1 Samweli 20 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yonatani anamusaidia Daudi

1Daudi alikimbia kutoka Nayoti katika Rama, akaenda mpaka kwa Yonatani, akamwambia: “Nimefanya nini? Kosa langu ni gani? Nimemutendea baba yako zambi gani hata anajaribu kuyaangamiza maisha yangu?”

2Yonatani akamujibu: “Jambo hilo lipite mbali nawe. Hautakufa. Baba yangu hafanyi jambo lolote, likuwe kubwa au dogo, bila kunielezea. Hata jambo hili hawezi kunificha. Sivyo inavyokuwa hata kidogo.”

3Daudi akaapa vilevile: “Hakika baba yako anajua vizuri kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako. Anafikiri kukuficha juu ya jambo hili kusudi usihuzunike atakapolitenda. Lakini kweli, kama Yawe anavyoishi na kama wewe mwenyewe unavyoishi, kati yangu na lufu kuna hatua moja tu!”

4Yonatani akamwambia: “Neno lolote utakalosema nitakutendea nalo.”

5Daudi akamwambia: “Kesho ni sikukuu ya mwandamo wa mwezi, nami nilipaswa kuwa kwenye meza kwa kula pamoja na mufalme. Lakini uniache, niende kujificha kule katika shamba mpaka siku ya tatu magaribi.

6Baba yako akitambua kwamba siko, basi umwambie: ‘Daudi amenisihi nimupe ruhusa kusudi aende mbio katika muji wake Betelehemu, kuhuzuria kwa sadaka ya kila mwaka pamoja na jamaa yake’.

7Ikiwa ataona hilo ni sawa, basi, ujue kwamba mambo yangu, mimi mutumishi wako, yako sawa. Kama sivyo, kusudi lake juu yangu ni baya.

8Hivyo unitendee mema maana umefanya agano nami, mimi mutumishi wako, mbele ya Yawe. Lakini, kama nimefanya kosa basi, uniue wewe mwenyewe. Kwa nini unipeleke kwa baba yako kusudi aniue?”

9Yonatani akamujibu: “Wazo lile likuwe mbali nawe. Hakika, kama ningejua kwamba baba yangu amekusudia mabaya juu yako nisingekuficha.”

10Daudi akauliza: “Nitajua namna gani ikiwa baba yako atakujibu kwa ukali?”

11Yonatani akamujibu: “Kuja tuende ndani ya shamba!” Basi, wakaenda.

12Yonatani akamwambia Daudi: “Yawe, Mungu wa Israeli, akuwe mushuhuda kati yetu. Kesho au kesho kutwa, wakati kama huu nitamwuliza baba yangu. Ikiwa musimamo wake juu yako ni muzuri nitakuelezea.

13Yawe aniue ikiwa Saulo anakusudia kukuzuru nami nisipokujulisha kusudi uende pahali pa mbali ambapo utakuwa salama. Yawe akuwe pamoja nawe kama alivyokuwa pamoja na baba yangu.

14Ikiwa nitaendelea kuishi basi, unionyeshe wema wa Yawe, kusudi nisikufe,

15tena usiache kuitendea jamaa yangu kwa uaminifu milele. Na Yawe atakapowateketeza waadui zako kutoka katika dunia,

16ninaomba jina langu lisikatiliwe kabisa kutoka katika jamaa yako. Yawe awalipize kisasi waadui zako.”

17Kwa mara ingine tena, Yonatani alimwambia Daudi aape kulingana na upendo wake kwake yeye Yonatani, maana alimupenda Daudi kama vile anavyojipenda yeye mwenyewe.

18Kisha akamwambia Daudi: “Kwa sababu kesho ni sikukuu ya mwandamo wa mwezi, watu wataona wazi kwamba hauko, maana kiti chako kitakuwa wazi.

19Tena, kesho kutwa, watu watakukosa kabisa. Siku hiyo uende pahali ambapo ulijificha wakati jambo hili lilipokuwa lingali motomoto, ujifiche nyuma ya lundo la mawe.

20Mimi nitapiga mishale mitatu kandokando kama vile ninapima shabaha fulani.

21Nitamutuma mutumishi wangu aende kuitafuta mishale hiyo. Kama nikimwambia: ‘Angalia, mishale hiyo iko upande ule wako, uikamate’, hiyo itakuwa na maana kwamba uko salama, nawe utajitokeza kutoka pahali ulipojificha, maana, kama vile Yawe anavyoishi, kuna amani kwako, na hakuna hatari.

