1Asubui mapema Yoshua pamoja na watu wote wa Israeli walianza safari kutoka Sitimu. Walipofika kwa muto Yordani, walipiga kambi hapo kwa muda mbele ya kuvuka.
2Nyuma ya siku tatu, viongozi walipita katikati ya kambi hiyo,
3wakawaambia watu: “Mutakapoliona Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wenu, limebebwa na makuhani Walawi, mutaondoka na kulifuata;
4ndivyo mutakavyojua njia ya kupita maana hamujapita huku hata kidogo. Lakini musilikaribie sana Sanduku la Agano; mukuwe kwa umbali wa kilometre moja hivi.”
5Yoshua akawaambia watu: “Mujitakase kwa sababu kesho Yawe atatenda maajabu kati yenu.”
6Kisha akawaambia makuhani: “Mutwae Sanduku la Agano, mutangulie nalo mbele ya watu.” Nao wakalitwaa na kutangulia mbele ya watu.
7Yawe akamwambia Yoshua: “Leo hii, nitaanza kukutukuza mbele ya watu wote wa Israeli kusudi wajue kwamba, kama vile nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo vilevile nitakavyokuwa pamoja nawe.
8Utawaamuru hao makuhani wanaobeba Sanduku la Agano wasimame karibu na ukingo wa muto Yordani wakati watakapofika kule.”
9Kisha Yoshua akawaambia Waisraeli: “Musogee karibu mupate kusikia maneno ya Yawe, Mungu wenu.”
10Yoshua akaendelea kusema: “Sasa mutajulishwa kabisa kwamba Mungu Mwenye Uzima yuko kati yenu na kwamba atawafukuza mbele yenu Wakanana, Wahiti, Wahivi, Waperizi, Wagirgasi na Waamoni, na Wayebusi.
11Muangalie, Sanduku la Agano la Bwana wa dunia yote liko karibu kupita mbele yenu kuelekea muto Yordani.
12Sasa, muchague watu kumi na wawili kutoka makabila ya Israeli, kila kabila mutu mumoja.
13Wakati miguu ya makuhani wanaobeba Sanduku la Agano la Yawe, Bwana wa dunia yote, itakapoingia katika maji ya muto Yordani, maji ya muto huo yataacha kutiririka. Na yale yatakayokuwa yanatiririka kutoka upande wa juu yatajikusanya pamoja kama lundo.”
14Basi, watu waliondoka katika kambi zao kwa kwenda kuvuka muto Yordani, nao makuhani wakiwa wamebeba Sanduku la Agano walitangulia watu.
15Na mara tu hao waliobeba Sanduku la Agano walipofika Yordani na miguu yao ilipokanyaga kwenye ukingo wa muto ule (muto Yordani unafurika wakati wa mavuno),
16maji yaliyokuwa yanatiririka kutoka upande wa juu yalisimama na kulundikana mpaka kule Adamu kijiji kinachokuwa karibu na muji wa Zaretani. Maji yaliyokuwa yanateremuka kwenda katika bahari ya Araba, ni kusema bahari ya Chumvi, yalitoweka kabisa, watu wakavuka mbele ya Yeriko.
17Wakati Waisraeli walipokuwa wanavuka, makuhani waliokuwa wanalibeba Sanduku la Agano walisimama pahali pakavu katikati ya muto Yordani mpaka taifa lote likavuka.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.