Matayo 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mufano wa mupandaji wa mbegu(Mk 4.1-9; Lk 8.4-8)

1Siku ile ile, Yesu akatoka ndani ya nyumba na kwenda kuikaa pembeni ya ziwa kwa kufundisha.

2Na kuona kundi kubwa la watu waliokusanyika karibu naye, akapanda ndani ya chombo na kukaa humo, nao watu walibaki wakisimama inchi kavu.

3Halafu akawafundisha mambo mengi akitumia mifano, akasema: “Mutu mumoja alikwenda kupanda mbegu.

4Alipokuwa akipanda mbegu katika shamba lake, zimoja zikaanguka pembeni ya njia, nao ndege wakakuja na kuzikula.

5Zingine zikaanguka pahali penye mawe, pasipokuwa udongo mwingi. Nazo zikaota upesi, kwa sababu hapakukuwa udongo mwingi.

6Wakati jua lilipokuwa kali, likazichoma, na kwa sababu hazikukuwa na mizizi mikubwa, zikakauka.

7Mbegu zingine zikaanguka katikati ya miiba. Ile miiba ikaota na kuzisonga.

8Lakini mbegu zingine zikaanguka katika udongo muzuri na kutoa matunda: zimoja zikazaa punje mia moja, zingine makumi sita na zingine makumi tatu.

9Basi mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!”

Kusudi la kutmia mifano(Mk 4.10-12; Lk 8.9-10)

10Wanafunzi wa Yesu wakamwendea na kumwuliza: “Kwa sababu gani unasema na watu hawa ukitumia mifano?”

11Akawajibu: “Ninyi mumefunuliwa kujua siri ya Ufalme wa mbinguni, lakini kwao si vile.

12Kwa maana mutu anayekuwa na kitu ataongezewa kingine, naye atakuwa na vitu vingi. Lakini mutu asiyekuwa na kitu, ataondolewa hata kile kidogo anachokuwa nacho.

13Ni kwa sababu hiyo ninasema nao kwa kutumia mifano: kwa kuwa wanaangalia, lakini hawaoni, nao wanasikiliza lakini hawasikii wala hawafahamu.

14Hivi yametimia kwao maneno haya yaliyosemwa na Mungu kwa njia ya nabii Isaya:

‘kusikia, mutasikia, lakini hamutafahamu;

kuangalia, mutaangalia, lakini hamutaona.

15Maana mioyo ya watu hawa imegeuka migumu,

wameziba masikio yao,

nao wamefunga macho yao,

kusudi wasipate kuona,

nao wasipate kusikia,

wala wasipate kunigeukia, nami ningewaponyesha.’

16“Lakini heri kwenu, kwa sababu macho yenu yanaona na masikio yenu yanasikia!

17Kweli ninawaambia: manabii wengi na wenye haki wengi walitamani kuona mambo munayoona, lakini hawakuyaona, na kusikia maneno munayosikia, lakini hawakuyasikia.

Yesu anaeleza mufano wa mupandaji(Mk 4.13-20; Lk 8.11-15)

18“Basi musikilize maana ya ule mufano wa mupandaji wa mbegu.

19Pahali zile mbegu zilipoanguka pembeni ya njia, ni mufano wa watu wanaosikia habari ya Ufalme na kukosa kuielewa. Na kisha yule mwovu Shetani anakuja na kuondoa mbegu zilizopandwa ndani ya mioyo yao.

20Udongo wenye mawe pahali mbegu zilipoanguka ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu, na mara moja wanalipokea kwa furaha.

21Lakini halizami ndani yao kama mizizi. Wanalishika kwa muda mufupi tu. Wakati taabu na mateso vinapowafikia kwa ajili ya Neno la Mungu, mara moja, wanaanguka.

22Pahali zile mbegu zilipoanguka katika miiba, ni mufano wa wale wanaosikia Neno la Mungu, lakini masumbuko ya dunia hii na udanganyifu wa mali vinasonga lile neno linalokuwa ndani yao na kulizuiza kuzaa matunda.

23Pahali zile mbegu zilipoanguka katika udongo muzuri ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu na kulielewa. Nao wanazaa matunda; wamoja matunda mia moja, wengine makumi sita na wengine makumi tatu.”

Mufano wa nyasi

24Yesu akawaambia mufano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mutu mumoja aliyepanda mbegu nzuri ya ngano katika shamba lake.

25Lakini siku moja usiku, wote walipokuwa wakilala usingizi, adui wa mutu yule akakuja na kupanda nyasi katikati ya ngano; kisha akajiendea.

26Ngano ilipoota na kutoa masuke, nyasi zikaonekana vilevile.

27Watumishi wa mwenye shamba wakamwendea na kumwuliza: ‘Ee Bwana, si ulipanda mbegu nzuri katika shamba lako? Basi nyasi hizi zimetoka wapi?’

28Naye akawajibu: ‘Ni adui aliyefanya vile.’ Basi watumishi wakamwuliza: ‘Unataka tuende kuongoa zile nyasi?’

29Lakini akajibu: ‘Hapana, mukiongoa nyasi, labda mutafikia kuongoa ngano pamoja nazo.

