2 Mambo ya Siku 32 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Waasuria wanaleta woga Yerusalema(2 Fal 18.13-37; 19.14-19,35-37; Isa 36.1-22; 37.8-38)

1Nyuma ya matendo hayo ya uaminifu ya mufalme Hezekia, mufalme Saniharibu wa Asuria akashambulia inchi ya Yuda. Akakuja kupiga makambi kwenye miji yenye kuta akitumaini kwamba ataishinda ikuwe mali yake.

2Mufalme Hezekia alipoona kwamba mufalme Saniharibu amekuja kwa kusudi la kuishambulia Yerusalema,

3akaamua, yeye pamoja na wakubwa wake na wakubwa wa majeshi kufunga maji ya chemichemi zilizokuwa inje ya miji; nao wakamuunga mukono, wakamusaidia.

4Wakawakusanya watu wengi pamoja, wakazifunga chemichemi zote pamoja na kijito kilichopitia kati ya sehemu hiyo wakisema: “Kwa nini kuwaachia wafalme wa Asuria, wakikuja wakute maji tele?”

5Hezekia akajitia moyo, akajenga upya ukuta wote uliokuwa umebomoka, na juu yake akajenga minara. Upande wa inje, akajenga ukuta mwingine wa pili, na akaiimarisha uwanja wa Milo katika muji wa Daudi. Zaidi ya hayo akatengeneza silaha na ngao kwa wingi.

6Akaweka watu wote wa muji chini ya uongozi wa majemadari, kisha akawaamuru wakusanyike katika uwanja penye Mulango wa Muji. Hapo akawatia moyo akisema:

7“Muwe imara na hodari. Musiogope wala musifazaike mbele ya mufalme wa Asuria au majeshi yake maana tunayekuwa naye ni mukubwa kuliko anayekuwa na Saniharibu.

8Yeye ana nguvu za kibinadamu tu, lakini sisi tuna Yawe, Mungu wetu, kwa kutusaidia na kutupigania vita vyetu.” Maneno haya ya mufalme Hezekia yakawatia moyo sana watu wale.

9Nyuma ya hayo, Saniharibu mufalme wa Asuria, ambaye alikuwa angali anauzunguka muji wa Lakisi akiwa na majeshi yake yote, akawatuma watumishi wake Yerusalema kwa Hezekia mufalme wa Yuda na kwa watu wote wa inchi ya Yuda waliokuwa Yerusalema, akisema:

10“Hivi ndivyo Saniharibu mufalme wa Asuria anavyosema: Munategemea nini hata munakaa Yerusalema, muji ambao umezungukwa?

11Si Hezekia ndiye anayewadanganya mukufe kwa njaa au kiu anapowaambia: ‘Yawe, Mungu wenu atawaokoa toka mikono ya mufalme wa Asuria?’

12Si ni huyu Hezekia ndiye aliyeharibu pahali pake pa kuabudia na mazabahu zake na kuwaamuru watu wote wa inchi ya Yuda na Yerusalema akisema: ‘Mutaabudu mbele ya mazabahu moja, na juu yake mutateketeza sadaka zenu?’

13Hamujui yale yote ambayo mimi na babu zangu tumewatendea watu wote wa inchi zingine? Miungu ya watu wa inchi hizo iliweza kukomboa inchi zao toka mikono yangu?

14Ni mungu gani kati ya miungu ya mataifa yale yaliyoharibiwa kabisa na babu zangu aliyeweza kuwakomboa watu wake kutoka katika mikono yangu ndiyo nanyi mukuwe na tumaini kwamba Mungu wenu atawaokoa toka mikono yangu?

15Musidanganywe na Hezekia wala musishawishiwe kwa hayo. Musimwamini mutu huyu, kwa maana hakujatokea mungu wa taifa au mufalme yeyote aliyeweza kuwakomboa watu wake kutoka mikono ya mufalme wa Asuria. Vile vile mungu wenu hataweza!”

16Watumishi wa mufalme wa Asuria walisema maneno mengine mengi mabaya juu ya Mungu wetu Yawe na juu ya Hezekia mutumishi wake.

17Mufalme mwenyewe aliandika barua akamutukana na kumuzarau Yawe, Mungu wa Israeli, akisema: “Kama vile ambavyo miungu ya inchi zingine haikuweza kuwaokoa watu wao kutoka mikono yangu, vile vile mungu wa Hezekia hataweza kuwaokoa watu wake.”

