1Kisha, Musa pamoja na Waisraeli wakamwimbia Yawe wimbo huu:
“Nitamwimbia Yawe,
maana ameshinda kwa utukufu;
farasi na mupanda-farasi wake
amewatupa katika bahari.
2Yawe ananijalia nguvu na uwezo,
yeye mwenyewe ndiye anayeniokoa.
Yeye ni Mungu wangu
nami nitamusifu;
ni Mungu wa baba yangu
nami nitamutukuza.
3Yawe ni shujaa kwa vita;
Yawe ndilo jina lake.
4“Magari na majeshi ya mufalme wa Misri
ameyatumbukiza ndani ya bahari;
majemadari wake wachaguliwa
wamezama katika bahari Nyekundu.
5Vilindi vya maji vimewafunika,
wameporomoka katika bahari kama jiwe.
6“Mukono wako wa kuume, ee Yawe,
unatukuka kwa nguvu;
kwa mukono wako wa kuume, ee Yawe,
unawaponda waadui.
7Kwa wingi wa ukubwa wako
unawaangamiza wapinzani wako;
unawapulizia kasirani yako
nayo inawateketeza kama maganda.
8Kwa pumzi ya pua yako
maji yalilundikana,
mawimbi yakasimama wima kama ukuta;
vilindi katikati ya bahari vikagandamana.
9Adui akajisemesha:
‘Nitawafuata na kuwakamata;
nitagawanya vitu mpaka hamu yangu iishe.
Tutafuta upanga wetu,
tutawaangamiza kwa mukono wetu.’
10Lakini wewe
uliuvumisha upepo wako,
nayo bahari ikawafunika.
Walizama ndani ya maji kama risasi.
11“Ewe Yawe,
ni nani kati ya miungu anayelingana nawe?
Ni nani aliyekuwa kama wewe
unayekuwa mutakatifu mukubwa,
unayetisha kwa matendo matukufu,
unayetenda mambo ya ajabu?
12Ulinyoosha mukono wako wa kuume,
nayo inchi ikawameza waadui zetu.
13“Kwa wema wako mukubwa
umewaongoza watu uliowakomboa,
kwa nguvu yako
umewaongoza kwenye makao yako matakatifu.
14Watu wa mataifa wamesikia hayo wakatetemeka;
Wafilistini wamepatwa na kitisho.
15Wakubwa wa Edomu
wamefazaishwa;
viongozi wa Moabu
wamepatwa na woga mukubwa;
wakaaji wote wa Kanana
wamevunjika moyo.
16Kitisho na hofu vimewashika.
Kwa sababu ya ukubwa wa nguvu zako,
wao wamenyamaza kimya kama jiwe,
mpaka watu wako, ee Yawe,
wapite,
mpaka watu wale uliowakomboa
wamewapita.
17Wewe utawaleta watu wako
na kuwapanda juu ya mulima wako,
pale ulipochagua, ee Yawe,
kuwa makao yako,
pahali patakatifu, ee Yawe,
ulipojenga kwa mikono yako.
18“Wewe, ee Yawe,
unatawala milele na milele.”
19Wakati farasi wa mufalme wa Misri na magari yake pamoja na wapanda-farasi wake walipoingia pahali pakavu katika bahari, Yawe aliyarudisha maji ya bahari yakawafunika. Lakini Waisraeli waliendelea kutembea pakavu katikati ya bahari.
20Basi nabii Miriamu, dada ya Haruni, akatwaa ngoma katika mukono, na wanawake wengine wote wakamufuata wakiwa na ngoma zao ndogo wakicheza.
21Miriamu akawaongoza kwa kuimba:
“Mumwimbie Yawe
maana ameshinda kwa utukufu.
Farasi na mupanda-farasi wake
amewatupa ndani ya bahari.”
Maji machungu22Kisha, Musa akawaongoza Waisraeli kutoka bahari Nyekundu, wakaenda mpaka kwenye jangwa la Suri. Wakasafiri kwa muda wa siku tatu katika jangwa bila kuona maji yoyote.
23Walipofika pahali panapoitwa Mara, hawakuweza kunywa maji ya Mara kwa sababu yalikuwa machungu. Kwa sababu hiyo pahali pale pakaitwa Mara, ni kusema “Uchungu”.
24Basi, watu wote wakamunungunikia Musa wakisema: “Sasa tutakunywa nini?”
25Halafu Musa akamulilia Yawe, naye akamwonyesha kipande cha muti, na Musa akakitumbukiza katika maji. Maji hayo yakakuwa mazuri.
Kule Mungu aliwapa Waisraeli sharti na agizo, kusudi awapime,
26akawaambia: “Ikiwa mutaisikiliza kwa uaminifu sauti yangu mimi Yawe, Mungu wenu, kutenda yale yanayokuwa sawa mbele yangu, na kuheshimu amri na masharti yangu yote, basi, mimi sitawaletea yale magonjwa niliyowaletea Wamisri. Kwa sababu, mimi ni Yawe ninayewaponya ninyi.”
27Kisha Waisraeli wakafika kule Elimu ambako kulikuwa chemichemi kumi na mbili na mingazi makumi saba. Wakapiga kambi yao kule karibu na maji.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.