1 Samweli 15 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Vita na Waamaleki

1Samweli alimwambia Saulo: “Yawe alinituma kukupakaa mafuta kwa kukusimika kuwa mufalme wa watu wake Waisraeli. Sasa sikiliza maneno ya Yawe.

2Yawe wa majeshi anasema hivi: ‘Nitawaazibu Waamaleki kwa ajili ya mambo waliyowatendea Waisraeli: wao waliwafungia njia walipokuwa wanatoka Misri.

3Sasa, uende kushambulia na kuangamiza vitu vyote wanavyokuwa navyo. Usiwaache wazima, lakini uwaue wote: wanaume kwa wanawake, watoto wachanga na wenye kunyonya, ngombe, kondoo, ngamia na punda.’ ”

4Saulo akaita waaskari wake, akawahesabu kule Telaimu. Kulikuwa waaskari wa miguu elfu mia mbili kutoka katika inchi ya Israeli na elfu kumi kutoka inchi ya Yuda.

5Halafu yeye na watu wake wakaenda kwenye muji wa Amaleki, wakajificha wakivizia katika bonde.

6Saulo akawaambia Wakeni: “Muende! Muondoke! Mutoke kati ya Waamaleki, kama sivyo, nitawaangamiza pamoja nao. Muondoke kwa sababu ninyi muliwatendea mema Waisraeli walipotoka Misri.” Basi, Wakeni wakaondoka kati ya Waamaleki.

7Saulo aliwashinda Waamaleki kuanzia Havila mpaka Suri, kwa upande wa mashariki wa Misri.

8Alimukamata mateka mufalme Agagi wa Waamaleki akiwa angali muzima. Akawaua watu kwa makali ya upanga.

9Lakini Saulo na watu wake hawakumwua Agagi, kondoo bora kabisa, ngombe wazuri, wana-ngombe, wana-kondoo na chochote kile kilichokuwa kizuri hawakukiangamiza. Lakini vitu vyote vibaya na visivyokuwa vya bei kali waliviangamiza.

10Neno la Yawe lilimufikia Samweli kusema hivi:

11“Ninajuta kwamba nimemufanya Saulo kuwa mufalme. Yeye ameacha kunifuata mimi na hajatimiza amri zangu.” Samweli alikasirika, akamulilia Yawe usiku kucha.

12Samweli alisikia kwamba Saulo alikuwa amekwenda kule Karmeli na amesimamisha munara wa ukumbusho wake, na kwamba amekwenda Gilgali. Hivyo, kesho yake, Samweli aliamuka asubui mapema, akaenda kukutana na Saulo.

13Samweli alipomufikia Saulo, Saulo akamwambia Samweli: “Yawe akubariki! Nimetimiza amri ya Yawe.”

14Samweli akamwambia: “Mbona ninasikia mulio wa kondoo na ngombe?”

15Saulo akajibu: “Watu waliwaacha wazima kondoo na ngombe bora kabisa kwa kumutolea Yawe, Mungu wako, lakini wengine wote tumewaangamiza.”

16Samweli akamwambia Saulo: “Nyamaza! Nitakuambia jambo Yawe aliloniambia leo usiku.”

Saulo akasema: “Uniambie.”

17Samweli akamwambia: “Ingawa unajiona kwamba wewe ni mudogo, lakini si wewe kiongozi wa makabila ya Israeli? Yawe alikupakaa mafuta kwa kukusimika kuwa mufalme juu ya Israeli.

18Yawe alipokutuma alikuambia: ‘Kwenda uwaangamize kabisa wale Waamaleki wenye zambi, upigane nao mpaka umewaua wote!’

19Kwa nini basi, haukuitii sauti ya Yawe? Kwa nini mukakimbilia vitu kwa kuvinyanganya na hivyo kutenda jambo ovu mbele ya Yawe?”

20Saulo akajibu: “Nimetii sauti ya Yawe. Nilikwenda kule Yawe alikonituma; nimemuleta Agagi mufalme wa Waamaleki, na nimewaangamiza kabisa Waamaleki.

21Lakini watu walinyanganya vitu: kondoo, ngombe na vitu vyote bora vilivyolaaniwa kwa kumutolea Yawe, Mungu wako, kule Gilgali.”

22Halafu Samweli akamwambia:

“Unazani kwamba Yawe anapendelea zaidi

sadaka za kuteketezwa kwa moto na matoleo mengine,

kuliko kuitii sauti yake?

Hapana. Kumutii yeye ni bora kuliko matoleo

na kumusikiliza kuliko kumutolea mafuta ya beberu.

23Uasi ni sawa na zambi ya kuaguza,

na kiburi ni sawa na uovu wa kuabudu sanamu.

Kwa sababu umeikataa amri ya Yawe,

naye amekukataa kuwa mufalme.”

24Saulo akamwambia Samweli: “Nimetenda zambi. Nimeasi amri ya Yawe na amri yako, kwa sababu niliwaogopa watu, nikawatii wao.

25Lakini sasa ninakuomba, unisamehe zambi yangu. Uniruhusu nirudi pamoja nawe kusudi niweze kumwabudu Yawe.”

26Samweli akamujibu: “Siwezi hata kidogo kurudi pamoja nawe. Wewe umeikataa amri ya Yawe, naye amekukataa kuwa mufalme juu ya Israeli.”

27Samweli alipogeuka kusudi aende zake, Saulo akashika pindo la nguo yake, nayo ikapasuka.

28Halafu Samweli akamwambia Saulo: “Tangu leo Yawe ameurarua ufalme wa Israeli kutoka kwako na atamupa mutu mwingine kati ya wajirani zako anayekuwa bora kuliko wewe.

29Na Mungu ambaye ni utukufu wa Israeli hadanganyi, wala habadilishi wazo lake. Yeye si mwanadamu hata apate kubadilisha mawazo.”

30Saulo akajibu: “Nimefanya zambi. Hata hivyo, uniheshimishe sasa mbele ya wazee wa watu wangu na Waisraeli. Uniruhusu nirudi pamoja nawe kusudi nimwabudu Yawe, Mungu wako.”

31Basi, Samweli akarudi pamoja naye mpaka Gilgali na Saulo akamwabudu Yawe.

32Kisha Samweli akasema: “Muniletee hapa Agagi mufalme wa Waamaleki.” Agagi akamwendea Samweli akiwa mwenye furaha maana alifikiri: “Uchungu wa kifo umepita.”

33Samweli akasema: “Kwa sababu upanga wako umewafanya wamama wengi wasikuwe na watoto, ndivyo na mama yako atakavyokuwa bila mutoto kati ya wamama.” Akamukatakata Agagi vipandevipande mbele ya Yawe kule Gilgali.

34Kisha, Samweli akaenda Rama; na mufalme Saulo akarudi kwenye nyumba yake kule Gibea.

35Tangu siku ile, Samweli hakumwona tena Saulo, mpaka siku alipokufa. Hata hivyo Samweli alimulilia Saulo. Naye Yawe alisikitika kwamba alikuwa amemusimika Saulo kuwa mufalme juu ya inchi ya Israeli.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help