1Basi, Yosefu akakwenda kwa mufalme wa Misri, akamwambia: “Baba yangu na wandugu zangu pamoja na kondoo, ngombe na mali yao yote, wamefika kutoka inchi ya Kanana. Sasa wako katika eneo la Goseni.”
2Yosefu alikuwa amewatwaa wandugu zake watano, akawajulisha kwa mufalme.
3Mufalme akawauliza: “Kazi yenu ni nini?”
Wakamujibu: “Bwana, sisi watumishi wako ni wachungaji, kama vile babu zetu walivyokuwa.”
4Kisha wakamwambia mufalme: “Sisi watumishi wako tumekuja kukaa kama wageni katika inchi kwa sababu njaa ni kali kule Kanana na hakuna tena malisho kwa nyama wetu. Hivyo, bwana, tunakuomba, sisi watumishi wako, uturuhusu kukaa katika eneo la Goseni.”
5Mufalme akamwambia Yosefu: “Baba yako na wandugu zako wamekufikia wewe.
6Inchi yote ya Misri iko chini yako; uwape baba yako na wandugu zako sehemu bora ya inchi hii. Uwaache wakae katika eneo la Goseni. Na ikiwa unawafahamu watu mashujaa kati yao, uwachague wakuwe waangalizi wa nyama wangu.”
7Kisha, Yosefu akamuleta baba yake Yakobo kumwamukia mufalme. Naye Yakobo akamupa mufalme baraka zake.
8Mufalme akamwuliza Yakobo: “Umri wako ni miaka mingapi?”
9Yakobo akamujibu: “Umri niliojaliwa kama musafiri ni miaka mia moja na makumi tatu. Miaka hiyo imekuwa michache na iliyojaa mateso, tena haijafikia hesabu ya miaka wazee wangu waliyoishi kama wasafiri.”
10Kisha Yakobo akamubariki mufalme, akaondoka.
11Basi, Yosefu akawapa baba yake na wandugu zake eneo la Ramesesi lililokuwa bora kabisa katika inchi ya Misri, likuwe makao yao, nao wakalirizi kama vile mufalme alivyoagiza.
12Yosefu akakuwa anawapatia baba yake, wandugu zake na jamaa yote ya baba yake chakula kulingana na hesabu ya watu waliowategemea.
Usimamizi wa Yosefu13Nyuma chakula kikakosekana kabisa katika inchi yote. Njaa ilikuwa kali sana hata ikawafanya watu wote katika inchi ya Misri na ya Kanana kukonda.
14Yosefu akakusanya feza yote ya inchi ya Misri na Kanana kutokana na ngano waliyonunua, akapeleka feza hiyo kwa nyumba ya mufalme.
15Nyuma ya watu wote wa inchi ya Misri na Kanana kutumia feza yao yote, Wamisri wote walimufikia Yosefu na kumwambia: “Utupatie chakula! Kwa nini tukufe mbele ya macho yako? Angalia, sasa feza yetu imekwisha!”
16Yosefu akawaambia: “Kama feza yenu imekwisha, basi munipe nyama wenu, nami nitawapa ngano.”
17Halafu wakamuletea Yosefu nyama wao: farasi, ngombe, kondoo, mbuzi na punda, naye akawapa chakula. Mwaka ule Yosefu akakuwa anawapa chakula kwa kubadilishana na nyama wao wote.
18Mwaka uliofuata wakamufikia tena na kumwambia: “Bwana, ukweli ni kwamba feza yetu yote imekwisha na nyama wetu wamekuwa mali yako. Sasa, bwana, sisi watumishi wako hatuna chochote tunachoweza kukupa isipokuwa miili yetu na mashamba yetu.
19Kwa nini sisi tukufe mbele ya macho yako na mashamba yetu yaharibike? Utununue sisi pamoja na mashamba yetu, tukuwe watumwa wa mufalme kusudi tupate chakula. Utupatie ngano tusikufe. Utupatie mbegu kwa ajili ya mashamba yetu.”
20Hivyo Yosefu akainunua inchi yote ya Misri ikuwe mali ya mufalme. Kila Mumisri aliuzisha shamba lake, kwa jinsi njaa ilivyokuwa kali. Inchi yote ikakuwa mali ya mufalme wa Misri,
21na Yosefu akawafanya watu kuwa watumwa, kutoka pembe moja mpaka pembe ingine ya inchi ya Misri.
22Udongo ambao Yosefu hakununua ni ule iliokuwa wa makuhani. Hao hawakulazimika kuuzisha udongo wao maana waliishi kwa posho waliyopewa na mufalme.
23Kisha Yosefu akawaambia watu: “Muangalie, nimekwisha kuwanunua ninyi wote na mashamba yenu kuwa mali ya mufalme. Mutapewa mbegu nanyi mutapanda mashamba yenu.
24Wakati wa mavuno, sehemu moja ya tano mutamupa mufalme. Sehemu ine zitakazobaki zitakuwa mbegu na chakula kwa ajili yenu na jamaa zenu na watoto wenu.”
25Wakamujibu: “Bwana, umeyaokoa maisha yetu! Kwa vile umetuonyesha wema wako, sisi tutakuwa watumwa wa mufalme.”
26Ndivyo Yosefu alivyotangaza sheria moja ambayo iko mpaka leo katika inchi ya Misri. Kila mwanainchi anapaswa kutoa sehemu moja ya tano ya mavuno yake kwa mufalme. Udongo wa makuhani tu ndio haukununuliwa na kufanywa mali ya mufalme.
Maagizo ya Yakobo juu ya kufa kwake27Basi, watu wa Israeli wakakaa katika eneo la Goseni katika inchi ya Misri. Wakiwa kule, wakapata mali nyingi, wakazaa na kuongezeka sana.
28Yakobo alikaa katika inchi ya Misri kwa muda wa miaka kumi na saba, mpaka alipofikia umri wa miaka mia moja makumi ine na saba.
29Wakati wa kufa kwake ulipokaribia, Yakobo akamwita mwana wake Yosefu, akamwambia: “Sasa, kama nimepata kukubaliwa mbele yako, weka mukono wako chini ya mapaja yangu, uniahidi kwamba utanitendea kwa wema na uaminifu. Usinizike huku Misri,
30lakini unilalishe pamoja na babu zangu. Unitwae kutoka Misri na kunizika katika makaburi yao.”
Yosefu akamujibu: “Nitafanya kama ulivyosema.”
31Yakobo akamwambia: “Uniapie!” Yosefu akamwapia. Kisha Israeli akainamia upande wa kichwa cha kitanda chake.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.