2 Mambo ya Siku 30 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Matayarisho ya Pasaka

1Mufalme Hezekia akawatumia ujumbe watu wote wa Israeli na Yuda, na vilevile akawaandikia barua watu wa kabila la Efuraimu na Manase, akiwaalika wote wakuje katika nyumba ya Yawe kule Yerusalema, kusudi wafanye sikukuu ya Pasaka kwa heshima ya Yawe, Mungu wa Israeli.

2Mufalme, viongozi na watu wote wa muji wa Yerusalema walifanya shauri kwa kufanya sikukuu hiyo ya Pasaka katika mwezi wa pili Ang. Hes 9.9-11

3pahali pa mwezi wa kwanza kama vile ilivyokuwa kawaida, kwa sababu hesabu ya makuhani waliokuwa wamekwisha kujitakasa ilikuwa ndogo, nao watu walikuwa bado hawajakusanyika Yerusalema.

4Mupango huu ukamupendeza mufalme pamoja na watu wote waliokuwa wamekusanyika.

5Kwa hiyo wakaamua kutoa tangazo katika inchi yote ya Israeli, kutoka Beri-Seba mpaka Dani, kwamba watu wakuje Yerusalema kwa kufanya sikukuu ya Pasaka ya Yawe, Mungu wa Israeli. Ilikuwa imepita muda murefu mbele ya watu kufanya Pasaka kulingana na sheria zake.

6Kwa hiyo wajumbe wakapita katika inchi yote ya Israeli na ya Yuda kwa kupeleka barua zile kufuatana na amri ya mufalme na wakubwa wake. Barua hizo zilikuwa na ujumbe huu:

“Enyi watu wa Israeli muliobaki nyuma ya mashambulizi ya wafalme wa Asuria. Mumurudilie Yawe, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Israeli, kusudi naye apate kuwarudilia.

7Musikuwe kama babu zenu na wandugu zenu ambao hawakukuwa waaminifu kwa Yawe Mungu wa babu zao, ambaye kama vile munavyoona aliwaazibu vikali.

8Sasa musikuwe wenye mioyo migumu kama babu zenu lakini mumutii Yawe. Mukuje katika Pahali Patakatifu pake Yerusalema, ambako ametakasa milele, mumwabudu Yawe, Mungu wenu, kusudi asiwakasirikie.

9Mukimurudilia Yawe, wale ambao walipeleka wandugu zenu na watoto wenu kuwa wafungwa, watawahurumia na kuwaacha warudi katika inchi hii. Kwa maana Yawe, Mungu wenu, ni mwenye huruma na rehema, naye hatawageuzia mugongo ikiwa mutamurudilia.”

10Basi wajumbe wale wakaenda toka muji mumoja mpaka mwingine katika inchi yote ya Efuraimu na Manase, wakafika hata katika inchi ya Zebuluni. Lakini watu waliwacheka na kuwazarau.

11Hata hivyo, watu wachache kati ya makabila ya Aseri, Manase na Zebuluni, walijinyenyekeza wakakuja Yerusalema.

12Nguvu za Mungu zilikuwa zikifanya kazi katika Yuda, zikitia moyo wa kutii amri za mufalme na wakubwa wake kadiri ya maagizo ya Yawe.

Pasaka inafanyika

13Watu wengi sana wakakusanyika Yerusalema katika mwezi wa pili, kwa kufanya sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu.

14Wakaanza kazi, wakaondoa mazabahu zote zilizokuwa Yerusalema, na zingine zote zilizotumiwa kwa kufukizia ubani, wakazibeba na kuzitupa katika Bonde la Kidroni.

15Siku ya kumi na ine ya mwezi ule wakachinja mwana-kondoo wa Pasaka. Makuhani na Walawi wakapata haya, wakajitakasa na kuleta sadaka za kuteketezwa katika nyumba ya Yawe.

16Wakatwaa nafasi zao katika hekalu kulingana na maagizo yaliyokuwa katika Sheria ya Musa, mutu wa Mungu. Walawi wakawapa makuhani damu ya sadaka, nao wakainyunyiza juu ya mazabahu.

17Kwa vile ambavyo wengi wa wale waliokusanyika pale hawakukuwa wamejitakasa. Walawi walipaswa kuwachinjia wana-kondoo wa Pasaka na kuwatakasa kwa ajili ya Yawe.

18Watu wengi kati ya wale waliotoka katika kabila la Efuraimu, Manase, Isakari na Zebuluni, walikuwa wakifanya Pasaka kinyume cha maagizo. Hii ni kwa kuwa mufalme Hezekia aliwaombea akisema: “Yawe, wewe ni mwema. Umusamehe mutu yeyote

19atakayekuomba kwa moyo wake wote wewe Yawe, Mungu wa babu zake, hata ingawa yule mutu si musafi kulingana na sheria za utakaso.”

20Yawe akakubali ombi la Hezekia, akawasamehe watu wale.

21Waisraeli wote waliokuwa wamekusanyika Yerusalema wakafanya sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu kwa muda wa siku saba, wakiwa na furaha kubwa. Walawi na makuhani wakamusifu Yawe kila siku, walimwimbia kwa nguvu zao zote.

22Mufalme Hezekia aliwasifu na kuwatia moyo makuhani kwa sababu waliendesha ibada kwa ujuzi mwingi.

Pasaka kwa mara ya pili

Nyuma ya kumaliza siku saba ambamo watu walikula, wakatoa sadaka za amani na kumutukuza Yawe, Mungu wa babu zao,

23watu waliamua kwa shauri moja kuendelesha sherehe kwa muda wa siku saba zaidi. Basi wakaendelea kusherehekea kwa furaha kubwa kwa muda wa siku saba zaidi.

24Mufalme Hezekia wa Yuda akawapa watu waliokusanyika jumla ya ngombe dume elfu moja na kondoo elfu saba. Vilevile, wakubwa wakawapa ngombe dume elfu moja na kondoo elfu kumi. Hesabu kubwa ya makuhani wakajitakasa.

25Kila mutu aliyehuzuria alifurahi sana. Watu wote wa Yuda, makuhani na Walawi, wakaaji wa Yerusalema waliohuzuria, wageni waliotoka inje ya Yerusalema na wale walioishi katika inchi ya Yuda, wote walifurahi sana.

26Kukakuwa furaha kubwa sana Yerusalema, maana tangu wakati wa mufalme Solomono mwana wa Daudi, mufalme wa Israeli jambo kama hilo lilikuwa halijatokea Yerusalema.

27Kisha, makuhani na Walawi wakawaombea watu baraka za Yawe, naye katika makao yake matakatifu kule mbinguni akasikia maombi yao na kuyakubali.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help