Yeremia 11 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Hasara ya kuvunja agano la Mungu

1Yawe akanitolea mimi Yeremia ujumbe, akisema:

2Sikiliza maneno ya agano hili, kisha uende kuyatangazia watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema.

3Utawaambia hivi:

Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Alaaniwe mutu yeyote asiyeshika masharti ya agano hili.

4Hili ni agano nililowaagiza babu zenu kutii nilipowaondoa katika inchi ya Misri, kutoka katika shimo la moto. Niliwaambia wanitii na kufanya yote niliyowaamuru, na kwamba wakifanya hivyo, watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.

5Na kwa njia hiyo mimi nitatimiza ahadi niliyowatolea babu zenu, kwamba nitawapa inchi inayojaa maziwa na asali, kama inavyokuwa hata leo. Nami nikajibu: Ikuwe hivyo, ee Yawe.

6Yawe akaniambia: Tangaza maneno hayo yote katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema. Uwaambie watu wayasikilize masharti ya agano hili na kuyashika.

7Maana niliwaonya vikali babu zao nilipowaondoa katika inchi ya Misri, nami nimeendelea kuwaonya wanitii mpaka siku hii ya leo.

8Lakini wao hawakunitii, wala hawakunisikiliza. Kila mumoja wao alizidi kuwa mugumu na mwovu. Basi, niliwaazibu kulingana na masharti ya agano hili nililowaamuru kushika, lakini hao wakakataa kulishika.

9Tena Yawe akaniambia: Watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema wanafanya shauri baya la kuniasi.

10Wameurudilia uovu wa babu zao ambao walikataa kusikiliza maneno yangu; wanaiabudu miungu mingine na kuitumikia. Watu wa Israeli na watu wa Yuda wamevunja agano nililofanya na babu zao.

11Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Nitaleta hasara juu yao ambayo hawataweza kuiepuka. Hata kama wakinililia namna gani, sitawasikiliza.

12Kwa hiyo wakaaji wa Yuda na wa Yerusalema watakapoiendea miungu yao ambayo wanaifukizia ubani, lakini miungu hiyo haitaweza kuwaokoa wakati huo wa hasara itakayowapata.

13Enyi watu wa Yuda, hesabu ya miji yenu ni sawasawa na hesabu ya miungu yenu. Na kama vile barabara zenu za Yerusalema zinavyokuwa nyingi, ndivyo mulivyojenga mazabahu ya haya, ni kusema ya kufukizia ubani kwa mungu Bali.

14Basi, wewe Yeremia, usiwaombee watu hawa, usinililie kwa ajili yao, wala kunisihi. Maana, hata wakiniomba watakapokuwa katika hasara, sitawasikiliza.

15Yawe anasema: Watu wangu wapendwa wana haki gani ya kuingia ndani ya hekalu langu ikiwa wametenda maovu? Wanazani kwamba viapo vyao na sadaka zao wanazonitolea zitawakingia hasara ile.

16Wakati fulani, mimi nilisema kwamba wao ni muzeituni wenye majani mabichi, muzeituni muzuri na wenye matunda mema; lakini sasa, kwa ngurumo ya zoruba kubwa, nitauchoma kwa moto na kuyateketeza matawi yake.

17Mimi Yawe wa majeshi niliuotesha huu muzeituni; lakini sasa ninatangaza hasara juu yake, kwa sababu ya maovu ambayo watu wa Israeli na Yuda wameyafanya. Wamenikasirikisha kwa kumufukizia mungu Bali ubani.

Shauri baya la kumwua Yeremia

18Yawe alinijulisha, nami nikaelewa;

Yawe alinijulisha shauri lao baya.

19Nami nilikuwa kama kondoo mupole anayepelekwa kuchinjwa;

sikujua kwamba shauri walilofanya lilikuwa juu yangu.

Wao walisema: Tuuharibu muti pamoja na matunda yake,

tumwue apate kusahaulika katika dunia,

jina lake lisikumbukwe tena.

20Lakini, ee Yawe wa majeshi,

wewe unayehukumu kwa haki,

unayechunguza mioyo na akili za watu,

unijalie nione jinsi utakavyowalipiza kisasi,

maana ninayaweka maneno yangu kwako.

21Kwa hiyo Yawe wa majeshi anasema hivi juu ya watu wa Anatoti ambao wanataka kuniua na kuniambia: Usitutabirie kwa jina la Yawe, kama si vile tutakuua.

22Ndiyo, Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitawaazibu watu hao. Vijana wao watauawa kwa upanga; watoto wao wanaume na wanawake watakufa kwa njaa.

23Nimepanga muda wa kuleta maangamizi juu ya watu wa Anatoti. Wakati huo utakapofika, hakuna hata mumoja wao atakayebaki muzima.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help