2 Samweli 18 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Abusaloma anashindwa na kuuawa

1Daudi aliwahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akawagawanya katika vikundi vya maelfu chini ya majemadari wao na kuweka wakubwa kwa kuwaongoza; na vikundi vya mamia, navyo vikiongozwa na wakubwa wao.

2Daudi akatuma waaskari wake kwa vita katika vikundi vitatu: sehemu moja ya tatu ikiwa chini ya uongozi wa Yoabu, sehemu ingine ya tatu chini ya uongozi wa Abisayi mwana wa Zeruya, ndugu ya Yoabu; na sehemu ingine ya tatu chini ya uongozi wa Itayi wa muji wa Gati. Kisha mufalme Daudi akawaambia wote: “Mimi mwenyewe vilevile nitakwenda pamoja nanyi.”

3Lakini watu wakamwambia: “Hautakwenda. Maana, ikiwa tutakimbia, hawatajali kitu juu yetu. Ikiwa nusu yetu watakufa, hawatahangaika nasi vilevile. Lakini wewe ni wa lazima kuliko watu elfu kumi kati yetu. Kwa hiyo inafaa wewe ubaki katika muji na kutupelekea musaada ukiwa katika muji.”

4Mufalme akawaambia: “Nitafanya sawa vile munavyoona kuwa vizuri.” Kwa hiyo, mufalme akasimama pembeni ya mulango, nao waaskari wake wakipita: mamia na maelfu.

5Mufalme akawaamuru Yoabu, Abisayi na Itayi: “Kwa ajili yangu, mumutendee yule kijana Abusaloma kwa upole.” Watu wote walimusikia mufalme alipoamuru wakubwa wake juu ya Abusaloma.

6Kwa hiyo, waaskari wa Daudi wakaenda katika mbuga kwa kupigana na watu wa Israeli. Mapigano hayo yalifanyika katika pori la Efuraimu.

7Watumishi wa Daudi waliwashinda watu wa Israeli. Mauaji ya siku hiyo yalikuwa makubwa maana watu elfu makumi mbili waliuawa.

8Mapigano hayo yalienea katika inchi yote na watu wengi walikufa katika pori kuliko wale waliouawa kwa upanga katika vita.

9Kisha Abusaloma, akiwa amepanda juu ya nyumbu, alikutana na watumishi wa Daudi. Nyumbu huyo alipokuwa anapita chini ya tawi kubwa la muti wa mwalo, halafu kichwa cha Abusaloma kikakwama kwenye muti wa mwalo. Abusaloma akaachwa akilembelea katika hewa. Lakini nyumbu wake akaendelea mbele.

10Mutu mumoja aliyeona tukio hilo, akamwambia Yoabu: “Nimemwona Abusaloma akilembelea kwenye muti wa mwalo.”

11Yoabu akamwambia mutu yule: “Nini? Ulimwona Abusaloma? Kwa nini, basi, haukumupiga na kumwua palepale? Ningefurahi kukulipa vikoroti kumi vya feza na mukaba.”

12Lakini yule mutu akamwambia Yoabu: “Hata kama ningeuona uzito wa vikoroti elfu moja vya feza katika mukono wangu, singeunyoosha mukono wangu juu ya mwana wa mufalme kwa kumwua. Maana, tulimusikia mufalme alipokuamuru wewe Abisayi na Itayi, kwamba kwa ajili yake, mumulinde kijana Abusaloma.

13Kwa upande mwingine, kama ningemutendea kwa udanganyifu, hakuna lolote linalofichwa kwa mufalme. Wewe mwenyewe haungalinitetea.”

14Yoabu akamwambia: “Mimi sina wakati wa kupoteza pamoja nawe.”

Yoabu akatwaa mikuki midogo mitatu katika mukono wake, akaenda na kumuchoma Abusaloma ndani ya moyo, Abusaloma akiwa angali muzima kwenye tawi la muti wa mwalo.

15Kisha, vijana kumi waliomubebea Yoabu silaha, wakakuja kumuzunguka Abusaloma, wakamupiga na kumwua.

