1Solomono alitawala falme zote kuanzia kwa muto Furati mpaka katika inchi ya Wafilistini, na kuendelea hata kwa mupaka na Misri. Mataifa yote yalimutumikia na kulipa kodi kwake wakati wote wa maisha yake.
2Chakula Solomono alichohitaji kwa siku moja kwa ajili ya nyumba yake kilikuwa unga laini madebe mia tatu na makumi sita, na unga wa kawaida madebe mia saba na makumi mbili,
3ngombe wanono kumi, na ngombe makumi mbili toka shamba la malisho, kondoo mia moja pamoja na kulungu, paa, swala na kuku wanono.
4Inchi yote upande wa magaribi wa muto Furati, kutokea Tifusa mpaka muji wa Gaza, ilikuwa chini ya utawala wake. Wafalme wote upande wa magaribi wa muto Furati walikuwa chini yake, na alikuwa na amani na inchi zote jirani.
5Siku zote za utawala wake, watu wa Yuda na wa Israeli walikaa salama, kila mutu akistawi kwenye miti yake ya mizabibu na ya tini.
6Solomono alikuwa na vibanda elfu makumi ine kwa ajili ya farasi wa magari yake ya kukokotwa, na waaskari wapanda-farasi elfu kumi na mbili.
7Wale maliwali wake kumi na wawili, kila mumoja kwa mwezi aliopangiwa, walipeleka chakula cha kutosha kwa ajili ya mufalme na wale wote waliokula katika nyumba yake. Mahitaji yao yote yalitoshelezwa.
8Zamu ya kila mumoja ilipofika, alipeleka vilevile shayiri na majani ya kulisha farasi na nyama wanaokimbia mbio.
9Mungu alimupa Solomono hekima zaidi na akili kwa wingi. Maarifa yake yalikuwa kama muchanga wa bahari, hayakukuwa na kipimo.
10Hekima ya Solomono iliipita hekima ya watu wa mashariki na iliishinda hekima ya watu wa Misri.
11Aliwashinda watu wote kwa hekima; aliwashinda Etani, yule Muezra, Hemani na Kalkoli na Darda, wana wa Maholi; na sifa zake zilienea katika mataifa yote jirani.
12Alitunga mezali elfu tatu na nyimbo elfu moja na tano.
13Alizungumuzia habari za miti, kuanzia mwerezi unaokuwa Lebanoni, hata hisopo, muti unaotambaa juu ya ukuta. Alizungumuzia vilevile juu ya nyama, ndege, viumbe vinavyotambaa, na samaki.
14Watu kutoka mataifa yote, na wafalme wote waliopata kusikia habari juu ya hekima yake, walikuja kumusikiliza.
Solomono anajitayarisha kujenga hekalu(2 Sik 2.1-17)15Mufalme Hiramu wa Tiro, aliyekuwa rafiki ya Daudi, alipopata habari kwamba Solomono amekuwa mufalme pahali pa baba yake, alituma watumishi kwake.
16Halafu Solomono akamupelekea Hiramu ujumbe huu:
17“Unajua kwamba baba yangu Daudi hakuweza kumujengea Yawe, Mungu wake, hekalu la kumwabudia, kwa sababu ya vita vilivyomuzunguka pande zote mpaka hapo Yawe alipomupatia ushindi.
18Lakini sasa, Yawe, Mungu wangu, amenijalia amani pande zote. Sina adui wala taabu.
19Basi, nimeamua kumujengea Yawe, Mungu wangu, nyumba ya kumwabudia. Na hii ni sawa kabisa kama Yawe alivyomwahidi baba yangu akisema: ‘Mwana wako ambaye nitamwikalisha katika kiti chako cha kifalme, atanijengea nyumba.’
20Sasa basi, uwaamuru watu wako wanikatie miti ya mierezi ya Lebanoni. Watu wangu watajiunga na watu wako katika kazi hiyo, nami nitawalipa watumishi wako kadiri utakavyosema. Maana kama vile unavyojua, hakuna yeyote mwenye kuwa fundi wa kukata miti kama ninyi Wasidoni.”
21Hiramu alifurahi sana alipopata ujumbe huu wa Solomono, akasema: “Yawe asifiwe wakati huu, kwa kumupa Daudi mwana mwenye hekima atawale taifa hili kubwa.”
22Kisha, Hiramu alimupelekea Solomono ujumbe, akisema: “Nimepokea ujumbe wako, nami niko tayari kutimiza mahitaji yako juu ya mbao za mierezi na za miberoshi.
23Watu wangu watasomba magogo na kuyateremusha kutoka Lebanoni mpaka katika bahari na kuyafunga mafungumafungu kusudi yaelee juu ya maji mpaka pahali utakaponielezea. Kule, yatafunguliwa nawe utayapokea. Kwa upande wako, wewe utanipa chakula kwa ajili ya watu wa nyumba yangu.”
24Basi, Hiramu alimupa Solomono mbao zote za aina ya mierezi na miberoshi alizohitaji,
25naye Solomono akamupa Hiramu ngano madebe elfu mia mbili na makumi ine, na mafuta safi madebe mia mbili kila mwaka, kwa ajili ya watu wa nyumba yake.
26Basi, Yawe akamupa Solomono hekima kama alivyomwahidi. Kukakuwa amani kati ya Solomono na Hiramu; wakafanya mapatano kati yao.
27Mufalme Solomono alikusanya watu elfu makumi tatu kutoka kila pahali katika inchi ya Israeli, wafanye kazi za kulazimishwa,
28akamuweka Adoniramu akuwe musimamizi wao. Aliwagawanya watu hao katika makundi matatu ya watu elfu kumi kila moja, akayapeleka makundi hayo kwa zamu, mwezi mumoja Lebanoni na miezi miwili kwao.
29Solomono alikuwa vilevile na wabebaji wa mizigo elfu makumi saba, na wachongaji wa mawe elfu makumi nane kwenye milima,
30bila kuhesabu wasimamizi elfu tatu na mia tatu waliosimamia kazi hiyo na wafanyakazi wote.
31Kwa amri ya mufalme, walichimbua mawe makubwa na ya bei kali, kusudi yachongwe kwa ajili ya kujenga musingi wa nyumba.
32Basi, hivi ndivyo wajengaji wa Solomono na Hiramu na watu wa muji wa Gebali walivyotayarisha mawe na mbao za kujenga nyumba hiyo.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.