18Wakubwa wale wakawaambia kwa sauti kubwa kwa luga ya Kiebrania, watu wa Yerusalema waliokuwa juu ya ukuta, wakikusudia kuwatia hofu na woga kusudi wakamate muji.

19Wakasema juu ya Mungu wa Yerusalema kama vile wangesema juu ya miungu ya mataifa mengine ambayo ni sanamu tu zilizotengenezwa kwa mikono ya wanadamu.

20Halafu mufalme Hezekia na nabii Isaya, mwana wa Amozi, wakamwomba Mungu na kumulilia awasaidie kwa ajili ya mambo haya.

21Naye Yawe akatuma malaika aliyewaua waaskari shujaa, majemadari na wakubwa katika kambi ya mufalme wa Asuria. Basi, mufalme wa Asuria akarudia katika inchi yake akijaa haya. Mara tu alipoingia ndani ya nyumba ya mungu wake, wana wake mwenyewe wakamwua palepale kwa upanga.

22Kwa njia hii basi, Yawe akamwokoa mufalme Hezekia na wakaaji wa Yerusalema kutoka mukono wa Saniharibu mufalme wa Asuria, na kutoka mukono wa waadui zake wote. Akawapa maisha ya amani na wajirani zao wote.

23Watu wengi sana walikuja wakamuletea Yawe sadaka kule Yerusalema, vilevile wakamuletea Hezekia, mufalme wa Yuda zawadi za bei kali. Hivyo kutoka wakati ule, akasifiwa sana na mataifa mengine yote.

Majivuno na ugonjwa wa Hezekia(2 Fal 20.1-3,12-19; Isa 38.1-3; 39.1-8)

24Wakati ule, Hezekia akagonjwa sana, karibu kufa. Akamwomba Yawe, naye akamujibu na kumwonyesha kitambulisho.

25Lakini Hezekia hakumutolea Yawe shukrani kwa yale yote aliyomutendea kwa sababu moyo wake ulikuwa umejaa majivuno. Hii ikasababisha kutaabika kwa inchi ya Yuda na Yerusalema.

26Kwa hiyo kasirani ikakuwa juu yake, juu ya inchi ya Yuda na juu ya Yerusalema. Kisha Hezekia akanyenyekea akaacha kuwa na moyo uliojaa majivuno, yeye na wakaaji wa Yerusalema wakajinyenyekeza; kwa hiyo kasirani ya Yawe haikuwafikia wakati wa utawala wa Hezekia.

Utajiri na utukufu wa mufalme Hezekia

27Mufalme Hezekia akatajirika sana na kuheshimiwa. Alijitengenezea hazina za feza, za zahabu, za mawe ya bei kali za viungo, ngao na za aina zote za vyombo vya bei kubwa.

28Vilevile alijijengea nyumba za kuwekea mazao ya ngano, divai na mafuta, na mazizi kwa ajili ya ngombe na mengine kwa ajili ya kondoo.

29Vile vile alijiongezea miji kwa ajili yake mwenyewe, makundi mengi ya ngombe na kondoo kwa sababu Yawe alimupa mali nyingi.

30Mufalme Hezekia ndiye aliyefunga maji ya chemichemi ya Gihoni, akayachimbia mufereji na kuyapitisha chini moja kwa moja mpaka upande wa magaribi wa muji wa Daudi. Hezekia alijaliwa katika kila jambo alilofanya,

31na hata wakati ambapo wajumbe wa wakubwa wa Babeli waliotumwa kwake kuuliza juu ya mambo ya ajabu yaliyotokea mule, Mungu, alimwacha ajiamulie mwenyewe, kusudi amupime na kujua yote yaliyokuwa ndani ya moyo wake.

Mwisho wa utawala wa Hezekia(2 Fal 20.20-21)

32Matendo mengine ya mufalme Hezekia na wema wake, yameandikwa katika “Maono ya nabii Isaya mwana wa Amozi,” katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli.

33Hezekia akakufa na kuzikwa kwenye sehemu ya juu ya makaburi ya wafalme. Watu wote wa inchi ya Yuda na wakaaji wa Yerusalema wakamutolea heshima kubwa wakati wa kifo chake, naye Manase, mwana wake, akatawala pahali pake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help