1Siku moja Yeroboamu alikuwa akisimama pembeni ya mazabahu kusudi afukize ubani. Basi, mutu wa Mungu kutoka Yuda akafika pale Beteli na ujumbe wa Yawe.
2Mutu huyo akailaani ile mazabahu akisema: “Ee mazabahu, Yawe anasema hivi: ‘Kutazaliwa mutoto katika ukoo wa Daudi, jina lake Yosia. Huyo atawatwaa makuhani wanaotumika kwa nafasi ya ibada na kufukiza ubani juu yako, na kuwatambika juu yako. Hakika, mifupa ya watu itateketezwa juu yako!’ ”
3Mutu huyo akaonyesha kitambulisho siku ileile, akasema: “Hiki ndicho kitambulisho Yawe alichosema: ‘Mazabahu hii itabomoka, na majivu yanayokuwa juu yake yatamwangika.’ ”
4Mufalme Yeroboamu aliposikia maneno hayo ya mutu wa Mungu juu ya mazabahu kule Beteli, alinyoosha mukono akasema: “Mumukamate mutu yule!” Na mara moja ule mukono wake aliounyoosha, ukakauka, hakuweza tena kuukunja.
5Mazabahu nayo ikabomoka, na majivu yake yakamwangika chini, kama kitambulisho kile yule mutu wa Mungu alichokitoa na ujumbe wa Yawe.
6Basi, mufalme Yeroboamu akamwambia nabii: “Tafazali, umusihi Yawe, Mungu wako, uniombee mukono wangu upate kupona.”
Naye nabii akamwomba Yawe, na mukono wa mufalme ukapona, ukarudia kwa hali yake ya zamani.
7Halafu mufalme akamwambia mutu wa Mungu: “Karibu katika nyumba yangu kula chakula, nami nikupe zawadi.”
8Lakini mutu wa Mungu akamwambia: “Hata kama ukinipa nusu ya urizi wako, sitakwenda pamoja nawe. Sitakula wala kunywa maji pahali hapa,
9maana Yawe aliniamuru nisikule chakula au kunywa maji, wala nisirudi kwa njia ileile niliyoifuata kwa kuja hapa.”
10Basi, mutu yule akaenda zake, wala hakurudi kwa njia ile aliyoifuata kwa kuja Beteli.
Nabii muzee wa Beteli11Wakati ule, kulikuwa nabii mumoja muzee kule Beteli. Wana wake wakamwendea, wakamwelezea mambo yote yule mutu wa Mungu aliyotenda siku hiyo, kule Beteli. Wakamwambia vilevile yale maneno yule mutu aliyomwambia mufalme Yeroboamu.
12Baba yao akawauliza: “Amefuata njia gani?” Nao wakamwonyesha njia yule mutu wa Mungu aliyoifuata kutoka Yuda.
13Naye akawaambia watoto wake: “Munitayarishie yule punda.” Nao wakamutayarishia punda, na muzee akapanda juu yake.
14Akamufuata yule mutu wa Mungu, akamukuta akiikaa chini ya muti wa mwalo. Basi, akamwuliza: “Wewe ndiwe yule mutu wa Mungu kutoka Yuda?”
Naye akamujibu: “Ndiyo. Mimi ndiye.”
15Yule muzee akamwambia: “Karibu katika nyumba yangu, ukule chakula.”
16Lakini yeye akamwambia: “Siwezi kurudi pamoja nawe, wala kuingia katika nyumba yako. Siwezi kula chakula au kunywa maji pahali hapa,
17maana, Yawe aliniamuru nisikule chakula au kunywa maji pahali hapa, wala nisirudie kwa njia niliyokuja nayo.”
18Yule muzee wa Beteli akamwambia: “Mimi vilevile ni nabii kama wewe, na Yawe amesema nami kwa njia ya malaika akisema: ‘Umurudishe kwako, akule chakula na kunywa maji.’ ” Lakini yule nabii muzee alikuwa anamudanganya tu.
19Basi, mutu wa Mungu akarudi pamoja naye, akakula chakula na kunywa maji kwa huyo muzee.
20Walipokuwa kwa meza, neno la Yawe lilimufikia yule nabii muzee
21naye akamwambia kwa sauti yule mutu wa Mungu kutoka Yuda: “Yawe anasema hivi: ‘Wewe umeacha kutii ujumbe wa Yawe. Wewe haukufuata amri Yawe, Mungu wako, aliyokupa.
22Kwa pahali pake, umerudi hapa, ukakula chakula na kunywa maji pahali hapa ambapo uliambiwa usikule chakula wala kunywa maji. Basi, mwili wako hautazikwa kwenye kaburi la babu zako.’ ”
23Walipomaliza kula, yule nabii muzee akamutayarishia yule mutu wa Mungu punda, naye akaondoka.
24Alipokuwa anakwenda zake, simba akakutana naye katika njia, akamwua. Mwili wake ukatupwa pale katika barabara. Punda wake na yule simba wakasimama pembeni yake.
25Watu waliopitia pale na kuiona maiti katika barabara, na simba akisimama karibu nayo, wakaenda mpaka katika muji yule nabii alimokuwa anakaa, wakawaambia watu.
26Nabii yule ambaye alikuwa amemukaribisha kwake aliposikia habari hiyo, akasema: “Huyo ni yuleyule mutu wa Mungu aliyekataa kutii neno la Yawe! Yawe amemutuma simba, akamushambulia na kumwua kama alivyokuwa amemwambia.”
27Hapo akawaambia wana wake: “Munitayarishie punda.” Nao wakamutayarisha.
28Muzee akaenda, akaikuta maiti ya mutu wa Mungu katika barabara, simba na punda wake pembeni yake. Yule simba hakuikula maiti wala hakumushambulia punda.
29Basi, yule nabii muzee akaitwaa maiti ya mutu wa Mungu, akaiweka juu ya punda wake, akairudisha Beteli, kuomboleza kifo chake na kumuzika.
30Basi, akamuzika katika kaburi lake, naye pamoja na wana wake wakaomboleza kifo chake wakisema: “Aa! Ndugu yangu!”
31Nyuma ya mazishi, nabii huyo akawaambia wana wake: “Nikikufa, munizike katika kaburi hilihili alimozikwa mutu wa Mungu, mifupa yangu pembeni ya mifupa yake.
32Mambo yote aliyoagizwa na Yawe juu ya mazabahu ya Beteli, na nafasi yote ya kutambikia juu ya vilima vya Samaria, hakika yatatimia.”
33Yeroboamu hakuuacha upotovu wake; aliendelea kuchagua watu wa kawaida kuwa makuhani, watumike kwa nafasi ya kutambikia juu ya vilima. Mutu yeyote aliyejitolea, alimutakasa kuwa kuhani wa nafasi ya kutambikia kule juu ya vilima.
34Tendo hili likakuwa zambi ambayo ilisababisha ukoo wa Yeroboamu ufutiliwe mbali na kuangamizwa.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.