Matayo 26 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Shauri la kuua Yesu(Mk 14.1-2; Lk 22.1-2; Yn 11.45-53)

1Yesu alipomaliza kusema maneno hayo yote, akawaambia wanafunzi wake:

2“Munajua kwamba kumebaki siku mbili mbele ya kutimia kwa sikukuu ya Pasaka, na Mwana wa Mutu apate kutolewa kusudi atundikwe juu ya musalaba.”

3Wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu wakakusanyika ndani ya nyumba ya Kuhani Mukubwa, aliyeitwa Kayafa,

4nao wakafanya shauri la kumukamata Yesu kwa werevu na kumwua.

5Lakini walijisemesha: “Tusimukamate kwa wakati wa karamu, kusudi fujo isitokee kati ya watu.”

Yesu anamimiwa marasi(Mk 14.3-9; Yn 12.1-8)

6Yesu alipokuwa Betania katika nyumba ya mutu aliyeitwa Simoni Mukoma,

7mwanamuke mumoja aliingia ndani ya nyumba, akiwa na chupa la jiwe lenye kuwa na marasi ya bei kali, akaimimia juu ya kichwa cha Yesu walipokuwa wakikula.

8Wanafunzi wake walipoona jambo lile, wakachukizwa na kusema: “Kwa nini kupoteza mali namna hii?

9Marasi hii ingeuzishwa kwa bei kali na kuwagawanyia wamasikini mali ile!”

10Lakini Yesu akatambua mawazo yao na kuwaambia: “Sababu gani munamusumbua mwanamuke huyu? Amenitendea jambo zuri.

11Kwa maana mutakuwa na wamasikini pamoja nanyi siku zote, lakini mimi sitakuwa pamoja nanyi siku zote.

12Mwanamuke huyu amemimia marasi hii juu ya mwili wangu kwa kuutayarisha kwa ajili ya maziko.

13Kweli ninawaambia: kwa ajili ya kukumbuka mwanamuke huyu, tendo lile alilofanya litaelezwa popote Habari Njema hii itakapohubiriwa katika dunia nzima.”

Yuda anakubali kumutoa Yesu(Mk 14.10-11; Lk 22.3-6)

14Halafu mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, aliyeitwa Yuda Iskariota, akaenda kwa wakubwa wa makuhani

15na kuwaambia: “Mutanipa nini kama nikimutoa Yesu kwenu?” Basi wakamupa vikoroti makumi tatu vya feza.

16Tangia wakati ule Yuda akaanza kutafuta wakati unaokuwa muzuri kwa kumutoa.

Yesu anakula Pasaka pamoja na wanafunzi wake(Mk 14.12-21; Lk 22.7-14,21-23; Yn 13.21-30)

17Siku ya kwanza ya karamu ya sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu, wanafunzi wakamwendea Yesu na kumwuliza: “Ni wapi unapotaka tukutayarishie karamu ya Pasaka?”

18Yesu akawaambia kwamba waende katika muji kwa mutu mumoja na kumwambia: “Mwalimu anasema: ‘Siku yangu inakaribia. Mimi na wanafunzi wangu tutakula karamu ya Pasaka kwako.’ ”

19Nao wanafunzi wakafanya sawa Yesu alivyowaagiza, wakatayarisha karamu ya Pasaka.

20Ilipokuwa magaribi, Yesu akaikaa kula chakula pamoja na wanafunzi wake kumi na wawili.

21Nao walipokuwa wakikula, akasema: “Kweli ninawaambia: mumoja kati yenu atanitoa.”

22Wanafunzi wakahuzunika sana na kuanza kumwuliza mumoja kwa mumoja: “Bwana, ni mimi?”

23Yesu akajibu: “Yule aliyechovya mukate pamoja nami ndani ya sahani ndiye atanitoa.

24Mwana wa Mutu atakufa sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema juu yake, lakini ole kwa mutu yule atakayemutoa! Ingekuwa heri kwake kama asingezaliwa!”

25Halafu Yuda, aliyemutoa, akamwuliza: “Mwalimu, ni mimi?”

Naye Yesu akamujibu: “Wewe umesema.”

Kusimikwa kwa karamu ya Bwana(Mk 14.22-26; Lk 22.15-20; 1 Kor 11.23-25)

26Walipokuwa wakikula, Yesu akatwaa mukate, akaubariki, kisha akaumega na kuwapa wanafunzi wake, akisema: “Mutwae na mukule, huu ni mwili wangu.”

