Mezali 15 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kujibu kwa upole kunatuliza hasira, lakini neno kali linachochea hasira.

2Ulimi wa mwenye hekima unaeneza maarifa, lakini watu wapumbafu wanamwanga maneno ya ujinga.

3Macho ya Yawe yanaona kila kitu, yanachunguza kibaya na kizuri.

4Ulimi mupole ni musingi wa uzima, lakini uovu wake unavunja moyo.

5Mupumbafu anazarau mafundisho ya baba yake, lakini anayekubali maonyo ni mwenye akili.

6Katika nyumba ya mwenye haki kuna wingi wa mali, lakini mapato ya waovu yanaleta hasara.

7Mudomo wa mwenye hekima unaeneza maarifa, lakini sivyo kwa mioyo ya wapumbafu.

8Sadaka ya waovu ni chukizo kwa Yawe, lakini maombi ya watu wa usawa yanamufurahisha Mungu.

9Mwenendo wa waovu ni chukizo kwa Yawe, lakini Mungu anawapenda wale wanaofuata mambo ya haki.

10Azabu kali ni kwa wanaoacha mwenendo mwema; yeyote anayechukia kuonywa atakufa.

11Ikiwa Yawe anajua kuzimu na shimo la kuangamia, mawazo ya mwanadamu yataweza namna gani kujificha mbele yake?

12Mwenye mazarau hapendi kuonywa, hatafuti hata kidogo maoni ya wenye hekima.

13Moyo wa furaha unaangarisha uso, lakini uchungu unavunja moyo.

14Mwenye akili anatafuta maarifa, lakini wapumbafu wanajikulisha upumbafu.

15Kwa mwenye kuteswa, kila siku ni mbaya, lakini kwa mwenye raha ni sikukuu.

16Afazali kuwa na kidogo na kumwogopa Yawe, kuliko kuwa na mali nyingi pamoja na taabu.

17Afazali kula mboga za majani kwa upendo, kuliko karamu ya nyama nono pamoja na chuki.

18Mutu wa hasira mbaya anasababisha ugomvi, lakini asiyekuwa mwepesi wa hasira anautuliza.

19Njia ya muvivu inajaa miiba, lakini njia ya mutu wa usawa ni wazi kama barabara kubwa.

20Mutoto mwenye hekima anamufurahisha baba yake, lakini mupumbafu anamuzarau mama yake.

21Upumbafu ni furaha kwa mutu asiyekuwa na akili, lakini mwenye akili anachagua njia inayokuwa sawa.

22Mipango inaharibika kwa kukosa shauri, lakini kwa washauri wengi, inasimama.

23Kutoa jibu zuri kunafurahisha; neno linalofaa kwa wakati wake ni jema sana!

24Njia ya mwenye hekima inaelekea juu kwenye uzima, kusudi aepuke kuingia chini katika kuzimu.

25Yawe anabomoa makao ya wenye kiburi, lakini analinda mipaka ya makao ya mujane.

26Mawazo ya mwovu ni chukizo kwa Yawe, lakini maneno mema yanamufurahisha.

27Anayetamani faida ya unyanganyi anataabisha jamaa yake, lakini anayechukia kituliro ataishi.

28Moyo wa mwenye haki unafikiri mbele ya kujibu, lakini kinywa cha mwovu kinatapika uovu.

29Yawe anajiweka mbali na watu waovu, lakini yuko karibu na wenye haki kwa kuwasikiliza.

30Uso wenye kuangaa unafurahisha moyo. Habari njema inarudishia mwili nguvu.

31Mutu ambaye anasikiliza maonyo mema ana nafasi yake kati ya wenye hekima.

32Anayekataa kufundishwa anajizarau mwenyewe, lakini anayekubali maonyo anapata ufahamu.

33Kumwogopa Yawe ni mafundisho ya hekima; mbele ya kuheshimika inafaa kuwa munyenyekevu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help