1Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Yawe, naye akawaacha watawaliwe na Wafilistini kwa miaka makumi ine.
2Kulikuwa mutu mumoja kule Zora, wa kabila la Dani, jina lake Manoa. Muke wake alikuwa tasa.
3Siku moja, malaika wa Yawe akamutokea yule mwanamuke, akamwambia: “Wewe ni tasa, hauna watoto. Lakini utapata mimba na kumuzaa mutoto mwanaume.
4Kwa hiyo ukuwe mwangalifu, usikunywe divai au kileo wala usikule kitu chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu,
5kwa maana utabeba mimba na kuzaa mutoto mwanaume. Nywele za mutoto huyo zisinyolewe hata kidogo, maana atakuwa Munaziri wa Mungu tangu kuzaliwa kwake. Naye ataanza kuwakomboa Waisraeli toka katika mikono ya Wafilistini.”
6Mwanamuke huyo akaenda kumwambia mume wake: “Mutu wa Mungu ambaye sura yake ilikuwa kama ya malaika wa Mungu alinitokea. Sikumwuliza anatoka wapi wala hakuniambia jina lake.
7Lakini aliniambia kwamba nitabeba mimba na kuzaa mutoto mwanaume. Aliniamuru nisikunywe divai au kileo wala kula chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu, maana mutoto huyo atakuwa Munaziri wa Mungu tangu kuzaliwa kwake mpaka atakapokufa.”
8Kisha Manoa akamwomba Yawe, akisema: “Ninakuomba, ee Yawe, umutume tena yule mutu wako uliyemutuma kusudi atufundishe mambo tunayopaswa kumutendea huyo mutoto atakayezaliwa.”
9Yawe akalisikia ombi la Manoa, na yule malaika wa Mungu akamwendea tena yule mwanamuke alipokuwa akiikaa katika shamba. Lakini mume wake Manoa hakukuwa pamoja naye.
10Mwanamuke akakimbia upesi, akamwambia mume wake: “Yule mutu aliyenijia siku ile amenitokea tena.”
11Manoa akafuatana naye mpaka kwa mutu huyo, akamwuliza: “Wewe ni yule mutu aliyezungumuza na mwanamuke huyu?”
Yule mutu akamujibu: “Ni mimi.”
12Kisha Manoa akasema: “Sasa maneno yako yatakapotimia ni mambo gani tutakayofuata kwa ajili ya huyo mutoto? Tutafanya nini kwa ajili yake?”
13Malaika wa Yawe akamwambia Manoa: “Muke wako atapaswa kushika yote niliyomwambia:
14asionje mazao yoyote ya muzabibu, wala asikunywe divai au kileo wala kula chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu. Yote niliyomwamuru, ayafuate.”
15Manoa akamwambia huyo malaika wa Yawe: “Tafazali, ukae kidogo tukutayarishie mwana-mbuzi.”
16Yule malaika wa Yawe akamwambia Manoa: “Hata kama mukinilazimisha kukaa, sitakula chakula chenu. Lakini kama ukipenda, tayarisha sadaka ya kuteketezwa kwa moto, umutolee Yawe.”
Manoa hakujua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe.
17Basi, Manoa akamwambia huyo malaika wa Yawe: “Utuambie jina lako kusudi tukuheshimu wakati maneno yako yatakapotimia.”
18Malaika wa Yawe akamujibu: “Kwa nini unataka kujua jina langu? Ni la ajabu.”
19Hapo Manoa akatayarisha mwana-mbuzi na sadaka, akaviweka juu ya jiwe apate kumutolea Yawe anayefanya maajabu.
20Basi wakati Manoa na muke wake walipokuwa wanaangalia ndimi za moto zikipanda juu mbinguni kutoka kwenye mazabahu, wakamwona malaika katika ndimi hizo akipanda kwenda mbinguni. Basi Manoa na muke wake wakainama uso mpaka chini.
21Manoa akajua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe. Malaika hakumutokea tena Manoa na muke wake.
22Basi, Manoa akamwambia muke wake: “Hakika tutakufa, maana tumemwona Mungu.”
23Lakini muke wake akamujibu: “Kama Yawe angetaka kutuua hangepokea sadaka yetu ya kuteketezwa kwa moto na ya ngano; wala hangetuonyesha mambo hayo wala kutuambia maagizo.”
24Kisha muke wa Manoa akazaa mutoto mwanaume, naye Manoa akamupa jina la Samusoni. Mutoto huyo akakomaa naye Yawe akamubariki.
25Roho wa Yawe akaanza kumusukuma akiwa kule Mahane-Dani, kati ya muji wa Zora na wa Estaoli.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.