Isaya 53 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Ni nani aliyeamini mambo tuliyoyasikia?

Mukono wa Mungu umefunuliwa kwa ajili ya nani?

2Maana, mbele ya Yawe,

mutumishi wake alikomaa kama kichipukizi,

kama muzizi katika inchi kavu.

Hakukuwa na umbo wala sura ya kupendeza,

wala hakukuwa na uzuri wowote wa kutuvuta.

3Alizarauliwa na kukataliwa na watu.

Alikuwa mutu wa uchungu na huzuni.

Alikuwa kama mutu wa kuchukiza kwa watu;

alizarauliwa na tukamwona si kitu.

4Hata hivyo alitwaa mateso yetu,

na kubeba huzuni zetu.

Sisi tulifikiri amepata azabu,

amepigwa na Mungu na kuteswa.

5Lakini aliumizwa kwa sababu ya zambi zetu,

alipondwa kwa sababu ya maovu yetu.

Kwa kuazibiwa kwake sisi tumepata uzima;

kwa kupigwa kwake sisi tumepona.

6Sisi wote tumepotea kama kondoo,

kila mumoja wetu ameelekea njia yake.

Lakini Yawe alimubebesha azabu,

ambayo sisi wenyewe tuliistahili.

7Alionewa na kuteswa,

lakini alivumilia kwa unyenyekevu,

bila kutoa sauti hata kidogo.

Alikuwa kama mwana-kondoo anayepelekwa kwenda kuchinjwa,

kama kondoo anavyokaa kimya anapokatwa manyoya.

Hakutoa sauti hata kidogo.

8Alikamatwa kwa kinguvu, akahukumiwa na kupelekwa kuuawa;

na hakuna mutu aliyejali mambo yanayomupata.

Alifukuzwa kutoka inchi ya wanaokuwa wazima,

kwa sababu ya makosa ya watu wangu.

9Walimuzika pamoja na waovu;

katika kifo aliwekwa pamoja na watajiri,

ingawa hakutesa watu hata kidogo,

wala hakusema neno lolote la udanganyifu.

10Yawe alipenda kumuponda kwa mateso.

Alitoa uzima wake kwa ajili ya kuondoa zambi.

Mutumishi wa Mungu atakuwa na wazao;

ataishi maisha marefu.

Yeye ndiye atakayetimiza mupango wa Yawe.

11Mungu anasema:

Kisha kutaabika sana,

mutumishi wangu atafurahi.

Kwa njia ya kujulikana kwa huyo mutumishi wangu wa haki,

atawafanya wengi wakuwe wenye haki,

naye atazibeba zambi zao.

12Kwa hiyo nitamugawanyia sehemu pamoja na wakubwa,

atagawanya vitu vilivyotekwa pamoja na wenye nguvu.

Alijitoa yeye mwenyewe hata kufa;

aliwekwa kundi moja na watu wakosaji.

Alizibeba zambi za watu wengi,

akawaombea musamaha hao wakosaji.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help