27Kisha akatwaa kikombe, akakibariki na kuwapa, akisema: “Mukunywe ninyi wote,

28kwa maana hii ni damu yangu inayomwangika kwa ajili ya wengi kusudi wasamehewe zambi. Nayo damu hii inahakikisha agano la Mungu.

29Nami ninawaambia kwamba tangia sasa sitakunywa tena divai mpaka siku ile nitakapoikunywa mupya pamoja nanyi katika Ufalme wa Baba yangu.”

30Nao walipokwisha kuimba, wakaondoka kwenda kwa mulima wa Mizeituni.

Yesu anatabiri kwamba Petro atamukana(Mk 14.27-31; Lk 22.31-34; Yn 13.36-38)

31Halafu Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Usiku huu ninyi wote mutaanguka kwa ajili yangu, kwa maana imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: ‘Nitamwua muchungaji, na kondoo wa kundi watasambazwa.’

32Lakini nitakapokwisha kufufuka, nitawatangulia Galilaya.”

33Petro akamujibu: “Hata wote wakianguka, mimi sitaanguka hata kidogo.”

34Yesu akamujibu: “Kweli ninakuambia kwamba katika usiku huu, mbele jogoo hajawika utakuwa umenikana mara tatu.”

35Lakini Petro akamwambia: “Hata ikinipasa kufa pamoja nawe, sitakukana hata kidogo.”

Na wanafunzi wote wengine wakasema sawasawa naye.

36Kisha Yesu pamoja na wanafunzi wake wakafika katika bustani inayoitwa Getesemane. Na Yesu akawaambia: “Muikae hapa, kwa wakati ninapokwenda kuomba kule.”

Yesu anaomba katika Getesemane(Mk 14.32-42; Lk 22.39-46)

37Na akatwaa Petro na wana wawili wa Zebedayo na kwenda nao. Akaanza kuhuzunika na kuhangaika.

38Halafu akawaambia: “Ninahuzunika sana, karibu kufa! Mubakie hapa na mukeshe pamoja nami.”

39Kisha akajitenga mbali kidogo nao, akainama uso chini. Akaomba akisema: “Ee Baba yangu, kama ikiwezekana, ninakuomba uniondolee mbali kikombe hiki cha mateso. Lakini isikuwe kama vile mimi ninavyotaka, lakini kama vile wewe unavyotaka.”

40Kisha akarudi pahali pale alipowaacha wale wanafunzi, akawakuta wamelala usingizi. Akamwambia Petro: “Hamukuweza kukesha pamoja nami hata kwa saa moja tu?

41Mukeshe na muombe, kusudi musianguke katika majaribu; kwa maana roho ni hodari, lakini mwili ni zaifu.”

42Akawaacha tena kwa mara ya pili, akaomba akisema: “Ee Baba yangu, kama kikombe hiki cha mateso hakiwezi kupita mbali nami, bila mimi kukikunywa, basi mapenzi yako yafanyike!”

43Aliporudi tena, akawakuta wanafunzi wale wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa yamewezwa sana na usingizi.

44Yesu akawaacha tena, na kwenda kuomba kwa mara ya tatu, akirudilia maombi yale yale.

45Kisha akarudi kwenye wanafunzi wake na kuwaambia: “Mungali munalala na kupumzika? Angalia, saa imetimia, sasa Mwana wa Mutu anatolewa katika mikono ya wenye zambi.

46Musimame, tuende! Angalia, yule anayenitoa amefika karibu!”

Kukamatwa kwa Yesu(Mk 14.43-50; Lk 22.47-53; Yn 18.3-12)

47Yesu alipokuwa hajamaliza kusema, Yuda, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akafika pamoja na kundi kubwa la watu wenye panga na magongo. Hawa wote walikuwa wametumwa na wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu.

48Yuda, yule aliyekuwa amemutoa, aliwapa kitambulisho hiki: “Yule nitakayemubusu ndiye yeye, mumukamate.”

49Yuda alipofika, akamujongelea Yesu, na kumwambia: “Jambo, Mwalimu.” Na kisha akamubusu.

50Lakini Yesu akamwambia: “Rafiki, ufanye lililokuleta.”

Halafu watu wale wakajongea na kumukamata Yesu na kumufunga.

51Na mumoja wa wale waliokuwa pamoja na Yesu akachomoa upanga wake, akamupiga mutumishi wa Kuhani Mukubwa, akamukata sikio.

52Halafu Yesu akamwambia: “Rudisha upanga wako katika kifuko chake, kwa maana yeyote anayetumia upanga, atauawa kwa upanga.

