Ezekieli 46 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mulango wa kiwanja cha ndani unaoelekea upande wa mashariki utafungwa siku zote sita za kazi. Siku za Sabato na siku za mwandamo wa mwezi utafunguliwa.

2Tokea inje, mufalme ataingia katika baraza ya ndani kwa kupitia kwenye mulango wa baraza hiyo. Naye atasimama karibu na nguzo ya mulango, wakati makuhani wanateketeza sadaka zake za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Kisha mufalme huyo atainama chini kwenye mulango kwa kuabudu na kisha atatoka inje. Mulango utabaki wazi mpaka magaribi.

3Kila siku ya Sabato na sikukuu ya mwandamo wa mwezi, watu wote wataniabudu mimi Yawe mbele ya mulango.

4Siku ya Sabato, mufalme ataleta kwa Yawe wana-kondoo sita na kondoo dume mumoja wote wasiokuwa na kilema kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto.

5Pamoja na kila kondoo dume, ataleta sadaka ya unga litre kumi na saba na nusu, lakini pamoja na kila mwana-kondoo ataleta sadaka yoyote anayoweza. Na kwa kila sadaka ya unga, ataleta litre tatu za mafuta.

6Wakati wa sikukuu ya mwandamo wa mwezi atatoa mwana-ngombe dume, wana-kondoo sita, na kondoo dume mumoja; wote wasiokuwa na kilema.

7Pamoja na kila ngombe dume na kila kondoo dume anayetolewa sadaka, kunapaswa kuwa litre kumi na saba na nusu za unga, na pamoja na kila mwana-kondoo, kunapaswa kuwa chochote ambacho mufalme anatoa. Tena kwa kila sadaka ya unga, kunapaswa kutolewa litre tatu za unga.

8Mufalme anapotoka anapaswa kutokea kwa njia ileile aliyoingilia.

9Watu wanapokuja kumwabudu Yawe wakati wa sikukuu yoyote, wale walioingia kwa njia ya mulango wa kaskazini, watatoka kwa njia ya mulango wa kusini; na wale walioingia kwa mulango wa kusini, watatoka kwa njia ya mulango wa kaskazini. Mutu asirudi kwa njia ya mulango alioingilia, lakini atatoka kwa njia ya mulango unaokuwa mbele yake.

10Mufalme ataingia ndani watu wanapoingia, na atatoka wanapotoka.

11Wakati wa siku za sikukuu na siku zilizopangwa, sadaka za unga zitakuwa litre kumi na saba zikiandamana na kila ngombe dume au kondoo dume, na chochote ambacho anayeabudu anaweza kutoa kwa kila mwana-kondoo. Kwa kila sadaka ya unga atatoa litre tatu za mafuta.

12Mufalme anapotaka kumutolea Yawe sadaka kwa mapenzi yake, ikiwa ni sadaka ya kuteketezwa au sadaka ya amani, watamufungulia mulango wa kiwanja cha ndani unaoelekea upande wa mashariki. Atatoa sadaka kama anavyofanya siku ya Sabato, na anapotoka, mulango ufungwe nyuma yake.

Sadaka za kila siku

13Kila siku asubui mutamutolea Yawe mwana-kondoo wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema, ambaye atateketezwa kwa moto.

14Vilevile kila siku, sadaka ya kilo mbili za unga itatolewa asubui pamoja na litre moja ya mafuta ya muzeituni yakichanganywa na unga. Inafaa kufuata maagizo za sadaka hii kwa Yawe milele.

15Mwana-kondoo, unga na mafuta vinapaswa kutolewa kila siku asubui kwa Yawe milele.

Mufalme na inchi

16Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ikiwa mufalme anamupa mumoja kati ya wana wake zawadi ya sehemu ya inchi, zawadi hiyo itakuwa mali ya huyo kijana milele kama sehemu ya jamaa yake.

17Lakini ikiwa atamupa mumoja kati ya watumishi wake sehemu yoyote ya inchi yake, zawadi hiyo itakuwa mali yake mpaka mwaka wa kuachwa huru. Kwa hiyo ndipo itamurudilia tena mufalme. Ni yeye tu na watoto wake wa kiume wanaoweza kuirizi kwa siku zote. Ang. Law 25.10

18Mufalme hapaswi kunyanganya hata kidogo mali ya watu. Sehemu ya inchi yoyote anayowapa watoto wake wa kiume inapaswa kutokana na eneo lake mwenyewe. Hivyo hatawatesa watu wangu kwa kuwanyanganya urizi wao.

Mafika ya hekalu

19Kisha, yule mutu akanipitisha kwenye nafasi ya kupitia kuingia kwenye vyumba vitakatifu vya makuhani vinavyoelekea upande wa kaskazini, karibu na mulango wa kusini wa kiwanja cha ndani. Akanionyesha nafasi moja, upande wa magaribi wa vyumba,

20akaniambia hivi: Hapa ndipo makuhani watakapopikia nyama ya sadaka ya malipo ya kosa, sadaka ya kusamehewa zambi, na kupika sadaka za vyakula. Kwa hiyo hawatoki inje ya baraza na chochote, kusudi watu wasijichafue kwa kugusa kitu kitakatifu.

21Kisha akanipeleka kwenye kiwanja cha inje, akanipitisha karibu na pembe ine za kiwanja; kwa kila pembe kulikuwa kiwanja kidogo,

22ni kusema, kwa pembe ine za kiwanja kulikuwa viwanja vine vidogo vya urefu wa metre makumi mbili na upana metre kumi na tano.

23Kulikuwa ukuta kukizunguka kila kiwanja, na mafika mbele ya ukuta.

24Yule mutu akaniambia: Haya ni mafika ambako watumishi wa nyumba ya Yawe watapikia sadaka watu wanazoleta.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help