1Sasa, Yobu, sikiliza masemi yangu;
sikiliza maneno yangu yote.
2Sikia! Ninafumbua kinywa changu.
Ulimi wangu utasema.
3Nitasema kadiri ya usawa wa moyo wangu;
ninayoyajua nitayasema kwa uaminifu.
4Roho ya Mungu iliniumba,
nayo pumzi ya Mungu Mwenye Uwezo inanipa uzima.
5Unijibu, kama unaweza.
Panga masemi yako vizuri mbele yangu,
ushike musimamo wako.
6Wewe na mimi ni sawa mbele ya Mungu;
mimi vilevile niliumbwa kwa sehemu ya udongo.
7Kwa hiyo hauna sababu ya kuniogopa;
maneno yangu mazito hayatakulemea.
8Kweli umesema, nami nikasikia;
nimesikia yote uliyosema.
9Wewe umesema hivi:
“Mimi niko safi, wala sina kosa.
Hakuna ubaya wowote katika moyo wangu.
10Mungu ananitafutia sababu,
ananiona kama adui yake.
11Ananifunga miguu kwa minyororo,
na kuchunguza hatua zangu zote.”
12Lakini Yobu, ninakuambia pale umekosa.
Mungu ni mukubwa kuliko mwanadamu.
13Kwa nini unashindana naye,
ukisema hatajibu ulizo lako moja?
14Mungu anaweza kusema kwa njia moja au ingine
lakini mutu hatambui.
15Mungu anaongea na watu katika ndoto na maono,
wakati usingizi muzito unapowapata,
16wanaposinzia katika vitanda vyao.
Halafu anawafungua watu masikio yao;
anawatia hofu kwa maonyo yake,
17wapate kuachana na matendo yao mabaya,
na kuvunja kiburi chao.
18Hivyo anamukinga mutu asiangamie katika shimo,
maisha yake yasiangamie kwa upanga.
19Mungu anamwazibu mutu kwa maumivu yanayomuweka katika kitanda,
maumivu yanashika viungo vyake bila kukoma;
20naye anapoteza hamu yote ya chakula,
hata chakula ni chukizo kwake.
21Mwili wake unakonda hata hawezi kutambuliwa,
na mifupa yake iliyofichama ikatokea inje.
22Yuko karibu sana kuingia ndani ya kaburi,
na maisha yake karibu na wale wanaoleta kifo.
23Lakini inawezekana kwamba malaika,
ambaye ni mupatanishi mumoja kati ya maelfu,
atakuwa karibu na mutu yule
kwa kumufunulia jambo la kufanya.
24Yule malaika anaweza kumwonea huruma na kumwomba Mungu:
“Umwokoe asiingie katika shimo;
nimepata ukombozi wake.”
25Mwili wake utaweza kuwa tena kama kijana,
ataweza kurudilia tena nguvu zake za ujana.
26Kisha atamwomba Mungu na kukubaliwa,
atakuja mbele yake kwa furaha,
na Mungu atamurudishia utukufu wake.
27Atashangilia mbele ya watu na kusema:
“Nilitenda zambi na kupotosha usawa,
nami sikuazibiwa kutokana na hayo.
28Mungu aliniokoa nisiangamie katika shimo;
nimebaki muzima na ninaona mwangaza.”
29Sikia! Mungu anamufanyia mwanadamu haya yote,
tena mara mbili, mara tatu.
30Anamwokoa mwanadamu asiangamie katika shimo,
aweze kuona mwangaza wa maisha.
31Sikia Yobu, unisikilize kwa uangalifu;
ukae kimya, nami nitasema.
32Kama una la kusema, unijibu;
sema, maana ninataka kukuona bila kosa.
33Kama sivyo, nyamaza unisikilize,
ukae kimya nami nikufundishe hekima.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.