Yoeli 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maonyo juu ya siku ya Yawe

1Mupige baragumu kule Sayuni;

mupige kelele la kujulisha hatari kule juu ya mulima mutakatifu!

Mutetemeke enyi wakaaji wa Yuda,

maana siku ya Yawe inakuja,

siku hiyo iko karibu!

2Hiyo ni siku ya giza na huzuni;

siku ya mawingu na giza nene.

Jeshi kubwa linakaribia

kama giza linalofunikia milima.

Namna hiyo haijapata kuwa hata kidogo

wala haitaonekana tena

katika vizazi vyote vinavyokuja.

3Kama vile moto unavyoteketeza,

Jeshi hilo linaharibu kila kitu mbele yake

na kuacha nyuma kila kitu kinateketezwa;

mbele ya kupita kwao, inchi ni kama bustani ya Edeni,

lakini wakisha kupita, ni jangwa tupu.

Hakuna kinachoweza kuponyoka!

4Wanaonekana kama farasi,

wanashambulia kama farasi wa vita.

5Wanaporukaruka kwenye vilele vya milima,

wananguruma kama magari yenye kukokotwa na farasi,

wanavuma kama moto wa majani yenye kukauka.

Wamejipanga kama kundi kubwa la waaskari

tayari kabisa kufanya vita.

6Wanapokaribia, watu wanajaa hofu,

nyuso zao zinawaivya.

7Wanashambulia kama mashujaa wa vita;

wanapanda juu ya kuta kama waaskari.

Wote wanakwenda mbele moja kwa moja,

bila hata mumoja wao kubadilisha njia.

8Hakuna anayemusukuma mwenzake;

kila mumoja anafuata njia yake.

Wanapita kati ya vizuizi vya silaha,

wala hakuna kinachoweza kuwazuia.

9Wanashambulia muji,

wanakimbia juu ya ukuta;

wanapanda juu ya nyumba na kuingia,

wanapenya katika madirisha kama wezi.

10Inchi inatetemeka mbele yao,

mbingu zinatikisika.

Jua na mwezi vinatiwa giza,

nazo nyota zinaacha kuangaza.

11Yawe anaamuru kundi lake kwa sauti;

waaskari wake ni wengi sana,

wanaomutii hawahesabiki.

Siku ya Yawe kweli ni kubwa na ya kutisha sana!

Nani atakayeweza kuivumilia? Mwito wa kumurudilia Yawe

12Lakini hata sasa,

munirudilie kwa moyo wote,

kwa kufunga kula, kwa kulia na kuomboleza.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

13Munapasua nguo zenu kwa kuonyesha huzuni,

lakini inafaa mioyo yenu ipasuke vilevile.

Murudilie Yawe, Mungu wenu.

Yeye amejaa huruma na rehema,

hakasiriki upesi,

ni mwingi wa wema,

na tayari kubadilisha nia zake kusudi asiazibu.

14Labda Yawe, Mungu wenu, atabadilisha nia

na kuwapa baraka ya mazao,

mutaweza kumutolea sadaka za chakula na kinywaji.

15Mupige baragumu kule Sayuni!

Mutoe amri watu wafunge kula;

muwaalike kuja kwa mukutano wa kidini.

16Muwakusanye watu wote,

muwatakase watu.

Muwalete wazee,

muwakusanye watoto,

hata watoto wanaonyonya.

Bwana-arusi na bibi-arusi

watoke katika vyumba vyao.

17Kati ya mazabahu na mulango wa hekalu,

makuhani wanaomutumikia Yawe,

walie na kuomba wakisema:

Uwahurumie watu wako, ee Yawe.

Usiyaache mataifa mengine yatuzarau

na kutuchekelea yakisema:

Yuko wapi basi Mungu wao?

Mungu ataifanikisha inchi

18Yawe anaipenda inchi yake

anawahurumia watu wake.

19Alisikiliza, akajibu maombi yao, akasema:

Sasa nitawapa tena ngano, divai na mafuta,

nanyi mutashiba navyo.

Sitawafanya muzarauliwe tena na mataifa.

20Nitawaondoa hao waadui wanaotoka kaskazini,

nitawafukuza mpaka katika jangwa;

waaskari wa mbele nitawatupa katika bahari ya Chumvi

na wale wa nyuma katika bahari ya Mediteranea.

Watatoa uvundo na harufu mbaya,

hao ambao wamefanya maovu makubwa.

21Usiogope, ewe inchi,

lakini ufurahi na kushangilia,

maana Yawe ametenda mambo makubwa.

22Musiogope, enyi nyama,

malisho katika mbuga yamekuwa mazuri,

miti inazaa matunda yake,

mizabibu na mitini zinazaa kwa wingi.

23Mufurahi, enyi watu wa Sayuni,

mushangilie kwa sababu ya Yawe, Mungu wenu,

maana amewapa mvua zinazowafalia,

amewapa mvua ya kutosha:

mvua za kwanza na mvua za katikati kama pale mbele.

24Nafasi ya kupepetea itajaa ngano,

vikamulio vitafurika divai na mafuta.

25Nitawarudishia miaka ile iliyokuliwa na nzige,

kila kitu kilichokuliwa na tunutu, parare na panzi,

hilo kundi kubwa nililowaletea!

26Mutapata chakula kingi na kutosheka;

mutalisifu jina la Yawe, Mungu wenu,

aliyewatendea mambo ya ajabu.

Watu wangu, hawatazarauliwa tena hata kidogo.

27Mutatambua kwamba mimi niko kati yenu,

enyi Waisraeli;

na kwamba mimi Yawe,

ndimi Mungu wenu wala hakuna mwingine.

Watu wangu, hawatazarauliwa tena hata kidogo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help