Zaburi 29 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Sauti ya Mungu katika zoruba

1Zaburi ya Daudi.

Mumupe Yawe heshima, enyi viumbe vya mbingu,

museme kwamba Yawe ni mutukufu na mwenye nguvu.

2Museme kwamba jina la Yawe ni tukufu.

Mumwabudu katika pahali pake patakatifu.

3Sauti ya Yawe inasikilika juu ya maji;

Mungu mutukufu anapiga radi,

sauti ya Yawe inasikilika juu ya bahari!

4Sauti ya Yawe ni yenye nguvu,

sauti ya Yawe ni yenye mamlaka.

5Sauti ya Yawe inavunja miti mikubwa ya mierezi;

Yawe anavunja mierezi ya Lebanoni.

6Anarusha milima ya Lebanoni kama mwana-ngombe,

milima ya Hermoni kama mwana-mbogo.

7Sauti ya Yawe inatokeza ndimi za moto.

8Sauti ya Yawe inatetemesha jangwa,

Yawe anatetemesha jangwa la Kadesi.

9Sauti ya Yawe inatikisa mivule,

inaongoa majani ya miti ya pori,

na wote wanaokuwa katika hekalu lake wanasema:

“Utukufu kwa Mungu!”

10Yawe ameikaa juu ya mafuriko ya maji;

Yawe ni mufalme anayetawala milele.

11Yawe awape watu wake nguvu!

Yawe awabariki watu wake kwa amani!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help