Matayo 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kujaribiwa kwa Yesu(Mk 1.12-13; Lk 4.1-13)

1Kisha Roho Mutakatifu akamwongoza Yesu kwenda katika jangwa kusudi ajaribiwe na Shetani.

2Naye Yesu alipomaliza kufunga kula chakula kwa muda wa siku makumi ine, muchana na usiku, akasikia njaa.

3Shetani akamufikia na kumwambia: “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, amuru mawe haya yageuke kuwa mikate.”

4Yesu akamujibu: “Imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: ‘Mutu hawezi kuishi kwa mukate tu, lakini kwa njia ya kushika kila neno Mungu analosema.’ ”

5Halafu Shetani akamupeleka katika Yerusalema, muji mutakatifu, akamusimamisha kwenye pembe la juu sana la hekalu, na kumwambia:

6“Kama wewe ni Mwana wa Mungu, ujitupe chini; kwa maana imeandikwa:

‘Mungu atawaamuru wamalaika wake

na watakubeba katika mikono yao,

kusudi muguu wako usijikwae juu ya jiwe.’ ”

7Yesu akamujibu: “Imeandikwa hivi vilevile: ‘Usimujaribu Bwana Mungu wako.’ ”

8Shetani akamupeleka tena mpaka juu ya mulima murefu, akamwonyesha falme zote za dunia na utajiri wao.

9Halafu akamwambia: “Nitakupa hivi vyote, kama ukipiga magoti mbele yangu na kuniabudu.”

10Lakini Yesu akamwambia: “Toka wewe, Shetani! Kwa maana imeandikwa: ‘Umwabudu Bwana Mungu wako na umutumikie yeye peke yake.’ ”

11Basi Shetani akamwacha Yesu, nao wamalaika wakakuja kushugulika naye.

Mwanzo wa mahubiri katika Galilaya(Mk 1.14-15; Lk 4.14-15)

12Yesu aliposikia kwamba Yoane ametiwa katika kifungo, akaenda zake Galilaya.

13Yeye akatoka Nazareti, akaenda kukaa Kapernaumu, pembeni ya ziwa la Galilaya, katika wilaya ya Zebuluni na ya Nafutali, kusudi yatimie

14maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii Isaya:

15“Inchi ya Zebuluni na ya Nafutali,

kufuata barabara inayokwenda kwenye ziwa, ngambo ya magaribi ya Yordani,

katika jimbo la Galilaya, inchi ya watu wa mataifa mengine.

16Watu hao wanaokaa katika giza,

mwangaza umewatokea!

Hao wanaoishi katika inchi yenye giza nzito sana ya lufu,

wameona mwangaza mukubwa.”

17Tangia wakati huo Yesu akaanza kuhubiri, akisema: “Mugeuke toka zambi zenu, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia!”

Yesu anawaita wavuvi wane wamufuate(Mk 1.16-20; Lk 5.1-11)

18Yesu alipokuwa akitembea pembeni ya ziwa la Galilaya, akawaona wavuvi wawili, waliokuwa wandugu wa tumbo, Simoni (aliyeitwa Petro) na ndugu yake Andrea. Walikuwa wakitupa nyavu katika ziwa.

19Yesu akawaambia: “Munifuate, nami nitawaweka kwa kazi ya kuopoa watu.”

20Mara moja wakaacha nyavu zao, na kumufuata.

21Yesu alipoendelea mbele kidogo, akawaona wandugu wengine wawili, Yakobo na Yoane, waliokuwa wana wa Zebedayo. Walikuwa ndani ya chombo pamoja na baba yao Zebedayo, wakitengeneza nyavu zao. Yesu akawaita.

22Na mara moja wakaacha chombo pamoja na baba yao, wakamufuata Yesu.

23Yesu alizunguka katika Galilaya yote akifundisha katika nyumba zao za kuabudia, akihubiri Habari Njema ya Ufalme. Aliponyesha watu waliokuwa na magonjwa yote na uzaifu wa kila namna.

24Habari zake zikavuma katika inchi yote ya Suria. Wakamuletea watu wote walioteswa na magonjwa mbalimbali na wenye maumivu ya kila namna, wenye pepo, wenye kifafa na wenye kupooza, naye Yesu akawaponyesha.

25Makundi mengi ya watu yakamufuata kutoka Galilaya, inchi ya Miji Kumi, Yerusalema, Yudea, na toka ngambo ya mashariki ya muto Yordani.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help