2 Mambo ya Siku 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Vita kati ya Abiya na Yeroboamu(1 Fal 15.1-8)

1Abiya akaanza kutawala inchi ya Yuda katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa mufalme Yeroboamu.

2Alitawala kwa muda wa miaka mitatu akiwa Yerusalema. Mama yake aliitwa Mikaya binti ya Urieli wa Gibea.

Kukatokea vita kati ya Abiya na Yeroboamu.

3Abiya alijitayarisha kupigana vita akiwa na jeshi la waaskari hodari elfu mia ine, naye Yeroboamu akajitayarisha na jeshi lake la waaskari hodari elfu mia nane.

4Mufalme Abiya akasimama juu ya mulima Zemaraimu, unaokuwa kati ya milima ya Efuraimu akamwambia Yeroboamu na Waisraeli: “Unisikilize, ewe Yeroboamu na Waisraeli wote!

5Hamujui kwamba Yawe, Mungu wa Israeli, amemupa Daudi na wazao wake ufalme kwa milele kwa kufanya naye agano lisilovunjika?

6Lakini Yeroboamu mwana wa Nebati mutumishi wa Solomono mwana wa Daudi alimwasi bwana wake.

7Na watu wa ovyoovyo wakajiunga naye, watu wapumbafu wasiofaa kitu, nao wakamushawishi Rehoboamu mwana wa Solomono kutenda yale waliyotaka wao, naye hangeweza kuwazuia maana wakati ule alikuwa angali kijana bila mazoezi mengi.

8“Sasa ninyi munazani munaweza kupinga ufalme wa Yawe ambao Daudi na wazao wake walipewa kwa sababu muko na jeshi kubwa na sanamu za zahabu za wana-ngombe, Yeroboamu alizowatengenezea kuwa miungu yenu!

9Hamukuwafukuza makuhani wa Yawe, wana wa Haruni, vilevile na Walawi, na kujifanyia makuhani wenu wenyewe kama vile watu wa mataifa mengine wanavyofanya? Yeyote anayekuja kwenu kujitakasa na mwana-ngombe dume au kondoo dume anakuwa kuhani wa vitu ambavyo si miungu.

10“Lakini kwa ngambo yetu, Yawe ni Mungu wetu, wala hatujamwacha. Tena tuko na makuhani wa uzao wa Haruni ambao wanamutumikia Yawe, nao wanasaidiwa na Walawi.

11Kila siku asubui na magaribi, makuhani wanamutolea sadaka za kuteketezwa na kumufukizia ubani wenye harufu nzuri, tena wanapanga mikate inayotolewa na Mungu juu ya meza ya zahabu safi, na kutunza kinara cha zahabu na kuwasha taa kila siku magaribi. Sisi tunayafuata maagizo ya Yawe, Mungu wetu, lakini ninyi mumemwacha.

12Na muangalie, Mungu mwenyewe ndiye kiongozi wetu na makuhani wake wako na baragumu zao tayari kuzipiga kwa kupana kitambulisho cha kuanza vita juu yenu. Enyi watu wa Israeli, muache kupigana vita na Yawe, Mungu wa babu zenu. Hamuwezi kushinda!”

13Lakini wakati ule, Yeroboamu alikuwa amekwisha kutuma waaskari wake wamoja kushambulia jeshi la Yuda kutoka upande wa nyuma, wakati wale wengine wamewashambulia kutoka upande wa mbele.

14Watu wa Yuda walipoangalia nyuma, walishituka kuona wamezungukwa; basi wakamulilia Yawe, nao makuhani wakapiga baragumu zao.

15Halafu waaskari wa Yuda wakapiga kelele la vita, na walipofanya hivyo, Mungu akamushinda Yeroboamu na jeshi lake la Waisraeli mbele ya Abiya na watu wa Yuda.

16Watu wa Israeli wakawakimbia Wayuda naye Mungu akawatia katika mikono yao.

17Abiya na jeshi lake akawapiga Waisraeli sana, akawashinda; akaua waaskari wa Israeli, elfu mia tano waliokuwa kati ya waaskari hodari sana katika Israeli.

18Kwa hiyo, watu wa Yuda walipata ushindi mbele ya Waisraeli kwa sababu walimutegemea Yawe, Mungu wa babu zao.

19Abiya akamufukuza Yeroboamu, akamunyanganya miji yake: Beteli, Yesana, Efuroni pamoja na vijiji vilivyokuwa kandokando ya miji hiyo.

20Yeroboamu hakuweza kupata nguvu tena wakati wa Abiya. Kwa mwisho Yawe akamupiga, naye akakufa.

21Lakini Abiya aliendelea kupata nguvu zaidi. Akaoa wanawake kumi na wane, akazaa wana makumi mbili na wawili na wabinti kumi na sita.

22Matendo mengine ya Abiya, njia zake na maneno yake, yameandikwa katika kitabu cha “Historia ya Nabii Ido.”

23Kwa mwisho, Abiya alikufa na kuzikwa katika muji wa Daudi na mwana wake Asa akatawala kwa pahali pake. Wakati wa Asa, kulikuwa amani katika inchi kwa muda wa miaka kumi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help