Ruta 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Boazi anamwoa Ruta

1Boazi akakwenda kwa nafasi ya kufanyia mukutano kule kwenye mulango wa muji, akaikaa chini. Kisha yule ndugu ya Elimeleki ambaye Boazi alikuwa amemutaja, akapita karibu na pale. Boazi akamwita, akasema: “Kuja, uikae hapa ndugu.” Basi yule mutu akakuja na kuikaa pale.

2Halafu Boazi akawaita wazee kumi wa muji, akawaomba wao vilevile waikae pale. Wakaikaa.

3Halafu Boazi akamwambia yule ndugu yake: “Sasa Naomi ambaye amerudi kutoka Moabu, anataka kuuzisha shamba ambalo lilikuwa la ndugu yetu Elimeleki.

4Basi mimi nimeona afazali nikujulishe habari hii. Sasa ikiwa unalitaka shamba hili, ulinunue mbele ya wazee wa watu wangu. Ikiwa unalitaka au haulitaki sema basi kwa sababu nafasi ya kwanza ya kulikomboa ni yako, na yangu ni ya pili.” Naye akasema: “Mimi nitalikomboa.”

5Boazi akasema: “Ni vizuri, lakini ukilinunua hilo shamba kutoka kwa Naomi, ni sherti umutwae vilevile Ruta wa Moabu, mujane ambaye ni jamaa wa marehemu, kusudi shamba hilo libaki katika jamaa ya yule marehemu.”

6Yule ndugu aliyekuwa wa karibu akajibu: “Ikiwa ni hivyo, sitalikomboa shamba hilo, kwa sababu inaonekana kwamba nitauharibu urizi wangu. Afazali nikupe wewe haki yangu ya kulikomboa, maana mimi siwezi kulikomboa.”

7Siku zile katika Israeli, kama watu walitaka kukomboa au kubadilishana kitu, ilikuwa desturi kwa mutu kuonyesha kitambulisho kwa kuvua kiatu chake na kumupa mwingine. Kwa kitambulisho hicho, Waisraeli walionyesha kwamba mambo yamesawazishwa.

8Basi, mutu huyo alimwambia Boazi: “Ulikomboe shamba”, kisha akavua kiatu chake na kumupa.

9Halafu Boazi akawaambia wazee na watu waliokuwa pale: “Leo ninyi ni washuhuda wangu. Mumeona kwamba nimenunua kutoka kwa Naomi, vyote vilivyokuwa vya Elimeleki, na vya Kiliona na Malona.

10Zaidi ya hayo, nimemupata Ruta wa Moabu mujane wa Malona, kusudi akuwe muke wangu. Mapatano haya yatafanya mali ya jamaa ya marehemu na ukoo wake kubakia kwa watu wake katika muji huu. Ninyi ni washuhuda.”

11Basi wazee waliokuwa kwenye mulango na watu wote waliokuwa pale wakajibu: “Ndiyo, sisi ni washuhuda. Yawe amufanye muke wako akuwe kama Rakeli na Lea, ambao wote wawili waliijenga nyumba ya Israeli. Nawe upate kustawi katika jamaa ya Efurata, ukuwe na sifa katika Betelehemu.

12Yawe akupatie watoto wengi kwa njia ya mwanamuke huyu, na jamaa yako ikuwe kama ya Peresi ambaye Tamari alimuzalia Yuda.”

Boazi na vizazi vyake

13Kwa hiyo, Boazi akamutwaa Ruta kuwa muke wake. Yawe akamujalia Ruta naye akapata mimba, akazaa mutoto mwanaume.

14Halafu wanawake wa muji huo wakamwambia Naomi: “Atukuzwe Yawe ambaye hakukuacha leo bila kuwa na ndugu wa kukutunza! Mujukuu wako akuwe mwenye sifa kubwa katika Israeli!

15Yeye atakurudishia uzima wako na atakutunza katika uzee wako. Mukwe wako ni wa lazima zaidi kwako kuliko watoto wa kiume saba, maana anakupenda na amekuzalia mujukuu huyu!”

16Basi Naomi akamutwaa mutoto yule akamuweka kwenye kifua chake na kuwa mulezi wake.

17Wanawake wajirani wakatangaza jina wakisema: “Mutoto amezaliwa kwa Naomi”, nao wakamwita jina la Obedi. Kisha Obedi akamuzaa Yese aliyemuzaa Daudi.

18Na hivi ndivyo vizazi vya Peresi: Peresi alimuzaa Hesironi,

19Hesironi akamuzaa Ramu, Ramu akamuzaa Aminadabu,

20Aminadabu akamuzaa Nasoni, Nasoni akamuzaa Salmoni,

21Salmoni akamuzaa Boazi, Boazi akamuzaa Obedi,

22Obedi akamuzaa Yese na Yese akamuzaa Daudi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help