1Zaburi ya Daudi.
Ee nafsi yangu, umusifu Yawe;
nafsi yangu yote isifu jina lake takatifu!
2Ee nafsi yangu, umusifu Yawe!
Usisahau hata kidogo matendo mazuri yake yote.
3Ananisamehe uovu wangu wote,
na kuniponyesha magonjwa yote.
4Ananiokoa kutoka kifo,
na kunijalia wema na rehema zake.
5Anajaza maisha yangu na raha,
hata ninabaki kijana mwenye nguvu kama tai.
6Yawe anahukumu kwa haki;
anawajalia wanaoteswa haki zao.
7Alimujulisha Musa njia zake,
aliwaonyesha watu wa Israeli matendo yake makubwa.
8Yawe ni mwenye rehema na huruma;
ni muvumilivu na mwingi wa wema.
9Hatukaripii siku zote,
wala hasira yake haidumu milele.
10Yeye hatuazibu kama tunavyostahili;
hatulipizi kadiri ya uovu wetu.
11Kama vile anga linavyokuwa juu mbali na dunia,
ndivyo kipimo cha wema wake kinavyokuwa kwa watu wanaomwabudu.
12Kama mashariki inavyokuwa mbali na magaribi,
ndivyo anavyotenga zambi zetu mbali nasi.
13Kama vile baba anavyohurumia mwana wake,
ndivyo Yawe anavyohurumia wote wanaomwabudu.
14Mungu anajua jinsi tulivyoumbwa;
anajua kwamba sisi ni mavumbi.
15Maisha ya mwanadamu ni kama majani tu,
yanachanua kama maua:
16upepo unapovuma juu yake yanatoweka,
na mahali yalipokuwa hapaonekani tena.
17Lakini wema wa Yawe unadumu milele,
kwa wale wote wanaomwabudu;
na haki yake inadumu vizazi vyote,
18kwa wote wanaoshika agano lake,
wanaokumbuka kutii amri zake.
19Yawe ameweka kiti chake cha kifalme mbinguni;
yeye anatawala juu ya vitu vyote.
20Mumusifu Yawe, enyi wamalaika wakubwa,
enyi munaotimiza amri zake na kutimiza neno lake!
21Mumusifu Yawe, enyi kundi lote la mbinguni,
enyi watumishi wake munaotimiza mapenzi yake!
22Mumusifu Yawe, enyi viumbe vyake vyote;
mumusifu popote munapokuwa katika utawala wake.
Ee nafsi yangu, umusifu Yawe!
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.