1 Wakorinto 3 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Watumishi wa Mungu

1Kweli wandugu zangu, sikuweza kusema nanyi kama watu wanaotawaliwa na Roho wa Mungu, lakini kama watu wanaotawaliwa na mambo ya kidunia. Mungali kama watoto wachanga katika mambo ya Kikristo.

2Niliwakunywesha maziwa, sikuwapa chakula kigumu, kwa maana mulikuwa hamujakiweza bado. Na hata sasa hamukiwezi,

3kwa sababu mungali munatawaliwa na mambo ya kidunia. Kwa maana ikiwa kungali wivu na ugomvi katikati yenu, haionyeshi kwamba munatawaliwa na mambo ya kidunia, nanyi munaishi kufuatana na hali ya kimutu?

4Wakati mumoja wenu anaposema: “Mimi ni wa Paulo” na mwingine anasema: “Mimi ni wa Apolo,” basi ninyi hamufanyi mambo ya kidunia?

5Basi, Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Sisi ni watumishi wa Mungu, waliowaonyesha ninyi njia ya kuamini. Tumefanya vile kila mumoja wetu kwa kadiri ya zawadi aliyopewa na Bwana.

6Mimi nilipanda mbegu na Apolo alinyweshea maji, lakini Mungu ndiye aliyeiotesha.

7Hivi yule anayepanda na yule anayenyweshea maji, wote si kitu; Mungu ndiye anayekuwa wa lazima kwa maana ni yeye anayeotesha mbegu.

8Yule anayepanda na yule anayenyweshea maji wote ni sawa; naye Mungu atamupa kila mutu mushahara wake kufuatana na kazi aliyofanya.

9Kwa maana sisi tunashirikiana na Mungu katika kazi, na ninyi ni shamba la Mungu.

Vilevile ninyi ni majengo ya Mungu.

10Kwa kadiri ya zawadi Mungu aliyonipatia, kama vile fundi wa kujenga mwenye hekima, niliweka musingi. Na sasa, mutu mwingine anajenga juu yake. Lakini inafaa kila mutu aangalie vizuri namna anavyojenga.

11Kwa maana hakuna mutu anayeweza kuweka musingi mwingine pahali pa ule uliokwisha kuwekwa, ni kusema Yesu Kristo.

12Mutu anaweza kujenga juu ya musingi huu na zahabu, feza, mawe ya bei kali, miti, nyasi au majani.

13Lakini hali ya kazi ya kila mutu itaonekana wazi, kwa sababu Siku ile ya hukumu itaionyesha waziwazi. Kwa maana Siku ile itajitokeza katikati ya moto, na moto ule ndio utakaopima na kuonyesha hali ya kazi ya kila mutu.

14Na ikiwa kile mutu alichojenga juu ya musingi huu hakiungui na moto, mutu yule atapokea zawadi.

15Lakini kama kile alichojenga kikiungua, yeye atakosa zawadi, hata hivi yeye mwenyewe ataokolewa, lakini itakuwa kama vile ameopolewa toka ndani ya moto.

16Hamujui hakika kuwa ninyi ni hekalu la Mungu na kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu?

17Basi mutu akiharibu hekalu la Mungu, Mungu atamuharibu vilevile. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, na ninyi ndilo hekalu lake.

18Mutu yeyote asijidanganye mwenyewe. Kama mutu fulani kati yenu akijizania kuwa mwenye hekima ya kidunia, ajifanye kama mupumbafu kusudi apate kuwa na hekima ya kweli.

19Kwa maana hekima ya kidunia ni upumbafu mbele ya Mungu. Ni sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Mungu anawanasa wenye hekima katika werevu wao wenyewe.”

20Nayo yanasema vilevile: “Bwana anatambua mawazo ya wenye hekima; anajua kwamba ni ya bure.”

21Basi mutu asijivune kwa ajili ya wanadamu. Kwa maana vitu vyote ni vyenu:

22ikiwa Paulo, Apolo au Petro, dunia, uzima, kifo, mambo ya sasa au mambo yatakayokuja.

23Lakini ninyi ni watu wa Kristo, naye Kristo ni wa Mungu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help