30Muviache vyote viwili vikomae pamoja mpaka wakati wa mavuno. Wakati ule nitawaambia wavunaji: muongoe kwanza nyasi, nanyi muzilundike kwa mafungu mafungu kwa kuzichoma, na kisha mukusanye ngano na kuweka mavuno ndani ya gala yangu.’ ”

Mufano wa mbego ndogo sana ya haradi(Mk 4.30-32; Lk 13.18-19)

31Yesu akawaambia mufano mwingine akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mbegu ya haradali mutu mumoja aliyoitwaa na kuipanda katika shamba lake.

32Mbegu hii ni ndogo sana kuliko mbegu zote, lakini inapokwisha kuota, inakuwa kubwa zaidi kuliko mimea yote, hata ndege wanakuja na kujenga chicha zao katikati ya matawi yake.”

Mufano wa chachu(Lk 13.20-21)

33Yesu akawaambia tena mufano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na chachu mwanamuke mumoja aliyoitwaa na kuichanga na vipimo vitatu vya unga kwa kuponda mikate hata yote ikapata kuvimba.”

Kusudi la Yesu la kutumia mifano(Mk 4.33-34)

34Yesu aliwaambia makundi ya watu maneno hayo yote akitumia mifano. Yeye hakusema nao pasipo kutumia mifano.

35Ilitokea vile kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii:

“Nitasema nao kwa mifano,

nitawaambia maneno yaliyofichwa tangu kuumbwa kwa dunia.”

Yesu anaeleza mufano wa nyasi

36Halafu Yesu akaagana na makundi ya watu na kurudi kwenye nyumba. Wanafunzi wake wakamwendea na kumwambia: “Utufasirie maana ya ule mufano wa nyasi katika shamba.”

37Naye akawajibu: “Yule anayepanda mbegu nzuri ni Mwana wa Mutu.

38Shamba ni dunia. Mbegu nzuri ni washiriki wa Ufalme. Nyasi ni washiriki wa yule Mwovu Shetani.

39Adui aliyepanda nyasi ni Shetani. Mavuno ni mwisho wa dunia, nao wavunaji ni wamalaika.

40Kama vile nyasi zinavyoongolewa kwa kuchomwa katika moto, ndivyo itakavyokuwa vilevile kwa mwisho wa dunia.

41Mwana wa Mutu atawatuma wamalaika wake, nao watakusanya toka katika Ufalme wake watu wote wanaowaangusha wengine katika zambi pamoja na wote wanaofanya maovu.

42Nao watawatupa ndani ya furu la moto, na mule watalia na kusaga meno.

43Lakini wenye haki watametameta kama jua katika Ufalme wa Baba yao. Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!”

Mufano wa mali iliyofichwa katika shamba

44“Ufalme wa mbinguni unafanana na mali iliyofichwa katika shamba moja. Mutu mumoja alipoiona, akaificha tena. Halafu kwa furaha kubwa akaenda kuuzisha vitu vyake vyote na kununua lile shamba.

Mufano wa ushanga wa bei kali

45“Ufalme wa mbinguni unafanana vilevile na muchuuzi mumoja aliyetafuta kununua ushanga muzuri.

46Alipoona ushanga mumoja muzuri sana, akaenda kuuzisha vitu vyake vyote na kuununua.

Mufano wa wavu

47“Ufalme wa mbinguni unafanana vilevile na wavuvi wamoja waliotupa wavu ndani ya ziwa, nao ukakusanya samaki wa kila namna.

48Wakati wavu ulipojaa, wavuvi wakaukokota inchi kavu. Halafu wakaikaa kwa kuchagua samaki: wakaweka samaki wazuri ndani ya vyombo na kutupa samaki wabaya.

49Ni hivi itakavyokuwa kwa mwisho wa dunia. Wamalaika watakuja na kuwatenga watu wabaya na watu wazuri.

50Na halafu watawatupa watu wabaya ndani ya furu la moto; na mule watalia na kusaga meno.”

Mufano wa vitu vipya na vya zamani

51Yesu akawauliza watu: “Mumeelewa maneno hayo yote?”

Nao wakamujibu: “Ndiyo.”

52Kisha akawaambia: “Basi, kila mwalimu wa Sheria aliyefundishwa katika Ufalme wa mbinguni, anafanana na mwenye nyumba anayetwaa vitu vipya na vitu vya zamani pamoja toka katika akiba yake.”

Watu wa Nazareti wanamukataa Yesu(Mk 6.1-6; Lk 4.16-30)

53Yesu alipomaliza kusema mifano hiyo, akaondoka kule

54na kwenda katika muji wake mwenyewe. Kule akaanza kuwafundisha watu katika nyumba zao za kuabudia, nao walishangaa na kuuliza: “Huyu amepata hekima na miujiza hii kutoka wapi?

55Huyu si mwana wa yule seremala? Mama yake si Maria? Nao Yakobo, Yosefu, Simoni na Yuda si wandugu zake?

56Na wadada zake, si wanaishi hapa kati yetu? Basi amepata mambo haya yote kutoka wapi?”

57Na kwa hiyo akakuwa kikwazo kwao.

Lakini Yesu akawaambia: “Nabii hakosewi heshima fasi zote, isipokuwa tu katika muji wake na katika jamaa yake.”

58Na hivi kwa sababu ya kutokuamini kwa watu hao, Yesu hakufanya miujiza mingi kule.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help