Zaburi 77 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maombi ya kufarijiwa wakati wa shida

1Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa Yedutuni. Zaburi ya Asafu.

2Ninamulilia Mungu kwa sauti.

Kwa sauti ninamulilia Mungu, anisikie.

3Wakati wa taabu ninamutafuta Bwana wetu;

ninamunyooshea mikono yangu usiku bila kuchoka,

lakini sifarijiwi na mutu yeyote.

4Ninafikiri juu ya Mungu na kuugua;

ninamukumbuka na kufa moyo.

5Unanizuiza hata kupata usingizi,

ninahangaika hata siwezi kusema.

6Ninafikiri juu ya siku za zamani;

ninakumbuka miaka ya hapo kale.

7Usiku ninawazawaza;

moyo wangu unafikiri,

nayo roho yangu inajiuliza:

8“Bwana ametuachilia kabisa?

Hatapendezwa tena nasi?

9Wema wake umekwisha kabisa?

Hatatimiza tena ahadi zake?

10Mungu amesahau kuwa na huruma?

Hasira yake imeondoa rehema yake?”

11Kisha nikasema: “Kinachoniumiza zaidi ni kwamba

Mungu Mukubwa hatendi tena kitu kwa ajili yetu!”

12Nitayakumbuka matendo yako, ee Yawe,

nitafikiri juu ya maajabu yako ya hapo kale.

13Ninafikiri juu ya kazi zako,

ninawaza juu ya matendo yako makubwa.

14Kila unachofanya, ee Mungu, ni kitakatifu.

Ni mungu gani anayekuwa mukubwa kama Mungu wetu?

15Wewe ni Mungu unayetenda maajabu;

wewe umeyaonyesha mataifa uwezo wako.

16Kwa mukono wako wa kuume uliwakomboa watu wako;

uliwakomboa wazao wa Yakobo na Yosefu.

17Maji yalipokuona, ee Mungu,

maji yalipokuona, yaliogopa sana;

bahari ilitetemeka mpaka chini.

18Mawingu yalinyesha mvua nyingi,

ngurumo zikavuma katika anga,

mishale ya umeme ikaangaza kila upande.

19Kishindo cha ngurumo yako kilitokea katika zoruba,

umeme wako ukaangaza ulimwengu,

dunia ikatikisika na kutetemeka.

20Wewe ukajifanyia njia juu ya bahari;

ulitembea juu ya maji yale mengi,

lakini pahali ulipopita hapakuonekana.

21Uliwaongoza watu wako kama kondoo,

chini ya uongozi wa Musa na Haruni.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help