2 Petro 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Walimu wa uongo

1Zamani manabii wa uongo walitokea kati ya watu, na ndivyo hivyo walimu wa uongo watakavyotokea kati yenu. Watu hawa wataingiza mafundisho mabaya sana ya uongo kwa siri, wakimukataa hata Bwana aliyewakomboa na kujiletea maangamizi upesi.

2Watu wengi watafuata matendo yao maovu na kwa ajili yao, mafundisho ya Bwana yatazarauliwa.

3Na kwa sababu ya tamaa yao mbaya ya mali, walimu hawa wa uongo watajipatia faida juu yenu kwa njia ya maneno ya uongo. Lakini tangia zamani hukumu yao imekwisha kutangazwa, nao hawatakawia kuangamizwa.

4Kwa maana Mungu hakuwahurumia wale wamalaika waliofanya zambi, lakini aliwatupa katika jehenamu. Wao wanalindwa mule wakifungwa minyororo katika giza nzito wakingojea Siku ile ya hukumu.

5Mungu hakuhurumia dunia ya zamani, lakini alimulinda Noa, muhubiri wa haki, pamoja na watu wengine saba alipoleta mafuriko ya maji juu ya dunia ile ya waovu.

6Vilevile Mungu alihukumu muji wa Sodoma na Gomora na kuiteketeza kwa moto. Kwa njia hiyo, alionyesha mufano wa mambo yatakayotokea kwa watu waovu.

7Mungu alimwokoa Loti, mutu wa haki, aliyehuzunishwa sana na mwenendo mubaya wa wale watu waovu.

8Kwa maana mutu yule mwenye haki aliishi kati ya watu wabaya, akiona na kusikia kila siku mambo yaliyochukiza roho yake ya haki.

9Basi, ni kusema kwamba Bwana anajua namna ya kuwaokoa wenye kumwogopa katika majaribu. Lakini anangojea kuwaazibu watu wabaya kwa Siku ile ya hukumu.

10Na zaidi atawaazibu wale wanaoishi kufuatana na tamaa mbaya za kimwili na kuzarau mamlaka ya Mungu.

Walimu wale wa uongo ni wenye kiburi, wenye kujivuna, nao hawaogopi kutukana viumbe vitukufu vya mbinguni.

11Ingawa vile, wamalaika wenye kuwapita nguvu na uwezo hawawashitaki vibaya kwa kuwatukana mbele ya Bwana.

12Walimu hawa wa uongo ni kama nyama wasiokuwa na akili ambao wanazaliwa tu kwa kunaswa na kuchinjwa. Wao wanasema vibaya juu ya mambo yote wasiyojua. Wataangamizwa kufuatana na ubaya wao wenyewe.

13Watalipwa mateso kwa sababu ya mateso waliyoleta. Wanafurahia kutimiza waziwazi tamaa zao mbaya za kimwili muchana kati. Kufika kwao katika karamu zenu kunaleta haya na chukizo kubwa wanapofurahia mambo yao ya udanganyifu.

14Macho yao yanajaa uzinzi. Wao hawachoki kufanya zambi. Wanavuta watu wasiokamilika. Wanatawaliwa na tamaa za kupata mali. Watu hao wamelaaniwa!

15Wameacha njia ya kweli na kupotoka wakifuata njia ile Balama, mwana wa Beori, aliyofuata. Huyu alipenda kupata mali kwa njia isiyokuwa ya haki,

16lakini alikaripiwa kwa ajili ya uovu wake. Basi punda, ambaye hasemi, alisema kama mutu na kuzuiza kitendo cha upumbafu wa yule nabii.

17Wale walimu wa uongo ni kama visima visivyokuwa na maji tena, wao ni kama mawingu yanayopeperushwa na upepo; makao yao yametayarishwa kwenye giza nzito.

18Kwa maana kwa masemi yao ya kujivuna na yasiyokuwa na maana, na kwa njia ya tamaa zao mbaya za kimwili, wanawavuta watu ambao wanaanza kuwaepuka, na wale wanaoishi katika udanganyifu.

19Wanawaahidi watu wengine kwamba watakuwa huru ijapokuwa wao wenyewe ni watumwa wa upotovu. Kwa maana kila mutu ni mutumwa wa jambo lolote linalomutawala.

20Kufuatana na hayo, ikiwa watu wamekwisha kuponyoka kuishi katika machafuko ya dunia kwa njia ya kumujua Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo, nao wakiyarudilia tena na kutawaliwa nayo, hali yao ya mwisho itakuwa mbaya zaidi kuliko ile ya kwanza!

21Maana ingekuwa heri kwao kama wasingejua njia ya haki, kuliko kuijua na kisha kuacha ile amri takatifu waliyopewa.

22Kile kitu walichofanya kinaonyesha wazi mufano unaosema: “Imbwa amerudilia kula matapiko yake,” na: “Nguruwe aliyesafishwa amerudia tena kugaagaa katika matope!”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help