Ruta 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Ruta anafanya kazi katika shamba la Boazi

1Naomi alikuwa na ndugu aliyeitwa Boazi, wa ukoo wa Elimeleki mume wake. Huyo alikuwa mutu mwenye heshima na tajiri.

2Siku moja, Ruta wa Moabu akamwambia Naomi: “Muniruhusu niende kukusanya masalio ya mavuno pahali nitakapopata kukubaliwa na mwenye shamba.” Naomi akamwambia: “Basi, uende binti yangu.”

3Basi Ruta akaenda katika shamba, akawafuata wavunaji naye akiyaokota masuke waliyoyaacha. Na kumbe akajikuta katika shamba la Boazi, yule wa ukoo wa Elimeleki.

4Nyuma ya muda, Boazi akafika kutoka Betelehemu, akawasalimia wavunaji, akasema: “Yawe akuwe nanyi.” Nao wakamujibu: “Yawe akubariki.”

5Kisha Boazi akamwuliza musimamizi wa wavunaji: “Yule binti ni nani?”

6Yule kiongozi wa wavunaji akajibu: “Ni binti Mumoabu aliyekuja pamoja na Naomi kutoka katika inchi ya Moabu.

7Aliniomba nimuruhusu awafuate nyuma wavunaji naye akiokota masalio kati ya miganda. Basi alikuja na amefanya kazi tangu asubui na ni sasa tu amekwenda kupumzika katika kibanda.”

8Halafu Boazi akamwambia Ruta: “Sasa sikiliza binti yangu. Usiende kuokota masuke pahali pengine, lakini katika shamba hili tu. Ushikamane na wanawake hawa.

9Angalia pahali wanapovuna ufuate nyuma yao. Nimewaonya vijana hawa wasikusumbue. Na ukisikia kiu, kwenda kwenye mitungi na ukunywe maji vijana hao waliyoyateka.”

10Hapo Ruta akamwinamia Boazi uso mpaka chini kwa unyenyekevu, akamwambia: “Nimepata namna gani kukubaliwa mbele yako? Mbona unanishugulikia ijapokuwa mimi ni mugeni tu?”

11Lakini Boazi akamujibu: “Nimeyasikia yote uliyomufanyia mama mukwe wako tangu mume wako alipokufa. Ninajua jinsi ulivyowaacha wazazi wako, ukaiacha inchi yako, na jinsi ulivyokuja kuishi kati ya watu ambao haukuwajua tangu zamani.

12Yawe akubariki kwa yote uliyoyafanya. Yawe wa Israeli uliyemukimbilia akulinde chini ya mabawa yake, akupe zawadi kamilifu.”

13Ruta akamujibu: “Bwana, wewe umenifanyia wema mukubwa sana. Ingawa mimi si kama mumoja wa watumishi wako, nimetosheka kwa sababu umenifariji sana na kuongea nami kwa upendo.”

14Wakati wa chakula, Boazi akamukaribisha Ruta akamwambia: “Karibu hapa, kuja ukule mukate vilevile na uuchovye ndani ya divai.” Kwa hiyo Ruta akaikaa pamoja na wavunaji, na Boazi akamupa ngano iliyokaangwa, akakula akashiba hata akaacha sehemu.

15Naye Ruta alipoendelea kuokota mavuno, Boazi akawaambia watumishi wake: “Muache akusanye hata pahali miganda inapokuwa wala musimukaripie.

16Zaidi ya pale, muchomoe masuke kutoka katika miganda na mumwachie aokote bila kumukaripia.”

17Basi Ruta akaendelea kuokota masuke mpaka magaribi; na kisha kupepeta hiyo shayiri alipata kilo makumi tatu na zaidi.

18Kisha akatwaa mavuno hayo mpaka katika muji na kumwonyesha mama mukwe wake kiasi alichookota. Vilevile alikitoa kile chakula alichokiacha kisha kushiba, akamupa.

19Basi mama mukwe wake akamwuliza: “Uliokota wapi haya yote? Ulikuwa katika shamba la nani? Abarikiwe yule aliyekutendea wema.” Hapo Ruta akamwambia Naomi kwamba alikuwa akifanya kazi katika shamba la mutu aliyeitwa Boazi.

20Basi, Naomi akamwambia mukwe wake: “Yawe amubariki Boazi! Mungu anatimiza siku zote ahadi zake kwa wanaokuwa wazima na waliokufa.” Kisha akaendelea kusema: “Huyo mutu ni ndugu yetu wa karibu na ni mumoja wa wale wenye mapaswa ya kututunza.”

21Kisha Ruta wa Moabu akasema: “Aliniambia vilevile nishikamane pamoja na watumishi wake mpaka wamalize mavuno yote.”

22Basi, Naomi akamwambia Ruta: “Hakika binti yangu, ni vizuri kufanya kazi pamoja na wanawake wengine katika shamba la Boazi, kwa maana labda ungesumbuliwa kama ungekwenda katika shamba la mutu mwingine.”

23Kwa hiyo, Ruta akashikamana nao, akaokota masuke mpaka mavuno ya ngano na shayiri yalipomalizika. Wakati ule wote, alikuwa anakaa na mama mukwe wake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help