1 Samweli 8 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Waisraeli wanaomba kuwa na mufalme

1Samweli alipokuwa muzee, aliwafanya wana wake kuwa waamuzi wa Waisraeli.

2Mwana wake wa kwanza aliitwa Yoeli, na wa pili aliitwa Abiya. Wote wawili walikuwa waamuzi kule Beri-Seba.

3Lakini watoto hao hawakufuata mwenendo wa baba yao. Lakini walianza kujitafutia faida. Wakapokea kituliro na kupotosha haki.

4Basi, viongozi wote wa Waisraeli walikusanyika pamoja, na kumwendea Samweli katika muji wa Rama,

5wakamwambia: “Angalia, wewe sasa ni muzee na watoto wako hawafuati mwenendo wako. Hivyo, utuchagulie mufalme wa kututawala sawa vile inavyokuwa kwa mataifa mengine.”

6Lakini jambo la Waisraeli la kutaka wapewe mufalme wa kuwatawala, halikumupendeza Samweli. Naye akamwomba Yawe.

7Yawe akamwambia: “Sikiliza kila kitu ambacho watu wanakuambia; maana hawajakukataa wewe, lakini wamenikataa mimi kuwa mufalme juu yao.

8Tangu nilipowatoa Misri, wameniacha mimi, wamekuwa wakiitumikia miungu mingine mpaka leo. Sasa hayo matendo ambayo wamekuwa wakinitendea mimi, ndiyo wanayokutendea na wewe.

9Basi, uwasikilize, lakini uwaonye vikali, na uwaelezee waziwazi jinsi mufalme atakayewatawala atakavyowatendea.”

10Samweli akawaambia wale watu waliokuwa wanaomba wapewe mufalme maneno yote ya Yawe.

11Samweli aliwaambia: “Hivi ndivyo mufalme wenu atakayewatawala atakavyowatendea: wana wenu atawafanya wakuwe waendeshaji wa magari yake, na wengine kuwa waaskari wapanda-farasi wake, na wengine watapiga mbio mbele ya magari yake.

12Atajichagulia wengine wakuwe wakubwa wa makundi ya waaskari wake wa maelfu na wengine wakuwe wakubwa wa makundi ya watu makumi tano. Atawafanya wengine wamulimie mashamba yake na kuvuna mazao yake. Atawafanya wengine vilevile wamutengenezee silaha za vita, na wengine wamutengenezee vyombo vya magari yake.

13Wabinti zenu atawatwaa kuwa watengenezaji wa marasi, wengine wapishi na wengine wachomaji wa mikate.

14Atayatwaa mashamba yenu mazuri, mashamba ya mizeituni, na mashamba ya mizabibu na kuwapa watumishi wake.

15Atatwaa sehemu ya kumi ya ngano zenu na ya zabibu zenu na kuwapa wakubwa wake na watumishi wake.

16Atatwaa watumishi wenu na wajakazi wenu na ngombe wenu wazuri na punda wenu wazuri kabisa na kuwafanya wamufanyie kazi yake.

17Atatwaa sehemu ya kumi ya kondoo wenu. Na ninyi wenyewe mutakuwa watumwa wake.

18Wakati huo, ninyi mutalalamika kwa sababu ya mufalme wenu ambaye mumejichagulia ninyi wenyewe. Lakini Yawe hatawajibu.”

19Hata hivyo watu walikataa kumusikiliza Samweli, wakasema: “Hapana! Sisi tutakuwa na mufalme juu yetu,

20kusudi nasi vilevile tukuwe sawa mataifa mengine. Mufalme wetu, atatuamulia haki zetu, atatuongoza na kutupigania vita vyetu.”

21Samweli alipokwisha kusikiliza kila kitu walichosema, akaenda na kumwelezea Yawe.

22Yawe akamwambia Samweli: “Uwasikilize na uwapatie mufalme.” Kisha Samweli akawaambia Waisraeli warudie kwao, kila mutu katika muji wake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help