1Kisha malaika wa tano akapiga baragumu. Halafu nikaona nyota iliyokuwa imeshuka toka mbinguni, na kuanguka katika dunia. Nayo ikapewa ufunguo wa shimo ndefu la kuzimu.
2Nyota ile ikafungua hilo shimo. Moshi unaokuwa kama moshi wa furu kubwa ukapanda toka ndani ya shimo lile. Giza la ule moshi uliotoka ndani ya lile shimo ulifunika jua na anga.
3Nzige wakatokea katika ule moshi, na kusambaa juu ya dunia. Nao wakapewa nguvu zinazokuwa kama za nge.
4Wakaambiwa wasiharibu majani yoyote wala mumea wowote, wala muti wowote, lakini wawatese watu wasiokuwa na chapa ya muhuri wa Mungu kwenye paji za nyuso zao.
5Nzige wale hawakupewa amri ya kuwaua watu wale, lakini wawatese kwa muda wa miezi mitano. Na maumivu yao yalikuwa kama vile nge wakati anapouma mutu.
6Na kwa muda ule, watu watatafuta kifo, lakini hakitawapata. Watatamani kufa, lakini kifo kitawakimbia.
7Umbo la nzige wale lilifanana na farasi waliopambwa kwa kupigana vita. Juu ya vichwa vyao kulikuwa vitu vinavyofanana na taji za zahabu, na nyuso zao zilifanana kama nyuso za watu.
8Nywele zao zilikuwa sawa nywele za wanawake, na meno yao yalikuwa kama meno ya simba.
9Na juu ya vifua vyao kulikuwa vitu vinavyofanana na ngao za chuma. Na sauti ya mabawa yao ilikuwa kama uvumi wa magari yanayovutwa na farasi wengi wanaokimbia mbio kwenda kwa vita.
10Walikuwa na mikia kama ya nge na yenye kuchoma kama miiba. Uwezo wao wa kuwatesa watu kwa muda wa ile miezi mitano ulikuwa ndani ya mikia yao.
11Na mufalme wao, ndiye malaika wa lile shimo ndefu la kuzimu, jina lake liliitwa kwa Kiebrania “Abidani” na kwa kigriki “Apolioni” (maana yake “Mwangamizaji”).
12Hasara ya kwanza imepita, na nyuma ya ile kutatokea hasara zingine mbili.
13Malaika wa sita akapiga baragumu. Halafu nikasikia sauti moja ikitokea kwenye pembe ine za mazabahu ya zahabu iliyokuwa mbele ya Mungu.
14Sauti ile ikamwambia yule malaika wa sita aliyeshika baragumu hivi: “Uwafungue wale wamalaika wane waliofungwa kwenye muto mukubwa Furati.”
15Wale wamalaika wane wakafunguliwa, nao walikuwa wamewekwa tayari kwa saa ile, siku, mwezi na mwaka ule, wapate kuua sehemu moja ya tatu ya wanadamu.
16Nikasikia hesabu ya makundi ya waaskari wapanda-farasi, nao walikuwa milioni mia mbili.
17Na katika maono yale, nikaona wale farasi pamoja na wale waaskari waliopanda juu yao. Waaskari wale walikuwa na ngao zenye rangi nyekundu kama moto na zingine za rangi ya samawi na ya kimanjano kama kiberiti. Vichwa vya farasi wale vilikuwa kama vichwa vya simba, na ndani ya vinywa vyao mulitoka moto, moshi na mawe ya viberiti.
18Na sehemu moja ya tatu ya wanadamu wakauawa kwa mapigo hayo matatu: kwa moto, moshi na viberiti vilivyotoka ndani ya vinywa vya wale farasi,
19kwa maana uwezo wa wale farasi ulikuwa ndani ya vinywa vyao na ya mikia yao vilevile. Mikia yao ilikuwa kama kichwa cha nyoka, na kwa mikia hiyo waliweza kuzuru watu.
20Watu waliobaki bila kuuawa na yale mapigo hawakuachana na sanamu walizojitengenezea wao wenyewe. Hawakuacha kuabudu pepo, sanamu za zahabu, za feza, za shaba, za mawe na za miti zisizoweza kuona, wala kusikia, wala kutembea.
21Watu wale hawakuacha hata matendo yao ya uuaji, ya uchawi, ya uasherati na ya wizi.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.