16Halafu Yoabu akapiga baragumu na waaskari wote wakaacha kuwafuatilia watu wa Israeli, maana Yoabu aliwakataza.

17Wakamukamata Abusaloma, wakamutupia ndani ya shimo kubwa katika pori na kulundika lundo kubwa sana la mawe juu yake. Watu wote wa Israeli wakakimbia, kila mumoja kwake.

18Abusaloma, alipokuwa angali anaishi, alikuwa amejijengea na kujisimikia nguzo inayokuwa kwenye Bonde la Mufalme, maana alisema: “Mimi sina mutoto mwanaume wa kudumisha jina langu kusudi nikumbukwe.” Nguzo hiyo aliipa jina lake, na inaitwa “Nguzo ya Abusaloma” mpaka leo.

Daudi anapashwa habari juu ya kifo cha Abusaloma

19Kisha, Ahimasi mwana wa Zadoki, akasema: “Uniruhusu nikimbie kumupelekea mufalme habari hizi kwamba Yawe amemukomboa toka katika nguvu za waadui zake.”

20Yoabu akamwambia: “Leo, hautapeleka habari hiyo. Unaweza kupeleka habari hizo siku nyingine. Lakini leo hautapeleka habari zozote kwa sababu mwana wa mufalme amekufa.”

21Halafu Yoabu akamwambia mutu mumoja wa inchi ya Etiopia: “Wewe, uende umwelezee mufalme yale uliyoona.” Mwetiopia yule akainama kwa heshima mbele ya Yoabu, akaondoka mbio.

22Kisha Ahimasi mwana wa Zadoki akamwambia Yoabu tena: “Si kitu; uniruhusu na mimi nimukimbilie yule Mwetiopia!”

Yoabu akamwambia: “Mbona unataka kukimbia mwana wangu? Wewe hautapata zawadi yoyote kwa habari hizi!”

23Ahimasi akamwambia: “Si kitu; nitakimbia.”

Yoabu akamwambia: “Basi, kimbia.” Kisha Ahimasi akakimbia akifuata njia ya mbuga, akamutangulia yule Mwetiopia.

24Daudi alikuwa ameikaa kati ya milango miwili ya muji. Naye mulinzi wa mulango akapanda juu ya ukuta mpaka juu ya mulango na alipoinua macho yake aliona mutu akikimbia peke yake.

25Huyo mulinzi akasema kwa sauti, akamwambia mufalme. Mufalme akasema: “Kama yuko peke yake, ni kusema ana habari.” Yule mutu akazidi kukaribia.

26Mulinzi akamwona mutu mwingine akikimbia, akasema tena kwa sauti kwenye mulango: “Angalia, mutu mwingine akikimbia peke yake!”

Mufalme akasema: “Naye analeta habari.”

27Yule mulinzi akasema: “Ninaona kwamba yule anayekimbia zaidi ni Ahimasi mwana wa Zadoki.”

Mufalme akasema: “Huyo ni mutu muzuri, anatuletea habari njema.”

28Halafu Ahimasi akamwambia mufalme kwa sauti kubwa: “Mambo yote ni sawa.” Akainama mbele ya mufalme, kwa heshima na kusema: “Yawe atukuzwe, Mungu wako, ambaye amekukomboa kutoka watu walioinua mikono yao juu yako, bwana wangu mufalme.”

29Mufalme akamwambia: “Kijana Abusaloma ni muzima?” Ahimasi akasema: “Wakati Yoabu aliponituma mimi mutumishi wako, niliona kulikuwa kelele nyingi, lakini sikufahamu maana yake.”

30Mufalme akasema: “Kaa pembeni, na usimame pale.” Basi, Ahimasi akaenda pembeni na kusimama kimya.

31Halafu yule Mwetiopia akafika; naye akasema: “Kuna habari njema kwako bwana wangu mufalme! Maana Yawe leo hii amekukomboa kutoka nguvu za wale wote waliokushambulia.”

32Mufalme akamwuliza: “Kijana Abusaloma ni muzima?”

Mwetiopia akasema: “Waadui zako, bwana wangu mufalme, pamoja na wote wanaokushambulia wakikutakia mabaya, wakuwe kama huyo kijana Abusaloma.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help