2 Wafalme 18 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mufalme Hezekia wa Yuda(2 Sik 29.1-3; 31.1)

1Katika mwaka wa tatu wa utawala ya Hoshea mwana wa Ela, mufalme wa Israeli, Hezekia mwana wa Ahazia, mufalme wa Yuda, alianza kutawala.

2Alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala. Akatawala miaka makumi mbili na tisa akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Abi binti ya Zakaria.

3Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe, kama vile Daudi babu yake alivyotenda.

4Aliharibu nafasi zote za kuabudu miungu na kuvunja nguzo na kukata Ashera. Vilevile, alivunja nyoka ya shaba ambayo Musa alitengeneza, iliyoitwa Nehustani. Mpaka wakati ule, watu wa Israeli walikuwa wakiitambikia.

5Hezekia alimutegemea Yawe, Mungu wa Israeli; hakuna aliyekuwa kama yeye kati ya wafalme wa Yuda waliomufuata au waliomutangulia.

6Yeye hakumwasi Yawe wala hakuacha kumufuata, lakini alishika amri ambazo Yawe alimupa Musa.

7Basi, Yawe alikuwa pamoja naye, na alimwezesha kwa kila jambo alilotenda. Alimwasi mufalme wa Asuria na kukataa kumutumikia.

8Aliwapiga Wafilistini mpaka muji wa Gaza na inchi iliyouzunguka, kuanzia kwenye munara wa walinzi mpaka muji wenye kuta.

9Katika mwaka wa ine wa utawala wa Hezekia, ambao vilevile ulikuwa mwaka wa saba wa utawala wa Hoshea mwana wa Ela mufalme wa Israeli, Salmanaseri mufalme wa Asuria alishambulia muji wa Samaria na kuuzunguka.

10Kwa mwisho wa mwaka wa tatu Waasuria waliuteka muji wa Samaria. Ilikuwa katika mwaka wa sita wa utawala wa Hezekia na vilevile mwaka wa tisa wa utawala wa Hoshea mufalme wa Israeli, muji wa Samaria ulipotekwa.

11Mufalme wa Asuria akakamata watu wa Israeli na kuwapeleka mpaka Asuria na kuwaweka wengine wao katika muji wa Hala, na karibu ya Habori, muji wa Gozani, vilevile na wengine katika miji ya Wamedi,

12kwa sababu Waisraeli hawakutii sauti ya Yawe, Mungu wao, lakini walivunja agano lake, hata hawakusikia wala kutii yote Musa, mutumishi wa Yawe, aliyowaamuru.

Waasuria wanatisha Yerusalema(2 Sik 32.1-19; Isa 36.1-22)

13Katika mwaka wa kumi na ine wa utawala wa mufalme Hezekia, mufalme Saniharibu wa Asuria aliishambulia miji yote yenye kuta ya Yuda na kuiteka.

14Hezekia akatuma ujumbe kwa Saniharibu kule Lakisi na kumwambia: “Nimefanya makosa. Tafazali, uache kunishambulia, nami nitalipa chochote unachotaka.” Mufalme wa Asuria akaagiza Hezekia amuletee kilo elfu kumi za feza na kilo elfu moja ya zahabu.

15Hezekia akamupelekea feza yote iliyokuwa katika nyumba ya Yawe na katika hazina za nyumba ya mufalme.

16Vilevile, akaondoa zahabu kutoka katika milango ya hekalu la Yawe na ile zahabu ambayo yeye mwenyewe aliiweka kwenye miimo ya mulango. Yote akamupelekea Saniharibu.

17Kisha mufalme wa Asuria alimutuma majemadari wakubwa watatu pamoja na kundi kubwa la waaskari kutoka Lakisi kwenda kwa mufalme Hezekia kule Yerusalema. Walisafiri na kufika Yerusalema. Nao walipofika waliingia na kusimama karibu na mufereji wa kisima kinachokuwa upande wa juu katika barabara kubwa inayoelekea kiwanja cha mufuaji wa nguo.

18Walipomwita mufalme Hezekia walipokelewa na Eliakimu mwana wa Hilkia ambaye alikuwa musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna aliyekuwa mwandishi wa mufalme, na Yoa mwana wa Asafu, mwandishi wa habari.

19Mumoja wa wale majemadari wakubwa akawaambia: “Mumwambie Hezekia kwamba mufalme mukubwa wa Asuria anamwuliza: Unategemea nini kwa kukazana kwako?

