Waefeso 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kuokolewa kwa neema

1Zamani ninyi mulikuwa mumekufa kiroho kwa sababu ya makosa na zambi zenu.

2Mulikuwa mukiishi kufuatana na mwenendo mubaya wa dunia hii. Mulitii mutawala wa roho zenye uwezo wa anga anayetawala sasa watu wasiomutii Mungu.

3Zamani, sisi wote vilevile tulikuwa kama wao. Tuliishi kufuatana na tamaa zetu za kimwili na kutenda kufuatana na mapenzi ya mwili na roho zetu. Kwa sababu ya hali yetu ya kimwili, hatungeponyoka kasirani ya Mungu kama wengine.

4Lakini Mungu ni mwenye huruma nyingi. Alitupenda kwa upendo wake mukubwa;

5sisi tuliokuwa tumekufa kwa sababu ya makosa yetu, alitufufua pamoja na Kristo. Hivi mumeokolewa kwa neema ya Mungu.

6Katika kuungana kwetu na Yesu Kristo, Mungu ametufufua pamoja naye kusudi tutawale pamoja naye mbinguni.

7Alifanya vile kusudi aonyeshe kwa vizazi vyote vitakavyokuja neema yake kubwa ya ajabu kwa njia ya wema wake katika kuungana kwetu na Yesu Kristo.

8Kwa maana mumeokolewa kwa neema ya Mungu, kwa njia ya imani. Jambo hili halitokani na ninyi wenyewe, lakini ni zawadi ya Mungu.

9Si kwa matendo yenu, kusudi mutu asipate kujivuna.

10Kwa maana sisi ni viumbe vya Mungu, na kwa kuungana kwetu na Yesu Kristo, alituumba kusudi tuishi maisha ya matendo mema, ambayo Mungu alitutayarishia tangu mbele tupate kuyatenda.

Umoja katika Yesu Kristo

11Basi mukumbuke namna mulivyokuwa zamani ninyi munaokuwa kwa kizalikio watu wa mataifa mengine. Wayuda wanawaita ninyi watu wasiotahiriwa, lakini wao wanajiita wenye kutahiriwa kwa sababu ya kitambulisho cha kutahiriwa na watu katika miili yao.

12Kwa wakati ule mulikuwa mumetengwa mbali na Kristo. Hamukukuwa kati ya watu waliochaguliwa na Mungu, mulikuwa wageni kati yao. Ninyi hamukukuwa na pato lolote katika agano zile Mungu alizotoa katika ahadi yake kwa watu wake. Muliishi katika dunia pasipo tumaini wala kumujua Mungu.

13Lakini sasa, katika kuungana kwenu na Yesu Kristo, ninyi muliokuwa mbali, mumekuwa karibu kwa njia ya damu ya Kristo.

14Kwa maana Kristo mwenyewe ndiye aliyetuletea amani akifanya Wayuda na watu wa mataifa mengine kuwa jamii moja. Kwa njia ya kutoa mwili wake, amevunja uadui uliokuwa kama ukuta uliowatenganisha.

15Yeye aliondoa Sheria ya Kiyuda pamoja na amri zake na maagizo yake akifanya watu wa jamii hizi mbili kuwa watu wa taifa moja jipya katika kuungana naye na kuleta amani.

16Kristo alivunja uadui kwa njia ya kufa kwake juu ya musalaba, akaunganisha watu wa makabila haya mawili kuwa moja na kuwapatanisha na Mungu.

17Hivi, Kristo amekuja kutangaza Habari Njema ya amani kwa ninyi watu wa mataifa mengine, muliokuwa mbali na Mungu, na kwa Wayuda waliokuwa karibu naye.

18Kwa maana, kwa njia ya Kristo sisi wote, Wayuda na watu wa mataifa mengine, tumefunguliwa njia ya kufika mbele ya Baba katika Roho mumoja.

19Basi sasa, ninyi watu wa mataifa mengine si wageni tena wala wapangaji. Lakini sasa mumekuwa wanainchi pamoja na watu wa Mungu na tena mumekuwa watu wa jamaa la Mungu.

20Ninyi vilevile ni kama jengo linalosimama juu ya musingi uliowekwa na mitume na manabii; Yesu Kristo mwenyewe ndiye jiwe kubwa la pembe.

21Katika kuungana naye, jengo lote nzima linaunganishwa vizuri na kuongezeka hata lipate kuwa hekalu takatifu kwa ajili ya Bwana.

22Katika kuungana pamoja na Kristo, ninyi vilevile munaunganishwa pamoja na wengine wote kuwa makao ya Mungu kwa njia ya Roho wake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help