1 Wafalme 10 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Safari ya malkia wa Seba(2 Sik 9.1-12)

1Malkia wa Seba aliposikia sifa za Solomono, kwa sababu ya jina la Yawe, alimwendea Solomono kwa kumujaribu kwa maulizo magumu.

2Akafika Yerusalema akisindikizwa na watu wengi sana pamoja na ngamia waliobeba marasi, zawadi nyingi sana, zahabu na mawe ya bei kali.

3Naye Solomono akayajibu maulizo yote; hakuna hata ulizo moja lililomushinda.

4Malkia wa Seba alishangaa sana alipoiona hekima yote ya Solomono, na nyumba aliyokuwa ameijenga,

5tena alipoona chakula kilicholetwa kwa meza yake, jinsi wakubwa wake walivyoikaa kwenye meza, jinsi watumishi walivyotumika na walivyovaa, vilevile wenye kuleta vinywaji na sadaka za kuteketezwa ambazo alizitoa katika nyumba ya Yawe, alipumbazika na kushangaa sana.

6Basi, akamwambia mufalme: “Mambo yote niliyosikia katika inchi yangu juu ya kazi zako na hekima yako ni kweli!

7Lakini sikuweza kuamini habari hizo mpaka nilipofika na kujionea mwenyewe. Kumbe sikuambiwa hata nusu yake; hekima yako na fanaka zako vimepita habari nilizopewa.

8Heri kwa wake zako! Heri kwa hawa watumishi wako ambao wanakutumikia siku zote na kusikiliza hekima yako!

9Asifiwe Yawe, Mungu wako, ambaye amependezwa nawe, akakuweka juu ya kiti cha kifalme cha Israeli! Kwa sababu Yawe anapenda Israeli milele, amekuweka wewe ukuwe mufalme, kusudi uimarishe haki na sheria ya Mungu.”

10Kisha malkia akamupa mufalme zaidi ya kilo elfu ine za zahabu, marasi nyingi sana na mawe ya bei kali. Hakuna aliyeweza hata kidogo kumuletea mufalme Solomono marasi mengi sana sawa yale malkia wa Seba aliyomuletea.

11Tena, mashua za Hiramu zilizoleta zahabu kutoka Ofiri, zilileta kwa wingi miti ya musandali na mawe ya bei kali.

12Naye mufalme aliitumia miti hiyo ya musandali kwa ajili ya nguzo za nyumba ya Yawe, na za nyumba ya kifalme na vilevile kwa kutengeneza vinubi na vinanda vya waimbaji. Kiasi cha miti ya musandali kama hicho hakijaonekana tena mpaka leo.

13Mufalme Solomono naye alimupatia malkia wa Seba kila kitu alichotamani na alichotaka, pamoja na vitu vingine ambavyo Solomono alimupa kutokana na desturi yake ya kifalme. Basi malkia akarudi kwake pamoja na watumishi wake.

Utajiri wa mufalme Solomono(2 Sik 9.13-28)

14Kila mwaka, Solomono alipelekewa zahabu kilo elfu makumi mbili na mbili.

15Kiasi hicho si pamoja na zahabu aliyopata kwa wafanyabiashara na wachuuzi, kwa wafalme wote wa Arabia na watawala wa inchi ya Israeli.

16Mufalme Solomono alitengeneza ngao kubwa mia mbili kwa zahabu iliyofuliwa; kila ngao kilo saba za zahabu.

17Alitengeneza ngao ndogondogo mia tatu kwa zahabu iliyofuliwa; kilo moja na nusu ilitumiwa kwa kila ngao. Halafu mufalme akaziweka katika jengo lililoitwa Nyumba ya Pori ya Lebanoni.

18Vilevile mufalme alitengeneza kiti cha kifalme kikubwa cha pembe, akakipakaa zahabu safi kabisa.

19Kiti hicho kilikuwa na ngazi sita. Sehemu ya juu ilikuwa imeviringwa na kiliwekewa pahali pa kuegemeza mukono pande zake mbili; na sanamu za simba wawili wamesimama mumoja pembeni ya pahali pale pa kuegemeza mukono.

20Kulikuwa vilevile sanamu kumi na mbili za simba wamesimama, mumoja kwa mwisho wa kila ngazi. Kiti kama hicho kilikuwa bado hakijatengenezwa katika ufalme wowote.

21Vyombo vyote vya kunywa divai vya mufalme Solomono vilikuwa vya zahabu, na vyombo vyote vilivyokuwa katika Nyumba ya Pori ya Lebanoni vilikuwa vya zahabu safi; hakuna kilichotengenezwa kwa feza maana madini ya feza haikuhesabiwa kuwa kitu wakati ule.

22Kwa sababu mufalme Solomono alikuwa na mashua kubwa za Tarsisi zilizokuwa zikisafiri pamoja na mashua za Hiramu, kisha kila miaka mitatu mashua hizo za Tarsisi zilimuletea mufalme zahabu, feza, pembe, kima, na tausi.

23Mufalme Solomono aliwapita wafalme wote katika dunia kwa mali na hekima.

24Watu wa inchi zote walikuwa na hamu ya kumwendea Solomono kwa kusikiliza hekima yake ambayo Mungu alikuwa amemujalia.

25Kila mumoja wao alimuletea zawadi: vyombo vya feza, vya zahabu, nguo, manemane, manukato, farasi na nyumbu. Zawadi hizi alizipokea kila mwaka.

26Solomono alikusanya magari ya vita na waaskari wapanda-farasi. Alikuwa na magari ya vita elfu moja na mia ine na waaskari wapanda-farasi elfu kumi na mbili ambao aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya vita, na kule Yerusalema.

27Basi, Solomono alifanya feza katika Yerusalema kuwa kitu cha kawaida kama mawe, na mbao za mierezi zilikuwa nyingi kama mbao za mikuyu ya Shefela.

28Solomono aliagiza farasi kutoka Misri, na vilevile kutoka Kilikia ambako wachuuzi wake waliwanunua.

29Gari moja liliweza kununuliwa kule Misri kwa feza inayopita kilo saba, na farasi mumoja aliweza kununuliwa kwa feza kilo mbili. Wachuuzi wa mufalme walisafirisha magari na farasi hao na kuwauzishia wafalme wote wa Wahiti na wa Waaramu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help