Ezra 5 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Wakati ule, manabii wawili, Hagai na Zakaria mwana wa Ido, wakawatolea unabii Wayuda waliokuwa wanakaa Yuda na Yerusalema, katika jina la Mungu wa Israeli.

2Nao Zerubabeli mwana wa Saltieli, na Yesua mwana wa Yosadaki, walipousikia ujumbe huo wakaanza tena kuijenga nyumba ya Mungu katika Yerusalema, wakisaidiwa na manabii wa Mungu.

3Kisha Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi na wenzao, wakakwenda Yerusalema na kuuliza: “Nani aliyewaamuru kuijenga nyumba hii mpaka kuimaliza?”

4Tena wakauliza: “Ni nani wanaojenga nyumba hii? Tunataka majina yao.”

5Lakini Mungu alikuwa anawalinda viongozi wa Wayuda, kwa hiyo wakubwa hao hawakuwakataza mpaka pale walipomwandikia mufalme Dario na kupata maoni yake.

6Basi, Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi na wenzao, wakamwandikia mufalme Dario.

7Walimutumia mufalme barua iliyoandikwa hivi:

Kwa mufalme Dario, tunakutakia amani.

8Tungetaka kukufahamisha, ee mufalme, kwamba tulikwenda katika jimbo la Yuda kunapokuwa nyumba ya Mungu Mukubwa. Nyumba hii inajengwa upya kwa mawe makubwamakubwa na kuta zake zinawekwa nguzo za miti. Kazi hiyo inafanywa kwa uangalifu mukubwa na inaendelea vizuri sana.

9Tuliwauliza viongozi hao watuambie ni nani aliyewapa amri ya kuijenga upya nyumba hii mpaka kuimaliza.

10Tukawauliza vilevile majina yao kusudi tuweze kukujulisha wale wanaoongoza kazi hiyo.

11Wao wakatujibu hivi: “Sisi ni watumishi wa Mungu wa mbingu na dunia, na tunaijenga upya nyumba ambayo ilikuwa imejengwa na kumalizika pale mbele na mufalme mumoja mukubwa wa Israeli.”

12Lakini kwa sababu babu zetu walimukasirikisha Mungu wa mbingu, yeye akawatia katika mikono ya mufalme Nebukadneza wa Babeli, Mukaldea, aliyeharibu nyumba hii na kuwapeleka watu katika uhamisho kule Babeli. Ang. 2 Fal 25.8-12; 2 Sik 36.17-20; Yer 52.12-15

13Lakini katika mwaka wa kwanza wa utawala wa mufalme Kiro wa Babeli akatoa amri kwamba nyumba hii ya Mungu ijengwe upya. Ang. Ezra 1.2-11

14Vilevile akavirudisha vyombo vya zahabu na feza ambavyo mufalme Nebukadneza alikuwa amevipeleka kutoka katika hekalu kule Yerusalema na kuviweka katika hekalu la Babeli. Vyombo hivyo Kiro akaviondoa toka hekalu la Babeli na kuvipatia Sesebasari ambaye alikuwa amemuchagua akuwe mutawala wa Yuda; akamwamuru akisema:

15“Utwae vyombo hivyo na kuvirudisha katika hekalu la Yerusalema, na kuijenga upya nyumba ya Mungu pahali pake.”

16Kisha Sesebasari akakuja na kuweka musingi wa nyumba ya Mungu katika Yerusalema, na tangu wakati huo ujenzi umekuwa ukiendelea mpaka sasa, lakini bado haujamalizika.

17Basi, ikikupendeza, ewe mufalme, amuru uchunguzi ufanyike katika kitabu cha habari za kifalme katika muji wa Bebeli kama mufalme Kiro alitoa amri nyumba hii ya Mungu ijengwe upya katika Yerusalema. Kisha, tunakuomba utujulishe maoni yako juu ya jambo hili.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help