Marko 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Desturi za babu(Mat 15.1-9)

1Wafarisayo na walimu wamoja wa Sheria waliotoka Yerusalema wakakusanyika mbele ya Yesu.

2Wakawaona wanafunzi wake wamoja wakikula chakula na mikono michafu, maana yake, mikono waliyokosa kunawa kufuatana na desturi ya dini yao.

3Ilikuwa vile kwa maana Wafarisayo na Wayuda wote wanashika desturi za babu zao; zinazokataza kula pasipo kunawa mikono kama inavyostahili.

4Tena, wanapotoka kwa soko, hawakuli pasipo kuoga kwanza. Na zaidi ya hii wanashika desturi zingine nyingi kama vile namna ya kusafisha vikombe, mitungi na vyungu vilivyotengenezwa na shaba.

5Basi Wafarisayo na walimu wa Sheria wakamwuliza Yesu: “Sababu gani wanafunzi wako hawafuati desturi za babu zetu, lakini wanakula chakula na mikono michafu?”

6Yesu akawajibu: “Isaya alitabiri vema wakati alipoandika maneno haya juu yenu ninyi wanafiki:

‘Mungu anasema:

Watu hawa wananiheshimu kwa midomo yao,

lakini mioyo yao ni mbali nami.

7Ibada wanayonifanyia ni ya bure,

sababu mafundisho yao

yanalingana na kanuni za watu tu.’ ”

8Yesu akaendelea kuwaambia: “Munaacha amri za Mungu pembeni na kushika desturi za watu.

9Munajua vizuri namna ya kutupilia amri za Mungu kusudi mushike desturi zenu!

10Maana Musa alisema: ‘Uwaheshimu baba yako na mama yako,’ na, ‘Anayemutukana baba yake au mama yake, anapaswa kuuawa.’

11Lakini ninyi munasema kwamba mutu akiwa na kitu cha kumusaidia baba au mama yake, lakini akimwambia kwamba kitu kile ni Korbane, (maana yake, kimetolewa kuwa sadaka takatifu kwa Mungu),

12munamuruhusu asiwasaidie wazazi wake.

13Hivi munazarau Neno la Mungu kwa ajili ya desturi zenu munazopokezana. Nanyi munafanya mambo mengine mengi ya namna ile.”

Mambo yanayomuchafua mutu(Mat 15.10-20)

14Kisha Yesu akaita tena kundi la watu na kuwaambia: “Ninyi wote munisikilize na kuelewa maneno haya.

15Hakuna kitu kinachoingia ndani ya mutu kutoka inje kinachoweza kumuchafua. Lakini kitu kinachotoka ndani yake ndicho kinachomuchafua.”

17Wakati Yesu alipoachana na kundi na kuingia ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamwuliza maana ya mufano ule.

18Naye akawaambia: “Hata ninyi vilevile hamuwezi kuelewa? Hamufahamu kwamba kila kitu kinachoingia ndani ya mutu kutoka inje hakiwezi kumuchafua?

19Kitu kile hakiingii ndani ya moyo wake, lakini kinaingia tu ndani ya tumbo na kisha kinatoka na kwenda katika choo.” (Kwa kusema hivi Yesu alionyesha kwamba vyakula vyote vinaruhusiwa kukuliwa.)

20Yesu akaongeza kusema: “Ni kile kinachotoka ndani ya mutu ndicho kinachomuchafua.

21Kwa maana ni ndani ya mutu, ni kusema ndani ya moyo wake, ndimo munamotoka mawazo mabaya yanayoleta: uzinzi, wizi, uuaji,

22uasherati, tamaa mbaya, matendo mabaya, ukorofi, maisha ya ovyo, wivu, matukano, majivuno na upumbafu.

23Maovu haya yote yanatoka ndani ya mutu, nayo yanamufanya kuwa muchafu.”

Imani ya mwanamuke Musuria(Mat 15.21-28)

24Kisha Yesu akaondoka pale, na kwenda katika jimbo lililokuwa karibu na muji Tiro. Akaingia ndani ya nyumba, naye hakutaka mutu ajue kwamba yuko mule, lakini haikuwezekana kwake kujificha.

25Mwanamuke mumoja, binti yake aliyeshikwa na pepo, akasikia habari za Yesu. Mara moja akamufikia Yesu na kujitupa kwa miguu yake.

26Mwanamuke yule hakukuwa wa taifa la Wayuda. Alikuwa muzaliwa wa jimbo la Foinikia, katika inchi ya Suria. Yeye akamwomba Yesu afukuze yule pepo kutoka ndani ya binti yake.

27Lakini Yesu akamujibu: “Uwaache kwanza watoto wa nyumba washibe, kwa sababu si vizuri kukamata chakula cha watoto na kukitupia imbwa.”

28Mwanamuke yule akamujibu: “Bwana, unasema ukweli, lakini hata imbwa wanazoea kula makombo watoto wanayoyaangusha chini ya meza.”

29Basi Yesu akamwambia: “Kwa sababu ya jibu hili, unaweza kurudi kwako, yule pepo ametoka ndani ya binti yako.”

30Mwanamuke yule alipofika kwake, akamwona binti yake akilala katika kitanda; na yule pepo alikuwa amekwisha kutoka ndani yake.

Yesu anaponyesha kiziwi

31Kisha Yesu akaondoka kule katika jimbo lililokuwa karibu na Tiro, akapita Sidona na katikati ya inchi ya Miji Kumi, hata akafika kwenye ziwa la Galilaya.

32Wakamuletea mutu mumoja aliyekuwa kiziwi na mwenye kigugumizi vilevile. Wale waliomuleta wakamusihi Yesu amuponyeshe kwa kuweka mikono juu yake.

33Basi Yesu akamwondoa yule mutu kati ya kundi, akaenda naye mbali kidogo, akamutia vidole ndani ya masikio, akatema mate na kumugusa ulimi kwa mate yale.

34Kisha Yesu akaangalia juu mbinguni, akasisimua na kumwambia yule mutu: “Efata,” maana yake, “Funguka!”

35Mara moja masikio yake yakafunguka, nao ulimi wake ukafunguliwa, akaanza kusema vizuri.

36Yesu akawaagiza wasimwambie mutu habari ya tendo hili. Lakini kwa kadiri alivyowakataza, wao walizidi kutangaza habari.

37Nao watu wakashangaa sana na kusema: “Mambo anayofanya ni mazuri kweli. Anawawezesha hata viziwi wasikie, nao wabubu wapate kusema.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help