Kumbukumbu la Sheria 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Waisraeli katika jangwa

1“Kisha, tukageuka, tukasafiri katika jangwa kwa kupitia njia ya bahari Nyekundu, kama vile Yawe alivyoniambia. Tukatangatanga karibu na mulima Seiri kwa muda murefu.

2Kisha Yawe akaniambia:

3‘Mumetangatanga ya kutosha katika inchi hii ya milima. Sasa mugeuke muelekee upande wa kaskazini.

4Muko karibu kupita katika inchi ya milima ya Seiri, inchi ya wandugu zenu wazao wa Esau. Hao watawaogopa, lakini mufanye angalisho,

5musipigane nao kwa sababu sitawapa sehemu yoyote ya inchi yao. Sitawapa hata pahali padogo pa kukanyaga. Inchi hiyo ya milima ya Seiri nimewapa wazao wa Esau ikuwe mali yao.

6Mukitaka chakula au maji kutoka kwao, munapaswa kununua.’

7“Basi, mukumbuke jinsi Yawe Mungu wenu alivyowabariki ninyi katika kila jambo mulilofanya. Aliwatunza mulipokuwa munatangatanga katika jangwa hili kubwa. Amekuwa pamoja nanyi miaka hii yote makumi ine na hamukupungukiwa na kitu chochote.

8“Hivyo tukaendelea na safari yetu, tukawapita wandugu zetu, wazao wa Esau ambao waliishi Seiri, tukaepuka vilevile ile njia ya bonde na sehemu za miji ya Elati na Esioni-Geberi. Kisha tukageuka tukafuata njia ya kupitia jangwa la Moabu.

9Yawe akaniambia: ‘Usiwasumbue watu wa Moabu, wala usipigane nao maana sitawapa sehemu yoyote ya inchi yao. Lakini eneo hilo la Ari nimewapa hao wazao wa Loti likuwe mali yao.’

10(Hapo zamani hiyo inchi ya Ari ilikuwa imekaliwa na watu wengi, wenye nguvu na ambao walikuwa warefu kama vile Waanaki.

11Kama vile Waanaki, watu hawa walijulikana vilevile kama Warefai, lakini Wamoabu waliwaita Waemi.

12Wahori vilevile waliishi huko Seiri zamani, lakini wazao wa Esau wakawafukuza na kuwaangamiza, kisha wao wenyewe wakakaa katika eneo hilo pahali pao. Waisraeli wakafanya vile vile katika inchi ile ambayo Yawe aliwapa ikuwe mali yao.)

13“Yawe akatuambia: ‘Muondoke sasa, muvuke kijito Zeredi’. Basi, tukavuka kijito Zeredi.

14Miaka makumi tatu na nane ilikuwa imepita tangu kuondoka Kadesi-Barnea mpaka kuvuka kijito Zeredi. Wakati huo, wote wenye umri wa kwenda kwa vita waliotoka Misri walikuwa wamekwisha kufa, kulingana na jinsi Yawe alivyowaapia.

15Yawe mwenyewe akawashambulia watu hao kwa kuwaangamiza huko katika kambi, hata wote wakaisha.

16“Basi, watu hao wote walipokwisha kufa,

17Yawe akaniambia:

18‘Leo hii mutauvuka mupaka wa Moabu kwa kupitia inchi ya Ari.

19Mutaifikia inchi ya Waamoni. Musiwasumbue wala musipigane nao kwa sababu sitawapa sehemu yoyote ya hao wazao wa Amoni ikuwe mali yenu. Hao ni wazao wa Loti, na nimewapa hiyo inchi ikuwe mali yao.’ ”

20(Inchi hiyo inajulikana vilevile kama inchi ya Warefai. Warefai walikuwa wanaishi huko hapo zamani; Waamoni waliwaita hao Wazamuzumi.

21Walikuwa watu wengi, wenye nguvu na warefu kama vile Waanaki. Lakini Yawe akawaangamiza mbele ya Waamori ambao walitwaa inchi yao wakaishi humo pahali pao.

22Yawe akafanya kama vile alivyowafanyia wazao wa Esau ndio Waedomu, ambao wanaishi katika inchi ya Seiri. Aliwaangamiza Wahori wakati Waedomu walipofika huko, wakanyanganya inchi yao na kuishi humo mpaka leo.

23Waavi walikuwa zamani wakiishi katika vijiji vya kando ya Mediteranea mpaka Gaza. Wakafutori kutoka kisiwa cha Kafutori wakawaangamiza, wakaishi humo pahali pao.)

24“Kisha Yawe akatuamuru: ‘Basi! Muanze safari. Muvuke bonde la Arnoni. Mimi nimetia katika mikono yenu Sihoni, mufalme wa Waamori wa Hesiboni na inchi yake. Mushambulie na kuanza kurizi inchi yake.

25Leo nitaanza kuwafanya watu wote katika dunia wakuwe na woga na hofu juu yenu. Watasikia habari zenu nao watatetemeka na kufazaika.’

Waisrael wana mushinda mufalme Sihoni(Hes 21.21-30)

26“Basi, nikatuma watu kutoka jangwa la Kedemoti waende kwa mufalme Sihoni wa Hesiboni na ujumbe huu wa amani:

27‘Uturuhusu tupite katika inchi yako. Tutapitia katika barabara na kwenda moja kwa moja bila kugeuka kuume wala kushoto.

28Chakula chetu tutakinunua kwako na maji ya kunywa vilevile. Tunachoomba tu ni ruhusa ya kupita kwa miguu katika inchi yako,

29tuvuke muto Yordani na kuingia katika inchi ambayo Yawe, Mungu wetu anatupatia. Wazao wa Esau wanaoishi Seiri na Wamoabu wanaoishi Ari walituruhusu vilevile kupita katika inchi yao’.

30“Lakini Sihoni, mufalme wa Hesiboni, hakuturuhusu tupite katika inchi yake. Yawe, Mungu wenu, akamufanya akuwe na kichwa kigumu na mugumu wa moyo, kusudi tumushinde na kutwaa inchi yake ambayo tunairizi mpaka leo.

31“Halafu Yawe akaniambia: ‘Nimeanza kumutia mufalme Sihoni na inchi yake katika mikono yenu. Muanze kutwaa inchi yake na kuirizi’.

32Kisha Sihoni akatoka na watu wake wote kupigana nasi karibu na muji wa Yahasa.

33Naye Yawe, Mungu wetu, akamutoa, tukamushinda yeye, watoto wake na watu wake wote.

34Tukaiteka na kuiharibu miji yake yote, tukaua wanaume na wanawake na watoto. Hatukumwacha mutu yeyote muzima.

35Tulibeba tu mifugo na mali tuliyokuta katika miji tuli Yosinda.

36Kuanzia Aroeri, muji unaokuwa kwenye ukingo wa bonde la Arnoni, na ule muji mwingine unaokuwa ndani ya bonde hili mpaka inchi ya Gileadi, hakuna muji wowote ambao hatukuweza kuushinda. Yawe aliitia miji yote katika mikono yetu.

37Lakini hatukukaribia inchi ya Waamoni au ukingo wa muto Yaboki wala katika miji ya inchi ya milima wala sehemu yoyote ambayo Yawe, Mungu wetu, alitukataza.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help