22Lakini nikimwambia ‘Angalia, mishale iko mbele yako’, kwa hiyo, ondoka. Yawe atakuwa anataka uende mbali.

23Kulingana na ahadi tulizowekeana, Yawe atakuwa mushuhuda kati yetu milele.”

24Basi, Daudi akajificha katika shamba. Wakati wa sikukuu ya mwandamo wa mwezi, mufalme Saulo akaikaa kwenye meza kwa kula.

25Kama ilivyokuwa kawaida yake, mufalme aliikaa kwenye kiti chake kilichokuwa karibu na ukuta. Yonatani akaikaa mbele kuelekea mufalme na Abeneri akaikaa karibu na mufalme. Lakini nafasi ya Daudi ikakuwa wazi.

26Siku hiyo, Saulo hakusema neno lolote, maana alifikiri kwamba labda Daudi amepatwa na tatizo au yeye si safi kwa kuhuzuria sikukuu hiyo.

27Siku ya pili ya sikukuu ya mwandamo wa mwezi, nafasi ya Daudi ilikuwa tu wazi. Saulo akamwuliza mwana wake Yonatani: “Kwa nini Daudi mwana wa Yese hakukuja kwenye chakula jana na leo?”

28Yonatani akamujibu: “Alinisihi sana nimuruhusu aende Betelehemu.

29Aliniambia: ‘Uniruhusu niende kwa jamaa yangu, kwa maana wanatolea sadaka kule katika muji, na ndugu yangu amenitaka nikuwe pale. Hivyo kama nimepata kukubaliwa mbele yako, uniruhusu niende kwa wandugu zangu’. Ndiyo maana hayuko hapa kushiriki chakula cha mufalme.”

30Kwa hiyo Saulo akawaka hasira juu ya Yonatani, akamwambia: “Mwana wa imbwa wewe! Ninajua kwamba umejichagulia mwana wa Yese kwa ajili ya haya yako mwenyewe, na kumufezehesha mama yako!

31Wewe, haujui kwamba wakati mwana wa Yese angali anaishi katika dunia, wewe hautaweza kuwa na uhakika wa kuwa mufalme wa inchi hii? Sasa hivi kwenda umulete hapa kwangu, kwa sababu anapaswa kuuawa.”

32Yonatani akamujibu: “Kwa nini auawe? Amefanya nini?”

33Lakini Saulo akamutupia Yonatani mikuki kusudi amwue. Naye Yonatani akatambua kwamba baba yake alikuwa amekusudia kumwua Daudi.

34Halafu Yonatani, akiwa amekasirika sana, aliondoka kwenye meza kwa haraka, wala hakukula chakula chochote siku hiyo ya pili ya sikukuu ya mwandamo mwezi. Yonatani alihuzunika sana juu ya Daudi kwa sababu baba yake alikuwa amemupatisha haya.

35Kesho yake asubui, Yonatani alikwenda kule katika shamba kwa kukutana na Daudi kama walivyoagana. Alikwenda kule na kijana mumoja wa kiume.

36Alipofika kule alimwambia yule kijana wake: “Kimbia uitafute mishale ambayo nitapiga.” Yule kijana alipokuwa anakimbia Yonatani akapiga mushale mbele yake.

37Yule kijana alipofika pahali ambapo mushale uliangukia, Yonatani akamwambia: “Mushale uko mbele yako.

38Fanya haraka na usisimame tu pahali pale.” Yule kijana alikusanya mishale na kumwendea bwana wake.

39Lakini yule kijana hakujua kitu chochote juu ya maana ya kitendo hicho. Waliojua ni Yonatani na Daudi tu.

40Yonatani akamupatia yule kijana silaha zake na kumwambia: “Kwenda urudi katika muji.”

41Yule kijana alipokwisha kuondoka, Daudi akasimama na kutoka pahali alipojificha karibu na lundo la mawe. Aliinama chini kwa heshima mara tatu mbele ya Yonatani. Wote wawili, Daudi na Yonatani, wakakumbatiana na kulia. Daudi alikuwa na uchungu zaidi kuliko Yonatani.

42Halafu Yonatani akamwambia Daudi: “Uende na amani. Tumekwisha wote kuapa kwa jina la Yawe kwamba Yawe akuwe mushuhuda kati yetu milele, na kati ya wazao wangu na wazao wako milele.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help