1Hili ni neno la Yawe lilomufikia Mika, wa muji wa Moreseti wakati Yotamu, Ahazi na Hezekia walipokuwa wafalme wa Yuda. Mika aliona mambo yote haya juu ya Samaria na Yerusalema. Yawe anakuja kuhukumu
2Musikilize enyi watu wote;
sikiliza ewe dunia na vyote vinavyokuwa ndani yako.
Bwana wetu Yawe anakuja kuwashitaki,
Bwana wetu anasema kutoka hekalu lake takatifu.
3Kweli, anakuja kutoka makao yake;
atashuka na kutembea juu ya vilele vya dunia.
4Milima itayeyuka chini ya miguu yake,
kama inta karibu na moto;
mabonde yatapasuka,
kama vile maji yanayoporomoka kwenye muteremuko.
5Haya yote yatatukia
kwa sababu ya makosa ya wazao wa Yakobo,
kwa sababu ya zambi za wazao wa Israeli.
Kosa la Yakobo linaonekana wapi?
Katika muji wake mukubwa Samaria!
Kosa la Yuda linaonekana wapi?
Katika Yerusalema kwenyewe!
6Kwa hiyo, anasema hivi:
Muji wa Samaria nitaufanya kuwa mabomoko katika mbuga,
shamba ambalo watu watapanda mizabibu.
Mawe yaliyoujenga nitayatupa ndani ya bonde,
na misingi yake nitaichimbuachimbua.
7Sanamu zake zote zitavunjwavunjwa,
kila kitu kilichochumwa kitateketezwa kwa moto.
Nitaharibu sanamu za miungu yake yote.
Zililundikwa kutokana na mushahara wa ukahaba,
nazo zitatumiwa tena kuwa mushahara wa ukahaba.
8Kwa sababu hiyo, mimi nitalia na kuomboleza;
nitatembea uchi na bila viatu.
Nitaomboleza na kulia kama mbweha,
nitasikitika na kulia kama mbuni.
9Vidonda vya Samaria haviwezi kupona,
navyo vimeipata vilevile inchi ya Yuda;
vimefikia kwenye mulango wa Yerusalema,
pahali watu wangu wanapokaa.
10Musiitangaze habari hii kule Gati,
wala musilie machozi!
Kule Beti-Leafura mugaegae katika mavumbi kwa huzuni.
11Enyi wakaaji wa Safiri,
muende mukiwa uchi na wenye haya.
Wakaaji wa Zanana musitoke inje ya muji wenu.
Watu wa Beti-Ezeli wanalia;
musaada wao kwenu umeondolewa.
12Wakaaji wa Maroti wanangojea musaada kwa hamu kubwa,
lakini maangamizi yanakuja kutoka kwa Yawe
karibu kabisa na mulango wa Yerusalema.
13Enyi wakaaji wa Lakisi,
mufunge farasi wepesi na magari ya vita.
Ninyi mulikuwa mumeiga zambi ya watu wa Sayuni,
makosa ya Waisraeli yalikuwa kwenu.
14Hivyo, munapaswa kuwaacha wakaaji wa Moreseti-Gati.
Nao muji wa Akizibu hautawasaidia
wafalme wa Israeli kwa kitu chochote.
15Enyi wakaaji wa Maresa,
Mungu atawaletea tena adui atakayewateka.
Waongozi waheshimiwa wa Israeli
watakimbilia ndani ya pango kule Adulamu.
16Enyi watu wa Yuda, munyoe vichwa vyenu
kwa kuwaomboleza watoto wenu wapenzi;
mupanue upaa wenu ukuwe mupana kama wa tai,
maana watoto wenu watawaacha kwenda katika uhamisho.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.