Waamuzi 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Debora na Baraka

1Nyuma ya kifo cha Ehudu, Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Yawe.

2Yawe akawatia katika mikono ya mufalme wa Kanana, jina lake Asikie, ambaye aliishi Hazori. Jemadari wa waaskari wake aliitwa Sisera, mukaaji wa Haroseti-Hagoimu.

3Mufalme Asikie alikuwa na magari ya vita mia tisa ya chuma. Aliwagandamiza sana Waisraeli kwa miaka makumi mbili; nao wakamulilia Yawe awasaidie.

4Wakati ule, kulikuwa nabii mumoja mwanamuke aliyeitwa Debora, muke wa Lapidoti, aliyekuwa mwamuzi wa Waisraeli wakati ule.

5Debora alikuwa anazoea kuikaa chini ya muti wa ngazi uliokuwa kati ya muji wa Rama na muji wa Beteli katika inchi ya milima ya Efuraimu. Watu wa Israeli walimufikia kusudi awaamulie mashauri yao.

6Siku moja akamwita Baraka mwana wa Abinoamu wa Kedesi katika inchi ya Nafutali. Alipokuja akamwambia: “Yawe, Mungu wa Israeli, anakuamuru hivi: ‘Kwenda ukusanye watu wako kwenye mulima Tabori, uchague watu elfu kumi kutoka makabila ya Nafutali na Zebuluni.

7Mimi nitamuchochea Sisera, jemadari wa waaskari wa mufalme Asikie, akuje na waaskari na magari yake kupigana nawe kwenye muto Kisoni, na kumutia katika mikono yako.’ ”

8Baraka akamwambia Debora: “Kama utakwenda pamoja nami, nitakwenda. Lakini usipokwenda pamoja nami, sitakwenda.”

9Debora akamujibu: “Sawa. Nitakwenda pamoja nawe; lakini hautapata heshima yoyote ya ushindi, maana Yawe, atamutia Sisera katika mikono ya mwanamuke.”

Basi, Debora akafuatana na Baraka kwenda Kedesi.

10Baraka akayaita makabila ya Nafutali na Zebuluni kule Kedesi. Watu elfu kumi wakamufuata. Debora akaenda pamoja naye.

11Wakati ule, Mukeni mumoja aliyeitwa Heberi alikuwa amejitenga na Wakeni wenzake ambao ni wazao wa Hobabu, baba mukwe wa Musa. Alikuwa amepiga hema lake mbali kule kwenye muti wa mwalo wa Sananimu, karibu na Kedesi.

12Sisera alipopata habari kwamba Baraka mwana wa Abinoamu amekwenda kwenye mulima Tabori,

13akakusanya waaskari wake wote na magari yake mia tisa ya chuma, akaondoka Haroseti-Hagoimu, akaenda kwenye muto Kisoni.

14Debora akamwambia Baraka: “Simama! Leo ni siku ambayo Yawe atamutia Sisera katika mikono yako. Yawe anakwenda mbele yako.” Basi, Baraka akashuka kutoka kwenye mulima Tabori akiwaongoza watu wake elfu kumi.

15Baraka akafanya mashambulizi, naye Yawe akamukimbiza Sisera na waaskari wake wote mbele ya Baraka kwa upanga. Sisera akatoka katika gari lake, akakimbia kwa miguu.

16Baraka akawafuatilia waaskari wale na magari mpaka Haroseti-Hagoimu na kuwaua waaskari wote wa Sisera kwa mapanga. Hakukubaki hata mutu mumoja.

17Lakini Sisera akakimbia kwa miguu mpaka katika hema ya Yaeli, muke wa Heberi Mukeni. Alifanya hivyo kwa sababu kulikuwa amani kati ya mufalme Asikie wa Hazori na jamaa ya Heberi.

18Yaeli akaenda kumupokea Sisera, akamwambia: “Bwana wangu, karibu kwangu, wala usiogope.” Akaingia ndani ya hema yake. Yaeli akamufunika kwa blanketi.

19Sisera akamwambia Yaeli: “Tafazali, unipe maji kidogo nikunywe, maana nina kiu.” Akamupa maziwa pahali pa maji, kisha akamufunika tena.

20Sisera akamwambia: “Simama kwenye mulango wa hema. Mutu yeyote akikuja kukuuliza kama kuna mutu yeyote hapa, umwambie hakuna.”

21Lakini Yaeli, muke wa Heberi, akatwaa musumari wa kufungia hema na nyundo, akamwendea polepole akaupigilia ule musumari wa kufungia hema katika paji la uso wake ukapenya mpaka katika udongo, kwa maana alikuwa amelala usingizi muzito sababu ya muchoko. Basi, Sisera akakufa palepale.

22Naye Baraka alipokuwa anamufuatilia Sisera, Yaeli akatoka inje kwa kumupokea akamwambia: “Ukuje nami nitakuonyesha yule unayemutafuta.” Baraka akaingia ndani ya hema la Yaeli na kumukuta Sisera chini, amekufa, na musumari wa hema ndani ya paji lake.

23Hivyo, siku hiyo Mungu akawapa Waisraeli ushindi juu ya mufalme Asikie wa Kanana.

24Waisraeli wakaendelea kumufuatilia Asikie, mufalme wa Kanana, mpaka walipomwangamiza.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help