Muhubiri 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Basi, nikawaza: “Ngoja nijitumbukize katika raha, nijifurahishe.” Lakini, niligundua kwamba hiyo nayo ni bure.

2Nikasema juu ya kicheko: “Ni wazimu”, na raha: “Iko na faida gani?”

3Nilitafuta kwa hekima namna ya kujichangamusha mwili kwa divai na kutenda sawa na wapumbafu. Nilitaka kuona kitu gani ni kizuri kwa wanadamu kufanya wanapoishi maisha yao mafupi hapa chini ya mbingu.

4Nilifanya mambo makubwa: nilijenga nyumba na kujilimia mashamba ya mizabibu.

5Nilijifanyia bustani na mashamba ya miti, nikapanda miti ya matunda ya kila aina.

6Nilijichimbia visima vya maji ya kumwangilia ile miti.

7Nilinunua watumwa, wajakazi, na wengine wakazaliwa katika nyumba yangu. Nilikuwa na mali mengi, makundi ya ngombe na kondoo wengi kuliko mutu yeyote aliyenitangulia kukaa Yerusalema.

8Nilijikusanyia feza na zahabu kutoka hazina za wafalme na toka katika majimbo, nami nilipata waimbaji wanaume na wanawake, na wahabara wanaotamaniwa.

9Nikakuwa mukubwa, mukubwa kuwapita wote waliopata kuwa katika Yerusalema mbele yangu. Na hekima yangu ikakaa ndani yangu.

10Kila kitu macho yangu yalichokitamani nilikipata. Moyo wangu sikuunyima raha yoyote. Moyo wangu ulifurahia mambo niliyotenda, na hii ilikuwa zawadi ya jasho langu.

11Kisha nikafikiri juu ya yote niliyokuwa nimefanya kwa mikono yangu, na jinsi nilivyotoa jasho kwa kuyafanya. Nikatambua kwamba yote ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. Hakukukuwa faida yoyote chini ya jua.

12Basi, nikaanza kufikiri maana ya kuwa na hekima, kuwa mwenda-wazimu, na kuwa mupumbafu. Nikajiuliza: “Mufalme mupya anaweza kufanya kitu gani? Atafanya tu kile kilichofanywa mbele yake.”

13Basi, mimi nikagundua kwamba hekima ni bora kuliko upumbafu, kama vile mwangaza unavyokuwa bora kuliko giza.

14Mwenye hekima anaona anakokwenda, lakini mupumbafu anatembea katika giza. Hata hivyo, ninajua vilevile kwamba mwisho wao wote wawili ni mumoja.

15Basi, nikasema ndani ya moyo wangu: “Yatakayomupata mupumbafu yatanipata na mimi vilevile. Kwa nini, basi, nimekuwa na hekima zaidi?”

Nikasema ndani ya moyo wangu: “Hayo nayo ni bure.”

16Maana hakuna anayemukumbuka mwenye hekima, wala anayemukumbuka mupumbafu, maana katika siku zinazokuja wote watasahaulika. Maana mwenye hekima anakufa sawasawa na mupumbafu!

17Kwa hiyo, nikachukia maisha, maana yote yanayotendeka chini ya jua yalinisikitisha. Yote ni bure sawa na kutaka kukamata upepo.

18Nikachukia jasho yote niliyotoa hapa chini ya jua, kuona kwamba ilinipasa nimwachie mutu ambaye atatawala nyuma yangu.

19Tena, ni nani anayejua kwamba atakuwa mwenye hekima au atakuwa mupumbafu? Hata hivyo, yeye atarizi yote niliyofanya kwa kutoa jasho na kutumia hekima yangu hapa chini ya jua. Hayo nayo ni bure.

20Basi, nilipofikiri tena juu ya jasho yote niliyotoa chini ya jua, nilikata tamaa.

21Maana, wakati mwingine, mutu ambaye amefanya kazi kwa kutumia hekima, akili na maarifa yake, anamwachia mutu mwingine afurahie matunda ya kazi ambayo hakuitoshea jasho. Hayo nayo ni bure. Ni jambo baya sana.

22Mutu anafaidia nini kutokana na jasho yake yote, na juhudi anazohangaika nazo chini ya jua?

23Maisha yake yote yamejaa taabu, na jasho yake ni mahangaiko matupu. Hata usiku akili yake haipumziki! Hayo nayo ni bure.

24Hakuna kitu kizuri kwa mwanadamu, isipokuwa kula na kunywa na kufurahia matunda ya jasho yake. Hili nalo nimeliona kwamba linatoka kwa Mungu, Muh 3.13; 5.18; 9.7

25maana usipojaliwa na Mungu, hauwezi kupata chakula wala kujifurahisha.

26Mungu anamujalia mutu anayependezwa naye hekima, akili na furaha; lakini anamupa mwenye zambi kazi ya kuvuna na kulundika, kisha Mungu anavipatia yule anayemupendeza. Hayo nayo ni bure sawa na kutaka kukamata upepo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help