Yobu 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Jaribu la pili

1Ikatokea tena siku ingine, wamalaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Yawe. Shetani akakuja kuwa pamoja nao.

2Yawe akamwuliza Shetani: “Unatoka wapi wewe?”

Naye Shetani akamujibu Yawe: “Ninatoka kutembeatembea na kuzungukazunguka katika dunia.”

3Yawe akamwambia Shetani: “Umemwona vizuri mutumishi wangu Yobu? Katika dunia hakuna mwingine anayekuwa kama yeye. Yeye ni mutu mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu. Yeye anadumu katika ukamilifu, ingawa wewe umenisukuma nimwangamize bure.”

4Shetani akamujibu Yawe: “Ngozi kwa ngozi! Mutu anatoa kila kitu anachokuwa nacho kusudi aokoe maisha yake.

5Lakini sasa, unyooshe mukono wako umuguse mwili wake. Utaona namna atakutukana waziwazi.”

6Yawe akamwambia Shetani: “Basi, unaweza kumufanya vile unavyotaka, lakini usimwue tu.”

7Kwa hiyo Shetani akaondoka mbele ya Yawe, akamutesa Yobu kwa vidonda vikali tangia kwenye miguu yake mpaka kwenye kichwa chake.

8Yobu akatwaa kigae, akajikuna nacho na kuikaa kwenye majivu.

9Muke wake akamwambia: “Unaendelea kushikilia ukamilifu wako? Umutukane Mungu, ukufe.”

10Akamujibu: “Wewe unasema kama wanawake wapumbafu. Tukipokea mazuri kutoka kwa Mungu, kwa nini tukatae kupokea vilevile mabaya kutoka kwake?” Katika mambo hayo yote, Yobu hakusema neno lolote la kumukosea Mungu.

Warafiki watatu wa Yobu wanafika

11Warafiki watatu wa Yobu walisikia juu ya hasara zote zilizomupata Yobu, wakaamua kwa pamoja waende kumupa pole na kumufariji. Majina yao ni: Elifasi kutoka inchi ya Temani, Bildadi wa inchi ya Suhi na Zofari wa inchi ya Namati.

12Walipomwona kwa mbali hawakumutambua. Basi, wakaanza kulalamika na kulia. Wakapasua nguo zao, wakarusha mavumbi katika anga na juu ya vichwa vyao.

13Kisha wakaikaa kwenye udongo pamoja na Yobu kwa siku saba, muchana na usiku, bila kumwambia neno lolote maana waliona mateso yake kuwa makubwa sana.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help