53Haujui kwamba ninaweza kumwomba Baba yangu musaada na mara moja angenitumia zaidi ya makundi kumi na mawili ya wamalaika?

54Lakini namna gani yangetimia Maandiko Matakatifu yanayosema kwamba mambo haya yanapaswa kuwa hivi?”

55Kisha Yesu akawaambia watu wale: “Mumekuja na panga na magongo kwa kunikamata kama watu wanavyokwenda kumukamata munyanganyi? Siku zote niliikaa ndani ya hekalu, nikifundisha, nanyi hamukunikamata.

56Mambo haya yote yamefanyika kusudi maneno yanayosemwa na manabii katika Maandiko Matakatifu yapate kutimia.”

Basi wanafunzi wake wote wakamwacha na kukimbia.

Yesu mbele ya Baraza Kubwa(Mk 14.53-65; Lk 22.54-55,63-71; Yn 18.13-14,19-24)

57Wale waliomukamata Yesu wakamupeleka kwa Kuhani Mukubwa Kayafa, pahali walimu wa Sheria na wasimamizi wa watu walipokuwa wamekusanyika.

58Lakini Petro akamufuata Yesu kwa mbali, hata akaingia ndani ya upango wa Kuhani Mukubwa. Akaingia katika kiwanja, akaikaa pamoja na walinzi kusudi aone mambo yatakayotokea.

59Wakubwa wa makuhani na wakubwa wote wa Baraza Kubwa walitafuta mashitaki ya uongo juu ya Yesu, kusudi wapate kumwua.

60Lakini hawakupata neno, ijapokuwa watu wengi walikuja kumusingizia maneno ya uongo. Mwisho watu wawili wakafika

61na kusema: “Mutu huyu alisema kwamba anaweza kubomoa hekalu la Mungu na kulijenga tena kwa muda wa siku tatu.”

62Kuhani Mukubwa akasimama na kumwuliza Yesu: “Haujibu hata neno? Watu hawa wanakushitakia nini?”

63Lakini Yesu akanyamaza. Kuhani Mukubwa akamwambia: “Ninakuapisha kwa jina la Mungu Mwenye Uzima, utuambie kama wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu.”

64Yesu akamujibu: “Wewe umesema. Lakini zaidi ya hiyo, ninawaambia ninyi kwamba mutamwona Mwana wa Mutu akiikaa na mamlaka karibu na Mungu Mwenye Uwezo. Mutamwona vilevile akikuja katika mbingu katikati ya mawingu!”

65Halafu Kuhani Mukubwa akapasua nguo zake na kusema: “Mutu huyu amemutukana Mungu! Hatuhitaji tena ushuhuda wowote juu yake. Angalia, munatoka kusikia jinsi alivyomutukana Mungu.

66Munawaza nini?”

Nao wakajibu: “Anastahili kufa.”

67Halafu wamoja wakamutemea mate juu ya uso, na kumupiga ngumi. Na wengine wakamupiga makofi,

68wakisema: “Ewe Kristo, tambua ni nani aliyekupiga!”

69Wakati ule Petro alikuwa akiikaa inje katika kiwanja. Mutumishi mumoja mwanamuke akamufikia na kumwambia: “Wewe vilevile ulikuwa pamoja na Yesu wa Galilaya.”

Petro anamukana Yesu(Mk 14.66-72; Lk 22.56-62; Yn 18.15-18,25-27)

70Lakini akakana mbele ya wote waliokuwa pale, akisema: “Sijui maneno unayotaka kusema.”

71Petro alipotoka inje kwa mulango wa upango, mutumishi mwingine mwanamuke akamwona na kuwaambia wale waliokuwa pale: “Huyu alikuwa pamoja na Yesu wa Nazareti.”

72Lakini Petro akakana tena akaapa akisema: “Ninaapa ya kuwa simujui mutu huyu!”

73Nyuma kidogo, wale waliosimama pale, wakamufikia Petro na kumwambia: “Hakika wewe ni mumoja wao, kwa maana hata usemi wako unakutambulisha.”

74Halafu Petro akaanza kusema: “Nilaaniwe ikiwa ninasema uongo! Ninaapa kwamba simujui mutu huyu!” Na mara moja jogoo akawika,

75naye Petro akakumbuka maneno yale Yesu aliyomwambia kwamba mbele jogoo hajawika, atakuwa amemukana mara tatu. Basi akatoka inje, akalia kwa uchungu sana.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help