Ezekieli 18 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu anahukumu kila mutu kadiri ya matendo yake

1Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

2Kwa nini munarudiliarudilia mezali hii katika inchi ya Waisraeli:

Wababa wamekula matunda mabichi ya mizabibu,

lakini ni meno ya watoto wao ndiyo yanaumizwa!

3Kama vile ninavyoishi, mezali hii haitatumiwa tena katika Israeli.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

4Mujue kwamba uzima wa kila mutu ni katika mikono yangu, ikiwa uzima wa muzazi na uzima wa mutoto. Yeyote anayetenda zambi, ndiye atakayekufa.

5-9Kama mutu ni wa haki, ataishi. Mutu wa haki anatenda hivi:

anafuata sheria ya Mungu na kutenda kwa haki,

hakuli sadaka kwenye milima,

haziangalii sanamu za miungu ya Waisraeli,

hamuchafui muke wa jirani yake,

halali na mwanamuke wakati wake wa ugonjwa wa mwezi,

hamutendei mutu yeyote ubaya,

anarudisha rehani,

haibi,

anawapatia wenye njaa chakula

anawavalisha wale wanaokuwa uchi,

anakopesha bila kudai faida wala kujipatia mazidio,

anaepuka kutenda uovu,

anaamua kwa haki kati ya mwenye kudai na mwenye kudaiwa,

anafuata masharti yangu na kutii maagizo yangu kwa moyo.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

10-13Lakini ikiwa mutu huyo ana mutoto ambaye anafanya mabaya baba yake asiyofanya, yule mutoto atakufa kama anafanya machukizo haya:

ananyanganya,

anaua,

anakula sadaka kwenye milima,

anamuchafua muke wa jirani yake,

anawatendea wamasikini na wakosefu vibaya,

anaiba,

harudishi rehani,

anaangalia sanamu za miungu na kufanya machukizo,

anakopesha kwa kupata faida na kujitafutia mazidio.

Hakika atakufa, na yeye mwenyewe atabeba lazima ya kifo chake.

14-17Lakini kama mutu yule akiwa na mutoto ambaye ameona zambi ambazo baba yake alitenda, lakini yeye hatendi mabaya yale, hatakufa juu ya uovu wa baba yake. Ni mutoto anayetenda hivi:

hakuli sadaka kwenye milima,

haziangalii sanamu za miungu ya Waisraeli,

hamuchafui muke wa jirani yake,

hamutendei mutu yeyote ubaya,

hakamati rehani,

haibi,

anawapatia wenye njaa chakula na kuwavalisha wale wanaokuwa uchi,

anaepuka kutenda uovu,

anakopesha bila kudai faida wala kujipatia mazidio,

anatii maagizo yangu na kufuata masharti yangu.

18Lakini baba yake, kwa sababu alilipisha bei isiyokuwa ya haki na kumwibia ndugu yake, wala hakuwatendea wandugu zake vizuri, hakika atakufa kwa sababu ya uovu wake.

19Lakini munauliza: Kwa nini mutoto asiazibiwe kwa sababu ya zambi za baba yake? Mutoto akitenda mambo ya haki na ya ukweli, kama akiwa mwangalifu kushika masharti yangu yote, basi, huyo hakika ataishi.

20Atakayetenda zambi huyo ndiye atakayekufa. Mutoto hatabeba uovu wa baba yake, wala baba hatabeba uovu wa mutoto wake. Uhaki wa mutu wa haki itamufalia yeye mwenyewe: na uovu wa mwovu ataubeba yeye mwenyewe.

21Kama mutu mwovu akiachana na zambi zake zote alizotenda, kama akishika masharti yangu yote, na kutenda mambo ya haki na ya ukweli, huyo hakika ataishi, hatakufa.

22Makosa yake yote aliyofanya hayatakumbukwa; kwa sababu ya haki yake ataishi.

23Basi, ninafurahia kufa kwa mutu mwovu? Hapana! Mimi ninapendelea aachane na njia zake mbaya apate kuishi.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

24Lakini, mutu wa haki akiacha haki yake na kutenda uovu na kufanya machukizo yaleyale mutu mwovu anayofanya, basi, huyo ataishi? Hapana! Matendo yake yote mema aliyotenda hayatakumbukwa tena; atakufa kwa sababu ya uasi na zambi aliyotenda.

25Lakini ninyi munasema: Matendo ya Yawe si sawa! Musikilize sasa, enyi Waisraeli: Ninachofanya mimi si sawa? Munachofanya ninyi ndicho kisichokuwa sawa.

26Mutu wa haki akiacha haki yake na kutenda uovu atakufa kwa ajili hiyo; atakufa kwa sababu ya uovu aliotenda.

27Lakini mutu mwovu akiachana na uovu aliofanya, na kutenda mambo ya haki na ya ukweli, huyo atayaokoa maisha yake.

28Kwa sababu amefikiri, akaachana na makosa aliyoyafanya, hakika ataishi; hatakufa.

29Lakini ninyi Waisraeli munasema: Anachotenda Yawe si sawa! Enyi Waisraeli, basi, ninachofanya mimi si sawa? Munachofanya ninyi ndicho kisichokuwa sawa.

30Kwa hiyo, nitawahukumu ninyi Waisraeli, kila mumoja wenu, kulingana na mwenendo wake.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

Mugeuke na kuachana na makosa yenu yasipate kuwaangamiza.

31Mutupilie mbali zambi mulizonitendea; mujipatie moyo na roho mupya. Enyi Waisraeli, mutakufa kwa sababu gani?

32Sifurahii kifo cha mutu yeyote. Hivyo mugeuke kusudi mupate kuishi.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help