Zaburi 115 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu mumoja wa kweli

1Si sisi, ee Yawe, si sisi;

lakini wewe peke yako utukuzwe,

kwa ajili ya wema na uaminifu wako.

2Kwa nini mataifa yanasema:

“Mungu wenu yuko wapi?”

3Mungu wetu yuko mbinguni;

yeye anafanya yote anayotaka.

4Miungu yao ni ya feza na zahabu;

imetengenezwa kwa mikono ya wanadamu.

5Ina vinywa lakini haisemi.

Ina macho lakini haioni.

6Ina masikio lakini haisikii.

Ina pua lakini hainusi.

7Ina mikono lakini haipapasi.

Ina miguu lakini haitembei.

Haiwezi hata kidogo kutoa sauti.

8Wote wanaoitengeneza wanafanana nayo,

na hata vilevile wote wanaoitumainia.

9Enyi Waisraeli, mumutumainie Yawe;

yeye ndiye musaada wenu na ngao yenu.

10Enyi wazao wa Haruni, mumutumainie Yawe;

yeye ndiye musaada wenu na ngao yenu.

11Enyi munaomwabudu Yawe, mumutumainie,

yeye ndiye musaada wenu na ngao yenu.

12Yawe anatukumbuka na atatubariki.

Atawabariki watu wa Israeli,

atawabariki wazao wa Haruni,

13atawabariki wote wanaomwabudu,

atawabariki wakubwa kama vile wadogo.

14Yawe awajalie muongezeke;

awajalie muongezeke ninyi na wazao wenu!

15Mubarikiwe na Yawe,

aliyeumba mbingu na dunia.

16Mbingu ni mali ya Yawe,

lakini amewapa wanadamu dunia.

17Wafu hawamusifu Yawe,

wala yeyote aliyeshuka katika kuzimu.

18Lakini ni sisi tutakaomusifu Yawe,

tutamusifu sasa na hata milele.

Haleluia!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help