1Nyuma ya hayo, mufalme Nahasi wa Waamori akakufa, na mwana wake aliyeitwa Hanuni akakuwa mufalme pahali pa baba yake.
2Mufalme Daudi akasema: “Nitamutendea mema Hanuni mwana wa Nahasi kama vile baba yake alivyonitendea mimi.” Halafu, Daudi akatuma wajumbe kumupa pole kwa ajili ya kifo cha baba yake. Nao wajumbe wa Daudi walipofika katika inchi ya Waamori,
3wakubwa wa Waamori walimwambia bwana wao, Hanuni: “Unazani kwamba Daudi kwa kukutumia watu wa kukufariji anamuheshimu baba yako? Daudi hakuwatuma watu hawa kwako kwa kuuchunguza na kuupeleleza muji halafu wauteke?”
4Basi, Hanuni akawakamata wajumbe wale wa Daudi, akanyoa kila mumoja ngambo moja ya ndevu zake, akapasua nguo zao katikati mpaka kwenye matako, kisha akawaacha waende zao.
5Walipata haya sana kurudia kwao. Daudi alipopashwa habari, alituma watu kwa kuwapokea maana wale wajumbe walipata haya sana. Naye mufalme aliwaambia: “Mukae katika muji wa Yeriko, hata mutakapoota ndevu, kisha murudi kwa nyumba.”
6Waamoni walipoona kwamba wamemuchukiza Daudi, walijilipia waaskari wa miguu wa Waaramu elfu makumi mbili kutoka Beti-Rehobu na Zoba, waaskari elfu kumi na mbili kutoka Tobu, na mufalme Maka akiwa na waaskari elfu moja.
7Naye Daudi aliposikia habari zile, alimutuma Yoabu kwenda na kundi lote la waaskari mashujaa.
8Waamoni walitoka na kujipanga tayari kwa vita kwenye mulango wa muji wa Raba, muji wao mukubwa; nao Waaramu kutoka Zoba na Rehobu na watu kutoka Tobu na Maka walijipanga katika mbuga.
9Yoabu alipoona kwamba ilimupasa kupigana kwa upande wa mbele na nyuma, alichagua waaskari wamoja Waisraeli hodari zaidi, akawapanga mbele ya Waaramu.
10Wale waaskari wengine waliobaki aliwaweka chini ya uongozi wa ndugu yake Abisayi, naye akawapanga mbele ya Waamoni.
11Yoabu akamwambia Abisayi: “Ikiwa Waaramu wananishinda nguvu, utanisaidia lakini kama Waamoni wanakushinda nguvu, nitakuja kukusaidia.
12Lakini ujipe moyo! Tupigane kama wanaume kwa ajili ya watu wetu na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu. Naye Yawe atutendee lile analoona ni jema kwake.”
13Basi, Yoabu na watu wake walisonga mbele kwenda kupigana na Waaramu, nao Waaramu walikimbia.
14Waamoni walipoona kwamba Waaramu wamekimbia, nao vilevile walimukimbia Abisayi na kuingia katika muji. Yoabu akaacha kupigana na Waamoni, akarudi Yerusalema.
15Lakini Waaramu walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, walijikusanya pamoja.
16Hadadezeri aliagiza Waaramu waliokuwa ngambo ya muto Furati waletwe, wapelekwe kule Helamu wakiongozwa na Sobaki, jemadari wa waaskari wa Hadadezeri.
17Daudi alipopata habari, aliwakusanya pamoja waaskari wote wa Israeli, akavuka muto Yordani na kwenda mpaka Helamu. Nao Waaramu walijipanga tayari kwa vita na Daudi, wakaanza kupigana naye.
18Lakini Waaramu walikimbia mbele ya Waisraeli. Daudi aliwaua Waaramu mia saba waliokuwa waendeshaji wa magari ya vita, waaskari wapanda-farasi elfu makumi ine. Vilevile alimwumiza Sobaki, jemadari wa waaskari wao, naye akakufia palepale.
19Kisha wafalme wote waliokuwa watumishi wa Hadadezeri walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, walifanya mapatano ya amani na Israeli, nao wakakuwa watumishi wa Israeli. Hivyo Waaramu hawakusubutu kuwasaidia Waamoni tena.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.