ya Misri, sikuwaambia kitu wala kuwapa amri yoyote juu ya sadaka za kuteketezwa na sadaka zingine.

23Lakini niliwapa amri kwamba waitii sauti yangu kusudi nikuwe Mungu wao, nao wakuwe watu wangu. Niliwaamuru vilevile waishi kama nilivyowaagiza, kusudi wapate uheri.

24Lakini wao hawakunitii wala kunitegea sikio. Lakini wakafuata mashauri yao wenyewe na ugumu wa mioyo yao, wakarudi nyuma pahali pa kusonga mbele.

25Tangu siku ile babu zenu walipotoka Misri mpaka leo, sikuchoka kuwatuma kwenu manabii wote, watumishi wangu.

26Lakini hawakunisikiliza wala kunitegea sikio, lakini wakazidi kufanya vichwa vyao kuwa vigumu na kuasi kuliko hata babu zenu.

27Sasa wewe Yeremia utawaambia maneno haya yote, lakini wao hawatakusikiliza. Utawaita, lakini hawatakuitikia.

28Basi utawaambia: Ninyi ni taifa ambalo halikutii sauti ya Yawe, Mungu wao, wala kukubali maonyo yake. Kwenu uaminifu umekufa; umetoweka kabisa katika vinywa vyenu.

Maovu katika Bonde la Hinomu

29Munyoe nywele zenu na kuzitupa, enyi wakaaji wa Yerusalema:

mufanye maombolezo juu ya vichwa vya milima,

maana, mimi Yawe nimewakataa ninyi,

nimewatupilia ninyi kizazi kilichosababisha hasira yangu!

30Watu wa Yuda wametenda maovu mbele yangu. Wameweka sanamu zenye kuchukiza ndani ya nyumba hii inayojulikana kwa jina langu na kuichafua.

31Wamejenga mazabahu inayoitwa “Tofeti” huko kwenye bonde la Mwana wa Hinomu, kwa kuwatolea wana na wabinti kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Mimi sikukuwa nimewaamuru kufanya jambo hilo, wala halikunifikia katika mafikiri.

32Kwa sababu hiyo, siku zinakuja ambapo hawataliita tena “Tofeti”, au “bonde la Mwana wa Hinomu”, lakini wataliita “bonde la Mauaji”.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Huko ndiko watakakozika watu, kwa sababu hapatakuwa pahali pengine pa kuzikia.

33Maiti za watu hao zitakuwa chakula cha ndege na nyama wa pori, na hapatakuwa mutu atakayewafukuza.

34Inchi itakuwa jangwa na katika miji ya Yuda na barabara za Yerusalema nitakomesha sauti zote za furaha na shangwe, nazo nyimbo za wenye kufanya ndoa, kwa sababu inchi itakuwa ukiwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help