1Wandugu zangu, kitu ninachotamani kwa moyo wote nami ninachomwomba Mungu kwa ajili ya Waisraeli, ni kwamba waokolewe.
2Kwa maana ninashuhudia kwamba wanajitoa kwa bidii kutumikia Mungu, lakini bidii ile haitokani na ufahamu wa kweli.
3Hawakufahamu namna Mungu anavyowahesabia watu haki na wakatafuta kusimamisha haki yao wenyewe. Wakakataa kufuata njia ya kuhesabiwa haki mbele ya Mungu.
4Kwa maana kwa njia ya Kristo, Sheria imepata kufikia ukomo wake kusudi kila mutu anayeamini apate kuhesabiwa haki mbele ya Mungu.
Wokovu ni kwa watu wote5Haya ndiyo mambo Musa aliyoandika juu ya kuhesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya kushika Sheria: “Mutu anayetimiza maagizo ya Sheria, ataishi kwa njia yake.”
6Lakini hivi ndivyo inavyosemwa juu ya kuhesabiwa haki kwa njia ya imani: “Usijiulize: ‘Ni nani atakayepanda mbinguni?’ ” (maana yake ni kumushusha Kristo toka kule.)
7Wala usijiulize: “Ni nani atakayeshuka katika kuzimu?” (maana yake kumupandisha Kristo toka kule kwenye wafu).
8Lakini inasemwa namna gani? “Neno la Mungu liko karibu nawe, liko ndani ya kinywa chako na ndani ya moyo wako.” Neno hili ni ujumbe tunaouhubiri juu ya imani.
9Kama ukiitikia kwa kinywa chako mwenyewe kwamba Yesu ni Bwana na kuamini katika moyo wako kwamba Mungu alimufufua, utaokolewa.
10Kwa maana mutu akiamini kwa moyo wake, Mungu anamuhesabia haki mbele yake; naye anapoitikia kwa kinywa chake, anaokolewa.
11Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Kila mutu anayemwamini hatapata haya.”
12Basi hakuna tofauti kati ya Wayuda na watu wa mataifa mengine, kwa maana Bwana wa wote ni mumoja tu, na anawabariki sana wote wanaomusihi.
13Ni kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Kila mutu anayemusihi Bwana, ataokolewa.”
14Basi namna gani watamusihi yule wasiyemwamini? Na namna gani watamwamini yule wasiyesikia habari zake? Na namna gani watasikia habari zake ikiwa hakuna wanaohubiri?
15Na namna gani watahubiri ikiwa hawatumwi? Ni kama inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Angalia jinsi kunavyofurahisha kuja kwa wale wanaoleta habari njema.”
16Lakini wote hawakukubali ile Habari Njema. Kwa maana Isaya, alisema: “Ee Bwana, ni nani aliyeamini habari tulizotangaza?”
17Hivi basi imani inatokana na kusikia habari, na habari ile inatokana na neno la Kristo.
18Basi ninauliza: hawakusikia habari hii? Ndiyo, wameisikia! Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema:
“Sauti yao imesikilika katika dunia yote,
maneno yao yamefika pande zote za dunia.”
19Ninauliza tena: Waisraeli hawakufahamu kitu? Kwanza Musa alikuwa amekwisha kujibu:
“Nitawafanya kuwa na wivu juu ya watu wasiokuwa taifa.
Nitawakasirikisha ninyi kwa njia ya taifa pumbafu.”
20Isaya kwa uhodari anaongeza kusema maneno haya:
“Nimepatikana kwa watu wasionitafuta,
nimejifunua kwa watu wasioniuliza.”
21Lakini juu ya Waisraeli anasema hivi: “Muchana kutwa ninanyoosha mikono yangu kwa kuita taifa lenye uasi na ubishi.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.