Waamuzi 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yawe anawagombeza watu wake

1Malaika wa Yawe aliondoka Gilgali, akaenda Bokimu, akawaambia Waisraeli: “Niliwaondoa katika inchi ya Misri na kuwaleta katika inchi ambayo niliahidi kwa kiapo kwa babu zenu. Nilisema kwamba sitalivunja agano langu nanyi hata kidogo.

2Na kwa upande wenu niliwaamuru musifanye agano na wenyeji wa inchi hii na kwamba mazabahu zao mutazibomoa. Lakini ninyi hamukuitii amri yangu. Kwa nini mambo haya?

3Kwa hiyo sasa ninasema: Sitawafukuza tena wakaaji wa inchi hii lakini watawataabisha ninyi, na miungu yao itakuwa mutego kwenu.”

4Malaika wa Yawe alipowaambia watu wote wa Israeli maneno haya, wakalalamika na kulia.

5Wakapaita pahali pale Bokimu, ni kusema “Wanaolia”. Pale wakamutolea Yawe sadaka.

Kifo cha Yoshua

6Yoshua aliwatuma Waisraeli wote waende kwenye maeneo yao waliyogawanyiwa kwa kurizi inchi.

7Waisraeli walimutumikia Yawe siku zote za maisha ya Yoshua na nyuma ya kifo chake kwa muda wote wale wazee waliobaki waliishi ambao waliyaona matendo makubwa ambayo Yawe aliwatendea Waisraeli.

8Yoshua mwana wa Nuni, na mutumishi wa Yawe, akakufa akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi.

9Wakamuzika katika sehemu aliyogawanyiwa ikuwe yake kule Timunati-Heresi, katika inchi ya milima ya Efuraimu upande wa kaskazini wa mulima Gasi.

10Kisha watu wote wa kizazi chake wakakufa, kizazi kingine kikafuata ambacho hakikumujua Yawe wala matendo aliyowatendea watu wa Israeli.

Waisraeli wanamwasi Yawe

11Basi, Waisraeli walitenda uovu mbele ya Yawe na kuabudu Mabali.

12Walimwacha Yawe, Mungu wa wazee wao, ambaye aliwaondoa katika inchi ya Misri, wakaifuata miungu mingine, miungu iliyoabudiwa na watu walioishi kandokando yao. Waliinama mbele ya miungu hiyo, wakamukasirikisha sana Yawe.

13Walimwacha Yawe, wakatumikia Mabali na Mastaroti.

14Basi, hasira ya Yawe ikawaka juu ya Israeli, naye akawaacha wanyanganyi wanyanganye mali zao. Akawatoa kwa waadui zao waliowazunguka hata wasiweze tena kuwashinda.

15Kila mara walipokwenda kupigana, mukono wa Yawe ulipambana nao kwa kuwaletea hasara, kama alivyokuwa amewaonya na kuapa. Nao wakakuwa katika huzuni kubwa.

16Halafu Yawe akawapa waamuzi ambao waliwaokoa toka katika mikono ya watu walionyanganya mali zao.

17Hata hivyo, Waisraeli hawakuwasikiliza waamuzi wao, maana walifanya kama wazinzi kwa kufuata miungu mingine na kuinama mbele yao. Wakaacha upesi njia ya babu zao. Babu zao walitii amri za Yawe lakini wao hawakuzitii.

18Kila mara Yawe alipowapelekea mwamuzi, yeye mwenyewe alikuwa pamoja na mwamuzi yule, akawaokoa toka katika mikono ya waadui zao muda wote wa maisha ya mwamuzi yule. Ingawa hivyo, Yawe aliwaonea huruma aliposikia kilio chao kutokana na mateso na masumbuko yao.

19Lakini kila mara mwamuzi alipokufa walirudilia mienendo yao ya zamani, wakaishi vibaya kuliko babu zao. Waliifuata miungu mingine, wakaitumikia na kuinama mbele yao, wala hawakuyaacha matendo yao wala uasi wao.

20Kwa hiyo Yawe akawaka hasira juu ya Waisraeli, akasema: “Kwa sababu watu hawa wamevunja agano nililofanya na babu zao, wakakataa kutii sauti yangu,

21sitayafukuza tena mataifa ambayo Yoshua aliyaacha, wakati alipokufa.

22Nitayatumia mataifa hayo kuwajaribu Waisraeli nione kama watairudilia njia yangu kama babu zao au sivyo.”

23Basi, Yawe akayaacha mataifa hayo ambayo hakumupa Yoshua ushindi juu yao, wala hakuyafukuza mara moja.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help