1Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Kiro mufalme wa Persia, Yawe akatimiza neno alilosema kwa njia ya nabii Yeremia. Yawe akaamusha nia ya Kiro mufalme wa Persia, naye akatoa amri hii katika ufalme wake, vilevile amri hiyo ikatolewa kwa maandiko:
2Hivi ndivyo Kiro mufalme wa Persia anavyosema: Yawe, Mungu wa mbingu, amenipatia falme zote katika ulimwengu na ameniagiza nimujengee nyumba katika Yerusalema, huko Yuda.
3Basi sasa, kila mutu kati yenu ninyi wote munaokuwa watu wake, Mungu wake akuwe naye na aende katika Yerusalema huko Yuda, na kuijenga upya nyumba ya Yawe, Mungu wa Israeli, Mungu anayeabudiwa kule Yerusalema.
4Kila mumoja aliyebaki muzima katika uhamisho akitaka kurudi, wajirani zake wamusaidie kwa kumupa feza, zahabu, mali na nyama, pamoja na matoleo ya mapenzi yake kwa ajili ya nyumba ya Mungu kule Yerusalema.
5Basi, viongozi wa ukoo za makabila ya Yuda na Benjamina wakaondoka, makuhani na Walawi, na kila mutu ambaye Mungu alimupa moyo wa kwenda kujenga upya nyumba ya Yawe, inayokuwa Yerusalema.
6Wajirani waliwasaidia watu hao kwa kuwapa vyombo vya feza, zahabu, mali, nyama na vitu vingine vya bei kali, mbali na vile vilivyotolewa kwa mapenzi.
7Mufalme Kiro akawarudishia vyombo ambavyo mufalme Nebukadneza alikuwa amevitwaa kutoka katika nyumba ya Yawe na kuviweka katika nyumba ya miungu yake.
8Akamupatia Mitiredati, mulinzi wa hazina, vyombo hivyo, naye akavihesabu mbele ya Sesebasari, mutawala wa Yuda.
9Hii ndiyo hesabu yake:
bakuli makumi tatu za zahabu,
bakuli elfu moja za feza,
vyetezo makumi mbili na tisa,
10bakuli ndogo za zahabu makumi tatu,
bakuli ndogo za feza mia ine na kumi,
vyombo vingine elfu moja.
11Vyombo vyote vya zahabu na feza, pamoja na vitu vingine vilikuwa jumla yake elfu tano mia ine. Vyote hivi, Sesebasari alivibeba mpaka Yerusalema wakati yeye pamoja na watu wengine walipotolewa toka katika uhamisho kule Babeli kwenda Yerusalema.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.