Mezali 28 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Waovu wanakimbia ijapokuwa hawafukuzwi na mutu, lakini wenye haki ni hodari kama simba.

2Taifa lenye fujo lina viongozi wengi, lakini kwa kiongozi mumoja mwenye akili na maarifa kuna utengemano.

3Mutu mwenye hitaji anayewatesa wamasikini, anafanana na mvua kubwa inayoharibu mimea.

4Watu wanaovunja sheria wanasifu waovu, lakini wanaoshika sheria wanapingana nao.

5Waovu hawaelewi haki ya sheria, lakini wanaomwogopa Yawe wanaielewa kabisa.

6Afazali masikini mwenye mwenendo mukamilifu, kuliko tajiri anayeishi kwa upotovu.

7Mutoto anayeshika sheria ni mwenye hekima, lakini rafiki wa walafi anafezehesha baba yake.

8Anayeongeza mali yake kwa mazidio na kulipisha faida, anamukusanyia mwingine mwenye kuwahurumia wamasikini.

9Anayekataa kuisikia sheria, yule, hata maombi yake, ni chukizo kwa Mungu.

10Anayepotosha mutu wa usawa katika njia mbaya, ataanguka katika shimo lake mwenyewe. Wakamilifu watarizi mazuri.

11Tajiri anajiona mwenyewe kuwa mwenye hekima, lakini masikini mwenye akili atamufichua.

12Watu wa haki wakipata madaraka, kuna utukufu mukubwa. Lakini waovu wakitawala, watu wanajificha.

13Anayeficha makosa yake hatafanikiwa, lakini anayeungama na kuyaacha atahurumiwa.

14Heri mutu anayemwogopa Yawe siku zote, lakini mwenye moyo mugumu atapata hasara.

15Mutawala mwovu anayetawala wamasikini ni kama simba anayenguruma au dubu anayeshambulia.

16Mutawala asiyekuwa na akili anawagandamiza sana watu, lakini anayechukia mali ya udanganyifu atatawala kwa muda murefu.

17Mutu anayelemewa na kosa ya kuua mutu, atakuwa mukimbizi mpaka katika kaburi. Mutu yeyote asijaribu kumusaidia.

18Mwenye mwenendo mukamilifu ataponyeshwa, lakini munafiki wa njia mbili ataanguka mara moja.

19Anayelima shamba lake atapata chakula kingi, lakini anayefuata mambo yasiyofaa atapata umasikini tele.

20Mutu mwaminifu atapata baraka tele, lakini mwenye pupa ya kuwa tajiri hataepuka azabu.

21Si vizuri kumubagua mutu. Watu wanafanya mabaya hata kwa ajili ya mukate.

22Mutu muchoyo anakimbilia mali, wala hajui kwamba ukosefu utamufikia.

23Anayemwonya mwenzake kwa mwisho atasifiwa naye, kuliko yule anayemubembeleza kwa maneno matamu.

24Anayeiba mali ya baba yake au ya mama yake na kusema si kosa, anatumika pamoja na yule anayeangamia.

25Muchoyo anachochea magomvi, lakini anayetegemea Yawe atafanikiwa.

26Anayetegemea akili yake mwenyewe ni mupumbafu; lakini anayeishi kwa hekima atakuwa salama.

27Anayesaidia wamasikini hatakosewa kitu, lakini anayekataa kuwaangalia atalaaniwa kwa wingi.

28Waovu wakitawala, watu wanajificha. Lakini wakiangamia, wenye haki wanaongezeka.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help