1Zaburi ya Asafu.
Hakika, Mungu ni muzuri kwa Israeli,
kwa watu wenye moyo safi.
2Nilikuwa karibu sana kujikwaa,
kidogo tu ningeteleza,
3maana niliwaonea wivu wenye kiburi,
nilipoona wakosaji wakifanikiwa.
4Maana hao hawapatwi na mateso;
miili yao ina afya, nao wana nguvu.
5Taabu za mwanadamu haziwapati hao;
hawapati mateso kama watu wengine.
6Kiburi kimekuwa kama mukufu katika shingo,
mateso makali ni kama nguo yao.
7Mazarau yanatokana na unene wao;
mioyo yao inatiririka mipango mibaya.
8Wanawachekelea wengine na kusema mabaya;
wanajivuna na kufanya mipango ya utesaji.
9Kwa vinywa vyao wanatukana mbingu;
kwa ndimi zao wanajitapa katika dunia.
10Hata watu wa Mungu wanawafuata,
hawaoni kwao kitu chochote kibaya
na kusadiki kila wanachosema.
11Wanasema: “Mungu hawezi kujua!
Mungu Mukubwa hataweza kugundua!”
12Hivi ndivyo watu waovu wanavyokuwa;
wako na kila kitu, nao wanapata hata zaidi.
13Kweli ni kwa bure nimejichunga katika usafi wa moyo,
na kujilinda nisitende zambi?
14Muchana kutwa ninapata mapigo,
kila asubui nimepata mateso.
15Ningalisema kama wao,
ningalikuwa mwenye uasi kati ya watu wako.
16Basi, nilijaribu kufikiri juu ya jambo hili,
lakini lilikuwa gumu sana kwangu,
17mpaka nilipoingia pahali pako patakatifu.
Halafu nikatambua yatakayowapata waovu.
18Kweli wewe unawaweka pahali penye utelezi;
unawafanya waanguke na kuangamia.
19Wanaangamizwa kwa rafla,
wateketezwe kabisa kwa vitisho.
20Ee Bwana, unapoinuka, wanatoweka kama ndoto,
kama ndoto wakati mutu anapoamuka.
21Nilipoona uchungu katika moyo
na kuchomwa katika roho,
22nilikuwa mupumbafu na mujinga,
nilikuwa kama nyama mbele yako.
23Hata hivyo siku zote niko nawe, ee Mungu!
Unanishika mukono wa kuume.
24Wewe unaniongoza kwa mashauri yako;
na kwa mwisho utanipokea kwenye utukufu.
25Mbinguni, nani anayeweza kunisaidia isipokuwa wewe?
Na katika dunia hamuna ninachokitamani isipokuwa wewe!
26Hata nikikosa nguvu katika mwili na katika roho,
wewe, ee Mungu, ni kikingio changu;
na hitaji langu lote ni wewe kwa milele.
27Anayejitenga nawe, hakika ataangamia.
Anayekukana, utamwangamiza.
28Lakini, kwangu ni vizuri kuwa karibu na Mungu.
Wewe Bwana wangu Yawe ndiwe usalama wangu.
Nitatangaza mambo yote uliyotenda!
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.