1Katika siku zile hakukukuwa mufalme katika Israeli. Basi kabila la Dani lilikuwa linatafuta eneo lake lenyewe la kuishi ndani yake, maana mpaka wakati ule, halikukuwa limegawanyiwa sehemu yake lenyewe kati ya makabila ya Israeli.
2Kwa hiyo watu wa kabila la Dani wakachagua kati yao watu hodari, wakawatuma kutoka kule Estaoli na Zora, wakawaamuru waende kuipeleleza inchi. Basi watu hao wakafika katika inchi ya milima ya Efuraimu katika nyumba ya Mika, wakaenda na kukaa mule.
3Walipokuwa kwa Mika, wakaitambua sauti ya yule kijana Mulawi. Wakamugeukia na kumwuliza: “Nani amekuleta huku? Una shuguli gani hapa?”
4Yeye akawajibu: “Mika amefanya nami mupango. Amenipa kazi nami nimekuwa kuhani wake.”
5Nao wakamwambia: “Tafazali utuulizie kwa Yawe kama tutafanikiwa katika safari yetu.”
6Yule kuhani akawaambia: “Muende kwa amani. Yawe anaichunga safari yenu.”
7Basi, watu hao watano wakaondoka, wakaenda Laisi. Waliwaona watu walioishi kule, na jinsi walivyokaa kwa usalama kama vile watu wa Sidona. Walikuwa watu watulivu wasiokuwa na wasiwasi na hawakupungukiwa mahitaji yoyote katika inchi. Walikuwa mbali na watu wa Sidona, na hawakukuwa na shuguli yoyote na watu wengine.
8Basi hao wapelelezi wakarudi kwa wandugu zao huko Zora na Estaoli, nao wakawauliza: “Mumetuletea habari gani?”
9Wao wakasema: “Musimame tuende na kuishambulia inchi hiyo. Tumeiona na kweli ni inchi yenye mboleo. Mutakaa hapa tu bila kufanya kitu? Musikawie kwenda kuirizi inchi hiyo.
10Mutakapofika kule mutakuta watu wasiokuwa na wasiwasi wowote. Inchi hiyo ni kubwa, haikupungukiwa chochote, na Mungu ameitia katika mikono yetu.”
11Basi, watu mia sita wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita wakaondoka kutoka Zora na Estaoli,
12wakaenda kupiga kambi yao kule Kiriati-Yearimu katika inchi ya Yuda. Ndiyo maana pahali pale, upande wa magaribi wa Kiriati-Yearimu pameitwa Kambi ya Dani mpaka leo.
13Kutoka kule wakaelekea inchi ya milima ya Efuraimu, wakafika katika nyumba ya Mika.
14Watu wale watano waliokwenda kuipeleleza inchi ya Laisi wakawaambia wandugu zao: “Munajua kwamba katika nyumba moja kati ya hizi kuna kizibao, sanamu ya kuchongwa na sanamu yenye kuyeyushwa? Basi, mufikiri namna ya kufanya.”
15Basi wale wapelelezi wakaelekea kwenye nyumba ya Mika, wakaingia ndani na kumwuliza habari za yule kijana Mulawi.
16Wakati ule, wale watu mia sita wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita wakasimama kwenye mulango.
17Wale watu watano waliokwenda kuipeleleza inchi wakaingia ndani, wakabeba ile sanamu ya mungu yenye kuyeyushwa, kile kizibao na sanamu ya ibada. Wakati ule yule kuhani alikuwa akisimama kwenye mulango pamoja na wale watu mia sita wenye silaha.
18Basi, alipowaona wale wapelelezi wanaingia ndani ya nyumba ya Mika na kutwaa sanamu ya kuchonga, kifuko cha kuomba shauri, sanamu ya kuchongwa na sanamu ile yenye kuyeyushwa, akawauliza: “Munafanya nini?”
19Nao wakamwambia: “Nyamaza, funga kinywa chako, ukuje pamoja nasi, ukuwe kuhani wetu na kama baba yetu. Au unaona namna gani? Inafaa kwako zaidi kuwa kuhani wa mutu mumoja au kuwa kuhani wa kabila moja la Israeli?”
20Yule kuhani akafurahi sana akatwaa kile kifuko, ile sanamu ya ibada, na ile sanamu ya mungu yenye kuyeyushwa, akafuatana nao.
21Basi, wakaanza safari yao, na walikuwa wanatanguliwa na watoto wao na nyama wao na mali zao.
22Walipokuwa wamefika mbali na nyumba ya Mika, watu waliokuwa jirani na Mika wakaitwa, wakawafuatilia watu wa kabila la Dani, wakawafikia.
23Kisha wakawapigia kelele, nao watu wa kabila la Dani wakageuka, wakamwuliza Mika: “Una shida gani hata umetufuatilia pamoja na kundi hili lote?”
24Mika akasema: “Ninyi mumebeba miungu yangu niliyojitengenezea, mukamutwaa na kuhani wangu, mukaniacha bila kitu chochote. Munaweza namna gani basi kuniuliza nina shida gani?”
25Watu wa kabila la Dani wakamwambia: “Afazali uache kelele zako, kama sivyo wengine wetu wenye hasira wanaweza kukushambulia, nawe utapoteza maisha yako na maisha ya jamaa yako.”
26Mika alipoona kwamba wamemuzidia nguvu, akageuka, akarudi kwake; nao watu wa kabila la Dani wakaenda zao.
27Hao watu wa kabila la Dani walivitwaa vitu vile ambavyo Mika alikuwa amevitengeneza, na kumupeleka yule kuhani aliyemutumikia. Basi wakaenda kushambulia muji wa Laisi, wakawaua wakaaji wake ambao waliishi mule kwa utulivu na bila wasiwasi, wakauteketeza muji ule.
28Wakaaji wa muji ule hawakukuwa na mutu wa kuwaokoa kwa sababu walikuwa mbali na muji wa Sidona, tena hawakukuwa na ushirika na watu wengine. Muji ule ulikuwa kwenye bonde la Beti-Rehobu. Watu wa kabila la Dani wakaujenga upya, wakaishi mule.
29Walibadilisha jina la muji ule, wakauita Dani, kufuata jina la babu yao aliyekuwa mwana wa Israeli. Lakini muji ule pale mbele uliitwa Laisi.
30Watu wa kabila la Dani wakaisimika ile sanamu ya kuchonga, naye Yonatani mwana wa Gersoni, mujukuu wa Musa, akakuwa kuhani wao. Wazao wake vilevile walikuwa makuhani wa kabila la Dani mpaka wanainchi wa inchi hiyo walipopelekwa katika uhamisho.
31Wakati wote nyumba ya Mungu ilipokuwa kule Shilo, watu wa kabila la Dani waliiabudu sanamu ya kuchonga ambayo Mika aliitengeneza.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.