20Unazani kwamba maneno matupu ndiyo maarifa na nguvu katika vita? Ni nani unayemutegemea hata ukaniasi?

21Angalia sasa. Unategemea Misri, utete uliovunjika ambao utamuchoma mukono mutu yeyote atakayeutegemea. Hivi ndivyo mufalme wa Misri anavyokuwa kwa wote wale wanaomutegemea.

22Lakini hata kama mukiniambia: ‘Tunamutegemea Yawe, Mungu wetu’, si huyohuyo ambaye Hezekia aliziharibu nafasi zake zote za kuabudu kwenye vilima pamoja na mazabahu zake na kuwaambia watu wa Yuda na Yerusalema: Munapaswa kuabudu mbele ya mazabahu hii ya Yerusalema tu?

23Basi, mufanye mapatano na bwana wangu mufalme wa Asuria. Mimi nitawapatia farasi elfu mbili, kama mutaweza kupata waaskari wapanda-farasi.

24Hata kama munategemea Misri kupata magari ya vita na waaskari wapanda-farasi, hamuwezi kumurudisha nyuma mutu mumoja wa cheo cha chini sana kati ya watumishi wa bwana wangu.

25Zaidi ya hayo, munafikiri nimekuja bila amri ya Yawe kwa kuishambulia na kuiangamiza inchi hii? Yawe ndiye aliyeniambia: Uishambulie inchi hii na kuiangamiza!”

26Kisha Eliakimu mwana wa Hilkia, Sebuna na Yoa wakamujibu yule jemadari: “Tafazali, useme nasi kwa luga ya Kiaramea maana tunaielewa. Usiseme nasi kwa luga ya Kiebrania. Watu wanaokuwa juu ya ukuta wanasikia.”

27Yule jemadari akawaambia: “Munafikiri kwamba bwana wangu amenituma kutoa ujumbe huu kwa bwana wenu na kwenu tu? Maneno yangu ni vilevile kwa watu wanaoikaa juu ya ukuta! Bado kidogo wao kama vile ninyi watakula mavi yao wenyewe na kunywa mikojo yao wenyewe!”

28Kisha huyo jemadari akasimama, akalalamika na kusema kwa luga ya Kiebrania: “Musikilize maneno ya mufalme mukubwa, mufalme wa Asuria!

29Hivi ndivyo mufalme anavyosema: Musikubali Hezekia awadanganye, kwa sababu hataweza kuwaokoa toka katika mikono yangu.

30Musikubali awashawishi kusudi mumutegemee Yawe, akisema: ‘Yawe atatuokoa na muji huu hautatiwa katika mikono ya mufalme wa Asuria.’

31Musimusikilize Hezekia, maana mufalme wa Asuria anasema: ‘Mukuwe na amani nami na kujitoa kwangu. Kisha kila mumoja wenu ataweza kula matunda ya mizabibu yake mwenyewe na matunda ya tini yake mwenyewe na kunywa maji ya kisima chake mwenyewe,

32mpaka nitakapokuja na kuwapeleka katika inchi kama hii yenu, inchi yenye ngano na divai, inchi yenye mukate na mashamba ya mizabibu, inchi yenye mizeituni na asali, kusudi mupate kuishi, nanyi hamutakufa. Musimusikilize Hezekia anapowadanganya akisema: Yawe atatuokoa.

33Kuna yoyote kati ya miungu ya mataifa aliyeokoa inchi yake toka katika mikono ya mufalme wa Asuria?

34Iko wapi ile miungu ya Hamati na Arpadi? Iko wapi ile miungu ya Sefarwaimu, Hena na Iwa? Imeokoa Samaria toka katika mikono yangu?

35Ni nani kati ya miungu ya inchi hizi aliyeokoa inchi zao toka katika mikono yangu. Yawe ataweza kuukoa Yerusalema?’ ”

36Lakini watu walinyamaza, wala hawakumujibu neno kama vile walivyoamuriwa na mufalme akisema: “Musimujibu.”

37Kisha Eliakimu mwana wa Hilkia aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna aliyekuwa katibu, na Yoa mwana wa Asafu mwandishi, wakamwendea Hezekia wakiwa na nguo zenye kupasuliwa, wakamwelezea maneno ya yule jemadari.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help